Wednesday, December 16, 2015

UTAMU WA MAISHA YA NDOA

(Sehemu ya Kwanza)

NDOA NI NINI?Ndoa ni muungano kati ya mwanamke na mwanamume kuishi pamoja kama mume na mke muda wote wa maisha yao.
Kwa kuwa si kusudi letu kutafakari sheria za nchi zinasema nini kuhusu Ndoa, tungependa kujikita zaidi katika maana ya Ndoa kwa imani ya kikristo ambayo msingi wake unajengwa katika neno la Mungu. Hata hivyo tunapenda kuweka wazi kwamba Ndoa ni suala la kisheria, na ni muhimu sana kwa wanandoa kutambua kwamba zipo taratibu za kisheria zilizowekwa na serikali zinazosimamia masuala ya Ndoa. Kwa kuwa tumefanyika wana wa Mungu, mwenendo wetu na maisha yetu ya Ndoa yanaongozwa na imani yetu kwa Mungu na si sheria za kibinadamu.
Katika imani ya kikristo, Ndoa inaweza kutafsiriwa kama “AGANO KATI YA MWANAMKE NA MWANAMUME AMBAO WAMEKUSUDIA KWA HIARI KUAMBATANA NA KUISHI PAMOJA KAMA MKE NA MUME KWA SIKU ZOTE ZA MAISHA YAO.” Jambo la msingi kulitambua hapa ni kwamba Ndoa ya kikristo ni AGANO. Kuna tofauti kubwa kati ya kile kinachoitwa “AGANO” na “MKATABA” kimsingi agano ni zaidi ya mkataba kwa namna nyingi.
i) Wanaooana wawe wamekubaliana pasipo kulazimishwa na mtu.
ii) Ndoa ni ya mwanamke na mwanamume.
iii) Ni ndoa ya kudumu maishani.
Mpango na utaratibu wa MUNGU kwa wanandoa umewekwa wazi katika kitabu cha Mwanzo.
“Bwana MUNGU akasema si vema mtu huyu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufafana naye”. Mwanzo 2:18.
Hapa tunaona kuna suala la mamlaka katika ndoa, kwamba mke ni msaidizi.
“Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja”. Mwanzo 2:24.
Hapa tunaona kusudi la MUNGU katika suala la kuachana na kuambatana. Wanandoa wanatakiwa kuachana na wazazi wao katika maeneo matatu.
i) Kimwili – wawe na makazi yao wenyewe
ii) Kihisia – wategemeane na kutiana moyo na kusaidiana
iii) Kiuchumi – wajitegemee kwa mahitaji yao ya kila siku.
TUWE MAKINI, NDOA SI JAMBO LA MCHEZOKatika maisha ya mwanadamu, kuna mambo mawili yaliyo muhimu zaidi. La kwanza ni uamuzi wa kumfuataYesu na la pili ni uamuzi wa kuoa. Tafakari, kuoa si sawa na kununua shati. Ukilichoka na shati unaweza kununua nyingine lakini, huwezi kumwacha mke wako hata kama ukimchoka. Neno la Mungu linatuonya hatari ya kuoa mwanamke asiye mchaji wa Mungu; Twasoma: “Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika; kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi” (Mithali. 21:19). “Kutonatona daima siku ya mvua nyingi, na mwanamke mgomvi ni sawasawa; 16atakaye kumzuia huyo huuzuia upepo” (Mithali. 27:15-16). Zingatia: Pengine mtu atasema, “mchumba wangu ana imani tofauti, walakini tukioana nitamfundisha.”Lakini ikumbukwe mara nyingi, baada ya kufunga ndoa, watu hubadilika asitake kufundishwa tena.Tukumbuke mfalme Sulemani alikuwa na hekima kuliko wanadamu wote. Walakini, alipata hasara kubwa kwa sababu aliwapenda wanawake wageni wasio mcha Mungu na matokeo yake badala ya kuwafundisha imani yake, “yeye mwenyewe alinaswa na imani yao” (1Wafalme 11:1-4). Basi tujiulize, je sisi tunayo hekima kuliko Sulemani? Ni bora mtu amfundishe mchumba kabla hawajaoana na kuhakikisha kuwa ameamua kumfuata Bwana kwa moyo wake wote na si kwa sababu ya ndoa, ndipo atakapokuwa na amani na furaha katika ndoa yake. Tukumbuke faida moja wapo ya kuoa katika katisa ni kupata mke alifundishwa maadili na wanawake waliomtangulia; Twasoma: “Vivyo hivyo na wazee wa kike wawe na mwenendo wautakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia mvinyo nyingi, bali wafundishao mema; ili wawatie – wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na uwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi,kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe, ili neno la Mungu lisitukanwe” (Tit. 2:3-5). Hivyo ni dhahiri kuna faida kwa mkristo kujipatia mke aliyefunzwa maadili ya ndani ya kanisa. Zingatia: Kuna baadhi ya watu wamevutwa sana na maumbile au mambo ya kimwili ya wachumba wao lakini Biblia inatukumbusha kuchunguza mioyo yao zaidi kuliko sura ya nje; Tasoma: “Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye Bwana, ndiye atakayesifiwa” (Mithali. 31:30). “Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye; bali mke mwenye busara, mtu hupewa na Bwana” (Mithali 19:14). Je unazijua sifa za mke mwema? Mungu ameeleza peupe; Soma: (Mithali 31:10-31)
NDOA -TAASISI TAKATIFUNdoa yenye furaha na kuheshimika ni ile ambayo kila mmoja anafahamu na kutimiza wajibu wake katika ndoa kwa mujibu wa nafasi yake. Na hii ndio sharti la msingi kutupelekea kwenye ndoa yenye mafanikio.
i) Kumheshimu mwenzi wako kutokana na hadhi aliyonayo kama MUNGU alivyoagiza.
ii) Heshima inasaidia kutuepusha na ubinafsi na kuongozwa na hisia.
iii) Heshima katika ndoa inachochea mapenzi.
HATARI YA KUOANA NA ASIYE MCHAJI WA MUNGUKama tulivyojifunza hako juu hatari moja wapo ya kuoana na wasio wachaji wa Mungu ni kuishia kuvutwa na upotofu na kuanguka kiimani; Twasoma:”Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya Bwana juu yenu, naye atakuangamiza upesi” (Kumbukumbu 7:4). Na hayo ndiyo yaliyomapata Suleima kama tulikwisha kuoona; Soma tena: (1 Wafalme 11:1-4) Tukumbuke ikiwa tutaanguka katika uovu, mwisho wake utakuwa ni kutupwa katika hukumu (adhabu ya milele); Twasoma: “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uachafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui,ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayo fanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Galatia 5:19-21) “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauwaji, na wazizi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili” (Ufunuo 21:8) “Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani hilo ziwa la moto. Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.” (Ufunuo 20:14- 15) Zingatia: Ndoa ni kifungo hivyo tukumbuke tunapoana hatuna ruhusa ya kuacha hata kama wenzi wetu ni wabaya vipi; Twasoma: “Lakini wale waliokwisha kuoana nawagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; lakini ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.” (1 Wakorintho 7:10-11) “Mwanamke hufungwa maadamu mumewe yu hai, lakini ikiwa mumwe amefariki, yu huru kuolewa na mtu ye yote amtakaye; katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39)
Hivyo ni dhahiri tunaaswa kuwa makini tunapo wachagua wenzi wetu, tukikumbuka ya kuwa kifungo cha ndoa ni mpaka kifo.
NDOA NI KUTOA1. Ndio sio mkataba wa kijamii bali agano la kiroho. Waefeso 5:31-33 Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja. Siri hiyo ni kubwa, ila mimi nanena habari ya KRISTO na Kanisa. Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe, wala mke asikose kumstahi mumewe.
Hapa tunajifunza
i) Ndoa ni fumbo la ajabu la kiroho linalowaunganisha watu wawili, mwanamume na mwanamke (mst.31)
ii) Ndoa ya kikristo inaliganishwa na uhusiano uliopo kati ya KRISTO na Kanisa (mst.32)
iii) Mpango wa MUNGU katika ndoa unahitaji upendo wa kujitoa sadaka kama KRISTO anavyofanya kwa Kanisa (mst.33)
2. Ndoa ya Kikristo ni kujitoa sio kupokea. Wafilipi 2:3-4 Msitende neno lolote kwa kushindana wala kwa majivuno, bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenzie kuwa bora kuliko nafsi yake mwenyewe. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.
Hapa tunajifunza
i) Kutokuwa wabinafsi
ii) Unyenyekevu
iii) Roho ya kutoa na kujitoa.
Wewe mume/mke, mahusiano yako na mwenzi wako yakoje? Unampenda mwenzi wako kama KRISTO anavyolipenda Kanisa lake? Kama wewe ni mmojawapo wa wasiofuata kielelezo cha KRISTO katika ndoa usijisikie vibaya kwani hakuna aliye mkamilifu. Hata hivyo wajibu huu haukwepeki kwani ni agizo la MUNGU na lazima kutii maagizo yake, kumpenda MUNGU kwa moyo waklo wote na kwa roho yako yote na kwa akili zako zote na kwa nguvu zako zote. Na kumpenda jirani yako kama nafsi yao. Marko 12:30-31. Hivyo, hii ni nafasi yako ya kumwonyesha mwenzi wako upendo ambao wa muda mrefu ameukosa, upendo ambao KRISTO ameuonyesa kwa kanisa lake.
Max Shimba Ministries

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW