Tuesday, February 25, 2014

Shetani Ni Nani? Ni Kiumbe Halisi?

WASOMI fulani wa kisasa wanasema kwamba Shetani si kiumbe halisi. Wanadai kwamba alibuniwa tu katika mawazo ya wanadamu. Ubishi wa aina hiyo umekuwapo kwa muda mrefu. “Ujanja wa hali ya juu wa Ibilisi,” akaandika Charles-Pierre Baudelaire, mshairi wa karne ya 19, “ni kutushawishi tuamini kwamba yeye hayuko.”


Je, Shetani ni kiumbe halisi? Ikiwa ndivyo, alitoka wapi? Je, yeye ndiye nguvu isiyoonekana inayosababisha matatizo ambayo wanadamu wanakabili? Unaweza kuepukaje kuathiriwa na uvutano wake?

Biblia Inasema Nini?
Biblia inamfafanua Shetani kuwa kiumbe halisi ambaye yuko katika makao ya roho. (Ayubu 1:6) Inatueleza kuhusu sifa zake za ukatili kutia ndani matendo yake ya uovu. (Ayubu 1:13-19; 2:7, 8; 2 Timotheo 2:26) Pia inasimulia mazungumzo kati ya Shetani na Mungu na pia kati yake na Yesu.—Ayubu 1:7-12; Mathayo 4:1-11.

Kiumbe huyo mwovu alitoka wapi? Muda mrefu kabla ya mwanadamu kuumbwa, Mungu alimuumba viumbe vya katika roho wanaoitwa Malaika, (Ayubu 38:4-7) Wote walikuwa wakamilifu na waadilifu. Hata hivyo, mmoja kati ya malaika hao aliuye julikana kwa jina la Lucifer akaja kuwa Shetani.

Malaika huyo hakuitwa Shetani alipoumbwa. Jina hilo ni la kumfafanua, na linamaanisha “Mpinzani; Adui; Mshtaki.” Alikuja kuitwa Shetani kwa sababu alichagua kumpinga Mungu.
Kiumbe huyo wa roho akaanza kukuza hisia za kiburi na za kushindana na Mungu. Alitaka wengine wamwabudu yeye. Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu alipokuwa hapa duniani, Shetani alimtaka Yesu ‘amfanyie tendo la ibada.’—Mathayo 4:9.

Shetani “hakusimama imara katika kweli.” (Yohana 8:44) Alidai kwamba Mungu alikuwa mwongo, ilhali kwa kweli, yeye ndiye alikuwa mwongo. Alimwambia Hawa kwamba angekuwa kama Mungu, lakini ni yeye hasa aliyetaka kuwa kama Mungu. Na kupitia mbinu zake za ujanja, alitosheleza tamaa yake yenye ubinafsi. Alimfanya Hawa amwone kuwa mkuu kuliko Mungu. Kwa kumtii Shetani, Hawa alimkubali kuwa mungu wake.—Mwanzo 3:1-7.


Kwa kuchochea uasi, malaika huyo ambaye awali alikuwa mwenye kuaminika akawa Shetani, yaani, mpinzani na adui ya Mungu na wanadamu. Neno “Ibilisi,” linalomaanisha “Mchongezi,” likawa pia jina la malaika huyo mwovu. Malaika huyo ambaye aliongoza katika kutenda dhambi mwishowe aliwachochea malaika wengine wakose kumtii Mungu na wamwasi kama yeye. (Mwanzo 6:1, 2; 1 Petro 3:19, 20) Kwa kufanya hivyo malaika hao waliwaongezea wanadamu shida. Kwa sababu ya kuiga njia za Shetani zenye ubinafsi, “dunia ikajaa jeuri.”—Mwanzo 6:11; Mathayo 12:24.

Uvutano wa Shetani Una Nguvu Kadiri Gani?
Mhalifu anaweza kupangusa alama za vidole ili asiache kitu chochote ambacho kitamtambulisha. Hata hivyo, polisi wanapofika, wanatambua kwamba iwapo uhalifu umetendwa, lazima kuwe na mhalifu. Shetani, “muuaji” wa zamani hujaribu kuficha kitu chochote ambacho kitamtambulisha. (Yohana 8:44; Waebrania 2:14) Alipozungumza na Hawa, Shetani alijificha kwa kutumia nyoka. Bado anajaribu kujificha leo. “Amezipofusha akili za wasioamini” ili watu wasitambue uvutano wake wenye nguvu umeenea kadiri gani.—2 Wakorintho 4:4.

Hata hivyo, Yesu alimfichua Shetani kuwa mhalifu mkuu anayeongoza ulimwengu huu wenye ufisadi tunamoishi. Alimwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 16:11) “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 5:19) Shetani hutumia “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani” ili ‘aipotoshe dunia nzima inayokaliwa.’ (1 Yohana 2:16; Ufunuo 12:9) Yeye ndiye yule ambaye wanadamu kwa ujumla humtii.

Kama ilivyokuwa kwa Hawa, wale wanaomtii Shetani, humfanya kuwa mungu wao. Hivyo, Shetani ndiye “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Matokeo ya utawala wake yanatia ndani unafiki na uwongo; vita, mnyanyaso na uharibifu; uhalifu, pupa na ufisadi.

Jinsi Unavyoweza Kuepuka Uvutano Wake
Biblia inaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda.” Kwa nini? Kwa sababu “adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama Simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Ingawa andiko hilo linatoa mwito wa ushindani, inatia moyo kujua kwamba wale tu ambao hawatunzi akili zao, yaani, wale ambao hawaendelei kukesha, ndio ‘watakaoshindwa akili na Shetani.’—2 Wakorintho 2:11.

Ni muhimu kwamba tukubali ukweli kuwa Shetani yuko na tumruhusu Mungu ‘atufanye kuwa imara’ na ‘kutufanya tuwe wenye nguvu.’ Katika njia hiyo ‘tunaweza kuchukua msimamo kumpinga Shetani’ na kusimama upande wa Mungu.—1 Petro 5:9, 10.

JE, UMEJIULIZA HIVI?
▪ Shetani alitoka wapi?—Ayubu 38:4-7; Yohana 8:44.
▪ Shetani huathiri ulimwengu kadiri gani?—Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9.
▪ Tunaweza kufanya nini ili kujilinda kutokana na mbinu za uovu za Shetani?—1 Petro 5:8-10.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW