Saturday, May 13, 2017

JE, TUNAWEZA AMINI UNABII NA MANABII WA SIKU ZA MWISHO? SOMO LA PILI

No automatic alt text available.
Somo la Pili:
Tunaanza na mwanamume ambaye anaheshimiwa na Waislamu, Wakristo, na Wayahudi. Alikuwa Mwebrania aliyeishi kuanzia mwaka wa 2018 hadi 1843 K.W.K.* Aliitwa Abrahamu.*
Abrahamu alihusika moja kwa moja katika baadhi ya unabii ulioandikwa mapema sana katika Biblia—unabii unaotuhusu sisi pia leo. Kulingana na kitabu cha Biblia cha Mwanzo, unabii huo ulitaja mambo yafuatayo:
(1) Uzao wa Abrahamu ungekuwa taifa kubwa.
(2) Ili wawe taifa kubwa, wangekuwa watumwa katika nchi ya kigeni.
(3) Wangekombolewa na kumiliki nchi ya Kanaani. Acheni tuchunguze mambo hayo kwa undani zaidi.
Unabii Mbalimbali Wenye Kustaajabisha
UNABII WA KWANZA:
“Nitafanya taifa kubwa kutokana nawe [Abrahamu].”—Mwanzo 12:2.
Utimizo: Wazao wa Abrahamu kupitia Isaka na Yakobo (ambaye pia anaitwa Israeli) walikuja kufanyiza taifa la kale la Israeli—taifa lililojitawala likiwa na wafalme wake.
Historia inafunua nini?
● Biblia inaonyesha waziwazi ukoo wa Abrahamu, kupitia Isaka, Yakobo, na wana 12 wa Yakobo. Nasaba hiyo ilitia ndani wafalme wengi waliotawala katika Israeli au Yuda. Kati ya watawala hao, 17 wanatajwa katika vitabu ambavyo si vya Biblia, na hilo linapatana na maandishi ya Biblia ya jinsi wazao wa Abrahamu kupitia Isaka na Yakobo walivyokuja kuwa taifa.*
UNABII WA PILI:
“Uzao wako [Abrahamu] utakuwa mkaaji mgeni katika nchi isiyokuwa yao, nao watawatumikia watu wale . . . Lakini katika kizazi cha nne watarudi hapa.”—Mwanzo 15:13, 16.
Utimizo: Kwa sababu ya njaa kali huko Kanaani, vizazi vinne vya wazao wa Abrahamu viliishi nchini Misri, kwanza wakiwa wakaaji wageni lakini baadaye wakiwa watumwa waliolazimishwa kutengeneza matofali kutokana na udongo na nyasi. Kwa mfano, tunaweza kufikiria kuhusu ukoo mmoja—ule wa Lawi, kitukuu wa Abrahamu, aliyehamia Misri pamoja na baba yake aliyezeeka—vizazi vyake vinne ni (1) Lawi, (2) mwana wake Kohathi, (3) mjukuu wake Amramu, na (4) kitukuu wake Musa. (Kutoka 6:16, 18, 20) Katika mwaka wa 1513 K.W.K., Musa aliwaongoza Waisraeli kutoka Misri.—Ona orodha ya matukio iliyo hapo chini pamoja na sanduku “Kuweka Wakati kwa Usahihi.”
Historia inafunua nini?
● Kulingana na James K. Hoffmeier, profesa wa Agano la Kale na Uchimbuaji wa Vitu vya Kale vya Mashariki ya Kati, maandishi ya Misri na uthibitisho wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa unaonyesha kwamba wazao wa Shemu (kama vile Waebrania wa kale) waliruhusiwa kuingia Misri wakiwa na mifugo yao kulipokuwa na njaa. Lakini je, Waisraeli waliwahi kuwa watumwa huko, waliolazimishwa kutengeneza matofali?
● Ingawa maandishi ya Wamisri hayawataji Waisraeli moja kwa moja, michoro katika makaburi ya Misri na vitabu vya kukunjwa vinathibitisha kwamba Wamisri waliwatumia wageni kutengeneza matofali kutokana na udongo na nyasi. Sawa tu na maandishi ya Biblia, maandishi ya Wamisri yanaonyesha kwamba wasimamizi wa kazi waliandika rekodi za kuonyesha idadi ya matofali yaliyotengenezwa. (Kutoka 5:14, 19) Hoffmeier anasema: “Maandishi ya Misri yanathibitisha kwamba wageni walilazimishwa kuwa watumwa . . . katika kipindi kilekile ambacho Waisraeli walikuwa wakikandamizwa. Hivyo basi, inaonekana kwamba ni sahihi kusema kuwa Waebrania wa kale waliingia Misri . . . wakati wa njaa na baadaye wakalazimishwa kuwa watumwa.”
UNABII WA TATU:
‘Nitawapa wazao wako nchi yote ya Kanaani.’—Mwanzo 17:8.
Utimizo: Ingawa Musa aliongoza taifa changa la Israeli kutoka Misri, Yoshua mwana wa Nuni ndiye aliyewaongoza kuingia nchi ya Kanaani katika mwaka wa 1473 K.W.K.
Historia inafunua nini?
● Ingawa huenda wachimbuaji wa vitu vya kale wakatoa tarehe zinazotofautiana, “tunapaswa kuzungumzia hasa kuingia kwa Waisraeli katika nchi ya Kanaani, na kukaa humo,” anaandika K. A. Kitchen, profesa aliyestaafu wa mambo ya Misri.
● Biblia inaonyesha kwamba Yoshua ‘aliteketeza jiji la Kanaani la Hasori katika moto.’ (Yoshua 11:10, 11) Katika magofu ya jiji hilo, wachimbuaji wa vitu vya kale wamechimbua mahekalu matatu ya Wakanaani ambayo yalikuwa yameharibiwa kabisa. Pia walipata uthibitisho kwamba jiji hilo liliteketezwa katika miaka ya 1400 K.W.K. Mambo hayo hakika yanapatana na Biblia.
● Jiji lingine la Kanaani linalostahili kufikiriwa ni Gibeoni, lililoko kilomita 9.6 hivi kutoka Yerusalemu. Wachimbuaji wa vitu vya kale waligundua jiji hilo walipopata jina lake likiwa limechongwa juu ya vishikio 30 hivi vya mitungi. Tofauti na wakaaji wa Hasori, Wagibeoni wa kale walikuwa wamefanya amani pamoja na Yoshua. Kwa sababu hiyo, akawafanya kuwa “watekaji wa maji.” (Yoshua 9:3-7, 23) Kwa nini aliwapa mgawo huo? Masimulizi yanayopatikana katika 2 Samweli 2:13 na Yeremia 41:12 yanaonyesha kwamba Gibeoni lilikuwa eneo lenye maji mengi. Basi kupatana na simulizi hilo la Biblia, kitabu Archaeological Study Bible, New International Version kinasema: “Kitu chenye kutokeza zaidi katika eneo la Gibeoni ni kwamba kulikuwa na maji mengi sana: chemchemi moja kubwa na saba ndogo.”
● Maandishi mengi ya kihistoria yamethibitisha kwamba watu wengi wanaotajwa katika Biblia waliwahi kuishi. Kama ilivyotajwa awali, orodha hiyo inatia ndani majina ya wafalme 17 waliokuwa wazao wa Abrahamu na wakatawala Israeli au Yuda. Kati yao Ahabu, Ahazi, Daudi, Hezekia, Manase, na Uzia. Kwa wazi, kuwepo kwa familia za kifalme kunakazia hoja ya kwamba taifa linaloitwa Israeli liliingia katika nchi ya Kanaani na kuimiliki.
● Mnamo 1896, wachunguzi walipata Jiwe la Merneptah huko Thebesi, Misri. Jiwe hilo lina maandishi yanayomsifu Farao Merneptah kwa kampeni yake ya kijeshi ya kuingia Kanaani karibu na mwaka wa 1210 K.W.K. Hayo ndiyo maandishi ya kwanza yasiyo ya Biblia yanazungumza kuhusu Israeli, jambo linalounga mkono hata zaidi kuwepo kwa taifa hilo.
Faida ya Kuwa na Habari Hususa
Kama vile ambavyo tumeona, Biblia ina habari nyingi hususa kuhusu watu, mahali, na matukio. Habari hizo hususa zinatuwezesha kuilinganisha Biblia na maandishi mengine, na hivyo kutusaidia kuthibitisha utimizo wa unabii wa Biblia. Kuhusiana na Abrahamu na uzao wake, mambo hakika yanaonyesha kwamba ahadi za Mungu zilitimizwa—uzao wa Abrahamu ulikuwa taifa, walifanywa kuwa watumwa nchini Misri, na baadaye waliimiliki nchi ya Kanaani. Mambo yote hayo yanatukumbusha maneno ya Petro, mwandikaji mmoja wa Biblia, ambaye alisema hivi kwa unyenyekevu: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:21.
Baada ya Israeli kuimiliki nchi ya Kanaani, historia ya taifa hilo ilianza kubadilika sana, na kukawa na matokeo mabaya sana. Matokeo hayo mabaya yalitabiriwa pia na waandikaji wa Biblia, kama toleo linalofuata litakavyoonyesha.
“K.W.K.” inamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.”
Mwanzoni Abrahamu aliitwa Abramu. Jina la Abrahamu alipewa baada ya kuitwa Baba wa Mataifa yote.
Ona 1 Mambo ya Nyakati 1:27-34; 2:1-15; 3:1-24. Wakati wa utawala wa Rehoboamu, mwana wa Mfalme Sulemani, taifa la Israeli liligawanywa kuwa ufalme wa kaskazini na ufalme wa kusini. Baada ya hapo, wafalme wawili walitawala Israeli wakati uleule.—1 Wafalme 12:1-24.
BARAKA KWA “MATAIFA YOTE”
Mungu aliahidi kwamba watu wa “mataifa yote” wangejibariki kupitia kwa uzao wa Abrahamu. (Mwanzo 22:18) Sababu kuu ambayo Mungu alifanya uzao wa Abrahamu uwe taifa ilikuwa kutokeza Masihi, ambaye angetoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu wote.* Kwa hiyo, ahadi ya Mungu kwa Abrahamu inakuhusu! Yohana 3:16 inasema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”
Unabii unaohusiana moja kwa moja na utambulisho wa Masihi utazungumziwa katika Sehemu ya 3 na ya 4 ya mfululizo huu.
KUWEKA WAKATI KWA USAHIHI
Mfano unaoonyesha umuhimu wa Biblia kuweka wakati kwa usahihi unaonyeshwa katika 1 Wafalme 6:1, andiko linaloonyesha wakati ambapo Mfalme Sulemani alianza kazi ya ujenzi wa hekalu huko Yerusalemu. Tunasoma hivi: “Ikawa kwamba katika mwaka wa 480 [miaka 479 kamili] baada ya wana wa Israeli kutoka katika nchi ya Misri, katika mwaka wa nne [wa utawala wa Sulemani], katika mwezi wa Zivu, yaani, mwezi wa pili, baada ya Sulemani kuwa mfalme juu ya Israeli, akaanza kumjengea Yehova nyumba.”
Mfuatano wa matukio ya Biblia unaonyesha kwamba mwaka wa nne wa utawala wa Sulemani ulikuwa mwaka wa 1034 K.W.K. Mwaka huo unatusaidia kufahamu wakati ambapo Waisraeli walitoka Misri kwani unapohesabu kurudi nyuma miaka 479 kamili inatufikisha kwenye mwaka wa 1513 K.W.K.
ABRAHAMU NI MTU ANAYETAJWA KATIKA HISTORIA
● Mabamba ya udongo ya mapema ya milenia ya pili K.W.K. yanaorodhesha majiji yaliyo na majina ya watu wa ukoo wa Abrahamu. Majiji hayo yanatia ndani Pelegi, Serugi, Nahori, Tera, na Harani.—Mwanzo 11:17-32.
● Kwenye Mwanzo 11:31, tunasoma kwamba Abrahamu na familia yake walihama kutoka “Uru la Wakaldayo.” Magofu ya jiji hilo yaligunduliwa kusini-mashariki mwa Iraki. Biblia pia inasema kwamba baba ya Abrahamu, Tera, alikufa katika jiji la Harani, ambalo huenda sasa liko nchini Uturuki, na kwamba mke wa Abrahamu, Sara, alifia huko Hebroni, ambalo ni moja kati ya majiji ya zamani zaidi ambayo bado watu wanaishi katika Mashariki ya Kati.—Mwanzo 11:32; 23:2.
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
ORODHA YA MATUKIO YANAYOHUSU UZAO WA ABRAHAMU NA KUTOKA KWA WAISRAELI MISRI
(K.W.K.)
1843 Abrahamu anakufa
Vizazi vinne vya
wazao wa Abrahamu
Lawi
1728 Yakobo anahamisha
familia Misri
1711 Yakobo anakufa Kohathi
1657 Yosefu anakufa Amramu
1593 Musa anazaliwa
1513 Musa anawaongoza
Waisraeli kutoka Misri
1473 Musa anakufa.
Yoshua anawaongoza
Waisraeli kuingia
Kanaani
Kipindi cha Waamuzi
1117 Samweli anatia mafuta
Sauli kuwa mfalme wa kwanza wa Israeli
1107 Daudi anazaliwa
1070 Daudi anakuwa mfalme wa Israeli
1034 Sulemani anaanza kujenga hekalu
Jiwe hili la ushindi lenye maneno “Nyumba ya Daudi,” ni moja kati ya maandishi 17 yanayowataja wafalme waliokuwa wazao wa Abrahamu na waliotawala Israeli au Yuda
[Hisani]
© Israel Museum, Jerusalem/The Bridgeman Art Library International
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW