Sunday, January 29, 2017

YESU ANAKUPENDA (SEHEMU YA KWANZA)

Image may contain: text
Swali la muhimu linazuka: Je, Mungu anampenda kila mmoja wetu?
Baadhi ya watu wanakubali kwamba Mungu anawapenda wanadamu kwa ujumla kama andiko la Yohana 3:16 linavyosema. Lakini wanahisi hivi: ‘Mungu hawezi kamwe kunipenda mimi.’
Shetani Ibilisi anataka sana tuamini kwamba Yesu hatupendi wala hatuthamini. Kwa upande mwingine, Yesu anatuhakikishia kuwa anamthamini kila mmoja wa watumishi wake waaminifu hata kama tunafikiri hatupendwi au hatuthaminiwi.
Kwa mfano, fikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:29-31. Yesu alitoa mfano huu ili kuonyesha kwamba wanafunzi wake wana thamani: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” Hebu fikiria jinsi wasikilizaji wa Yesu katika karne ya kwanza walivyoyaelewa maneno hayo.
Katika siku za Yesu, Shore alikuwa ndege wa bei rahisi sana aliyenunuliwa ili kuliwa. Mtu aliyelipa sarafu moja ya thamani ndogo sana, alipewa Shore wawili. Lakini kulingana na andiko la Luka 12:6, 7, baadaye Yesu alisema kwamba mtu aliyelipa sarafu mbili, alipewa shore watano badala ya shore wanne. Shore mmoja aliongezwa kana kwamba hakuwa na thamani yoyote. Huenda ndege hao hawakuwa na thamani machoni pa wanadamu, lakini Muumba aliwaonaje? Yesu alisema: “Hakuna hata mmoja wao [hata yule aliyeongezwa] hupata kusahaulika mbele ya Mungu.” Sasa huenda tumeanza kuelewa alilomaanisha Yesu. Ikiwa Mungu anamthamini sana shore mmoja, namna gani mwanadamu! Kama Yesu alivyosema, Mungu Baba anatujua vizuri sana. Kwani, hata nywele za kichwa chetu zimehesabiwa zote!
Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hakutia chumvi aliposema kwamba nywele za kichwa chetu zimehesabiwa?
Huenda wengine wakafikiri kwamba Yesu alitia chumvi. Hata hivyo, hebu fikiria ufufuo. Ni lazima Mungu Baba awe anatujua vizuri sana ili aweze kutuumba upya! Anatuthamini sana hivi kwamba anakumbuka kila jambo, hata chembe zetu za urithi, kumbukumbu, na ujuzi wetu wote. Kichwa cha mtu huwa na nywele 100,000 hivi, kwa hiyo kuhesabu nywele za vichwa vyetu ni jambo rahisi sana ikilinganishwa na kukumbuka mambo hayo yote. Bila shaka, maneno hayo ya Yesu yanatuhakikishia kabisa kwamba Mungu Baba anamjali kila mmoja wetu.
Kisa cha Mfalme Yehoshafati kinaonyeshaje kwamba Mungu hutafuta mema ndani yetu ingawa sisi si wakamilifu?
Biblia hufunua jambo lingine linalotuhakikishia kwamba Mungu anatupenda. Yeye hutafuta na huthamini mema yaliyo ndani yetu. Kwa mfano, fikiria Mfalme Yehoshafati aliyekuwa mwema. Mfalme huyo alipotenda jambo la kipumbavu, nabii wa Mungu alimwambia hivi: “Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa BWANA.” Ulikuwa ujumbe wenye kuogofya kama nini! Lakini ujumbe wa Mungu haukukomea hapo. Uliendelea kusema hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:1-3) Kwa hiyo, hasira adilifu ya Mungu haikumzuia asione “mema” yaliyokuwa ndani ya Yehoshafati. Inatia moyo sana kujua kwamba Mungu wetu hutafuta mema ndani yetu hata ingawa sisi si wakamilifu.
Kumbuka kuwa Yesu anakupenda.
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.
Max Shimba Ministries @ 2015

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW