Sunday, May 14, 2017

JE, TUNAWEZA AMINI UNABII NA MANABII WA SIKU ZA MWISHO? Somo la Tatu:

Image may contain: 1 person, text
Katika makala iliyotangulia ya mfululizo huu, tulichunguza sehemu tatu za unabii unaopatikana katika Biblia kuhusu uzao wa Abrahamu. Uthibitisho unaonyesha kwamba Mungu alitimiza unabii huo kupitia taifa la Israeli ambalo lilifanyizwa na wazao wa Abrahamu.
Babiloni la kale lilikuwa taifa lingine lililotimiza sehemu muhimu katika historia ya Biblia, hasa katika karne ya saba K.W.K. Acheni tuchunguze sehemu tatu za unabii wa Biblia kuhusu taifa hilo na tuone ikiwa kuna uthibitisho kwamba unabii huo mbalimbali uliongozwa na roho ya Mungu.
Nabii Musa aliwaonya watu wa Israeli ya kale hivi: ‘Ikiwa mtamsahau Mungu wenu hata kidogo nanyi mfuate miungu mingine na kuitumikia na kuiinamia, ninyi mtaangamia kabisa.’ (Kumbukumbu la Torati 8:19; 11:8, 9) Hata hivyo, Waisraeli walimwasi Mungu mara nyingi kwa kujihusisha katika ibada ya sanamu.—1 Wafalme 14:22-24.
Baada ya muda, Mungu alichoka kuwaonyesha subira, na akaruhusu taifa lake lililoasi lishindwe na Wababiloni. Majeshi ya Babiloni yakiongozwa na Mfalme Nebukadneza—au Nebukadreza—yalikuja dhidi ya Israeli na kulizingira Yerusalemu. Je, kuzingira huko kulikuwa na umuhimu wowote? Acheni tuchunguze kile ambacho nabii Yeremia aliandika miaka 20 hivi kabla ya tukio hilo.—Yeremia 25:1.
UNABII WA KWANZA:
“Kwa sababu [Waisraeli] hamkuyatii maneno yangu [Mungu], tazama, ninatuma . . . Nebukadreza mfalme wa Babiloni, . . . , nami nitawaleta wao [Wababiloni] juu ya nchi hii na juu ya wakaaji wake . . . Na nchi hii yote itakuwa mahali palipoharibiwa, kitu cha kushangaza, na mataifa haya yatamtumikia mfalme wa Babiloni miaka 70.”—Yeremia 25:8-11.
UTIMIZO:
Baada ya kulizingira jiji hilo kwa muda mrefu, Nebukadneza alilipora na kuliharibu Yerusalemu katika mwaka 607 K.W.K. Pia aliyashinda majiji mengine ya Yudea, kutia ndani Lakishi na Azeka. (Yeremia 34:6, 7) Aliwahamisha waokokaji wengi na kuwapeleka Babiloni ambako walikaa wakiwa mateka kwa miaka 70.
Historia inafunua nini?
● Biblia inaonyesha kwamba Nebukadneza ndiye aliyekuwa mfalme wa Babiloni karibu na wakati ambapo Yerusalemu liliharibiwa. Vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinaunga mkono kile ambacho Biblia inasema kuhusu kuwapo kwake. Jiwe fulani la shohamu lililo na mchongo limewekwa huko Florence, Italia. Sehemu fulani ya maandishi yaliyo juu ya jiwe hilo yanasema hivi: “Kwa heshima ya Merodaki, bwana wake, Nebukadneza, mfalme wa Babiloni, alipokuwa hai aliagiza hili lijengwe.” Nebukadneza alitawala kuanzia mwaka wa 624 hadi 582 K.W.K.
● Kitabu The Bible and Archaeology kinasema kwamba mambo yafuatayo yamethibitishwa baada ya eneo la Lakishi kuchimbuliwa na kufanyiwa uchunguzi: “Uharibifu wa mwisho ulikuwa wenye jeuri, na moto ulioharibu jiji [Lakishi] ulikuwa mkali sana hivi kwamba mawe ya chokaa yaligeuzwa kuwa ungaunga wa chokaa.”
UNABII WA PILI:
“Kupatana na kutimia kwa miaka 70 katika Babiloni [mimi Mungu] nitawakazia ninyi fikira [Wayahudi walio uhamishoni], nami nitawatimizia neno langu jema kwa kuwarudisha tena mahali hapa [nchi ya Yuda].”—Yeremia 29:10.
UTIMIZO:
Baada ya miaka 70 ya uhamisho, kuanzia 607 hadi 537 K.W.K., Mfalme Koreshi wa Uajemi aliwaachilia Wayahudi waliokuwa utekwani na kuwaruhusu warudi nyumbani kwao ili wakajenge upya hekalu huko Yerusalemu.—Ezra 1:2-4.
Historia inafunua nini?
● Je, Waisraeli waliendelea kuwa mateka Babiloni kwa miaka 70 kama Biblia ilivyotabiri? Hebu ona maelezo ya Ephraim Stern, ambaye ni mmoja wa wataalamu wakuu wa wachimbuaji wa vitu vya kale nchini Israel. “Kuanzia mwaka wa 604 K.W.K. hadi 538 K.W.K.—hakuna uthibitisho unaoonyesha kuwa kuna mtu aliyeishi nchini Israeli. Wakati huo, hakuna hata mji mmoja ulioharibiwa na Wababiloni unaoonekana kuwa ulikuwa na watu.” Kipindi hicho ambacho hakukuwa na mtu katika eneo lililoshindwa kinapatana sana na uhamisho wa Waisraeli kupelekwa Babiloni kuanzia 607 hadi 537 K.W.K.—2 Mambo ya Nyakati 36:20, 21.
● Mataifa ya kale katika eneo lote la Mesopotamia yalikuwa na kawaida ya kuandika kwenye mabamba yaliyofanyizwa kwa udongo laini. Bamba moja gumu linalojulikana kama Mwanzi wa Koreshi, linakadiriwa kuwa la mwaka wa 539 K.W.K. hivi, mwaka uleule ambao Mfalme Koreshi wa Uajemi aliipindua Milki ya Babiloni. Sehemu fulani ya maandishi hayo inasema hivi: “Mimi ni Koreshi, . . . mfalme wa Babiloni.” Maandishi hayo yanaendelea kusema hivi: “Nilirudisha kwenye majiji matakatifu [ambayo tayari yalikuwa yametajwa] yaliyokuwa upande ule mwingine wa Tigri, majengo matakatifu ambayo yamekuwa magofu kwa muda mrefu sana, [na] sanamu zilizokuwepo ndani yake . . . Mimi (pia) niliwakusanya wakazi wake wote (wa awali) na nikawarudishia makao yao.”
Maandishi hayo yanapatana na unabii wa Biblia unaosema kwamba Wayahudi waliohamishwa wangerudishwa nyumbani kwao—unabii uliokuwa umerekodiwa miaka 200 hivi mapema.
UNABII WA TATU:
“Babiloni, lile pambo la falme, uzuri wa fahari ya Wakaldayo, litakuwa kama wakati Mungu alipoangamiza Sodoma na Gomora. Hatakaliwa kamwe.”—Isaya 13:19, 20.
UTIMIZO:
Jambo lenye kushangaza lilitukia wakati serikali kubwa ya ulimwengu ya Babiloni ilipoangushwa na jeshi la Wamedi na Waajemi katika mwaka wa 539 K.W.K.* Jiji hilo halikuwahi kurudia hali yake ya awali. Badala yake, lilianza kuzorota na mwishowe likawa mahame yenye ukiwa “bila mkaaji.”—Yeremia 51:37.
Historia inafunua nini?
● Kutoweka kwa Babiloni kulikuwa kamili kabisa hivi kwamba msomi Tom Boiy anazungumza kuhusu “wanahistoria na wasafiri kutoka nchi za Ulaya wa karne ya kumi na sita hadi kumi na nane” ambao walifahamu umuhimu wa jiji hilo lakini walipata matatizo kutambua “mahali hususa lilipokuwa.”
● Katika mwaka wa 1919, H. R. Hall, msimamizi wa kitengo cha Vitu vya Kale vya Misri na Ashuru katika Jumba la Makumbusho la Uingereza alifafanua Babiloni katika njia hii: “Ni rundo la mawe ya kuta zilizoangushwa . . . zilizofunikwa kwa mchanga.”
Tunaweza kufikia mkataa gani kutokana na uchunguzi wetu kuhusu utimizo wa unabii huo mbalimbali? Inapaswa kuwa wazi kwamba tena na tena Biblia imethibitika kuwa kitabu cha unabii sahihi. Ujumbe wa kinabii kuhusu Yuda na Babiloni ulitimizwa kabisa kama ilivyotabiriwa!
Yerusalemu liliharibiwa kwa sababu watu hawakutii maonyo kutoka kwa Mungu kwamba waache mwenendo usiompendeza Mungu. Baada ya miaka 70 iliyotabiriwa ya kuwa mateka huko Babiloni, Waisraeli waliruhusiwa kurudi nyumbani huko Yerusalemu. Jiji la kale la Babiloni liliharibiwa kama tu ilivyokuwa imefafanuliwa, na hadi leo hakuna mtu anayeishi katika eneo hilo. Lakini huo ni baadhi tu ya unabii mwingi unaopatikana katika Biblia.
Makala yetu inayofuata itazungumzia jinsi matukio katika karne ya kwanza W.K. yalivyotabiriwa mapema sana. Unabii huo uliotimizwa unatufanya tuwe na hakika kwamba Biblia ni sahihi.
Isaya alikuwa pia ametabiri miaka 200 hivi mapema kwamba Wamedi wangetimiza sehemu kubwa katika vita dhidi ya Babiloni.—Ona Isaya 13:17-19; 21:2.
ORODHA YA MATUKIO YANAYOHUSU BABILONI
m. 732 K.W.K.: Isaya
anatabiri kuanguka kwa Babiloni
(K.W.K.)
647 Yeremia anawekwa rasmi kuwa nabii
632 Babiloni inaishinda Ashuru
625 Nebukadneza anaanza kutawala
617 Danieli na Ezekieli wanahamishwa hadi Babiloni
607 Nebukadneza Wayahudi wanapelekwa anaharibu Yerusalemu utekwani Babiloni kwa miaka 70
582 Utawala wa Nebukadneza unakoma
539 Babiloni linaangushwa na Wamedi na Waajemi
537 Wayahudi waliokuwa utekwani wanaruhusiwa kurudi Yerusalemu
Barua za Lakishi zinaunga mkono ufafanuzi wa Yeremia kuhusu uvamizi wa Babiloni dhidi ya Yuda
Maandishi kwenye Mwanzi wa Koreshi yanaonyesha sera ya Koreshi ya kuwarudisha mateka nyumbani kwao
Page 12, Lachish Letter: Photograph taken by courtesy of the British Museum; page 13, Cyrus Cylinder: © The Trustees of the British Museum
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW