Saturday, May 13, 2017

JE, TUNAWEZA AMINI UNABII NA MANABII WA SIKU ZA MWISHO? SOMO LA KWANZA

Image may contain: one or more people and text
Somo la Kwanza:
Karibu kila kitabu cha Bibilia kiko na unabii kuhusu nyakati za mwisho. Kuzungumzia huu unabii na kuupanga waweza kuwa kazi ngumu.
Miaka 2,000 hivi iliyopita, Biblia ilitabiri kwamba hali mbaya za ulimwengu zingefikia mwisho wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Hatumaanishi “mwisho wa dunia” kama watu wengi wanavyofikiri utatukia. Badala yake, Biblia inaeleza kuhusu mfuatano wa matukio na mitazamo, au dalili, ambayo ingetokea katika kipindi cha wakati unaoitwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba wanapoona “mambo hayo yakitukia” wajue kwamba kitulizo kitafuata punde baadaye. (Luka 21:31) Fikiria baadhi ya unabii unaoonyesha kwamba wakati wetu ni wa pekee.
UNABII WA KWANZA:
“Taifa litasimama kupigana na taifa.”—Mathayo 24:7.
Utimizo: Katika miaka ya mapema ya karne ya 20, wengi walikuwa wakitazamia kwamba amani ingeendelea kuwapo. Ulimwengu ulishtuka Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipozuka, na enzi ya vita visivyo na kifani ikaanza. Kama kitabu cha Ufunuo kilivyotabiri, amani iliondolewa “duniani ili [wanadamu] wauane.”—Ufunuo 6:4.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
“Kutokea kwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu katika mwaka wa 1914 kuliashiria mwisho wa enzi moja na kuanza kwa enzi nyingine.”—The Origins of the First World War, kilichochapishwa mnamo 1992.
Ingawa idadi ya watu waliokufa wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu haiwezi kujulikana kabisa, ensaiklopedia moja inakadiria kwamba idadi ya wanajeshi waliokufa ni 8,500,000.
Watu wengi zaidi walikufa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, kwani inasemekana kuwa kati ya wanajeshi na raia milioni 35 hadi milioni 60 waliuawa.
Kati ya mwisho wa vita vya pili vya ulimwengu na mwaka wa 2010, kumekuwa na vita 246 katika maeneo 151 ulimwenguni pote.
UNABII WA PILI:
“Kutakuwa na upungufu wa chakula.”— Mathayo 24:7.
Utimizo: Njaa ilisababisha zaidi ya vifo milioni 70 katika karne ya 20 na bado ni tatizo kubwa ulimwenguni pote.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
Kulingana na Umoja wa Mataifa, njaa ndiyo tisho kubwa zaidi kwa afya ulimwenguni, na mtu 1 kati ya 7 ulimwenguni hana chakula cha kutosha.
“Leo upungufu wa chakula hausababishwi na kukosekana kwa mavuno ya kipindi fulani kwa sababu ya hali mbaya ya hewa ya muda, bali unasababishwa na mambo manne yanayoendelea kwa muda mrefu: kuongezeka ghafula kwa idadi ya watu, kupotea kwa udongo wa juu, kuenea kwa upungufu wa maji, na kuongezeka kwa kiwango cha joto.”—Scientific American.
UNABII WA TATU:
“Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi.”— Luka 21:11.
Utimizo: Kwa sababu watu wengi zaidi wanaishi katika maeneo ambayo hupatwa na matetemeko ya nchi mara nyingi, idadi ya watu wanaokufa au wanaolazimika kuhama kwa sababu ya tetemeko la nchi imeongezeka haraka.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
Ripoti inayoitwa World Disasters Report 2010 inasema hivi: “Kati ya misiba yote mikubwa, matetemeko ndiyo yamesababisha vifo vya watu wengi zaidi katika miaka ya karibuni.”
Kila mwaka, kuanzia 1970 hadi 2001, kulikuwa na wastani wa matetemeko ya nchi 19 yaliyosababisha misiba, * na wastani wa watu 19,547 walikufa kutokana nayo. Katika miaka kumi kabla ya 2012, wastani huo uliongezeka kufikia matetemeko ya nchi 28 kwa mwaka, kukiwa na wastani wa watu 67,954 waliokufa.
UNABII WA NNE:
“Mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni.”—Luka 21:11.
Utimizo: Licha ya kwamba kuna maendeleo ya kitiba na sayansi, bado mamilioni ya watu hufa kila mwaka kwa sababu ya magonjwa ya kuambukiza. Usafiri wa kimataifa na kuongezeka kwa idadi ya watu katika majiji kumeongeza uwezekano wa kutokea na kuenea upesi kwa magonjwa.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
Inakadiriwa kwamba ugonjwa wa ndui uliwaua watu milioni 300 hadi 500 hivi katika karne ya 20.
Taasisi ya Worldwatch inaripoti kwamba katika miaka 30 iliyopita, “zaidi ya magonjwa 30 ambayo hayakuwa yamejulikana hapo awali kama vile Ebola, virusi vya UKIMWI, virusi vya Hanta, na Mafua ya Ndege yametokeza hatari.”
Shirika la Afya Ulimwenguni limeonya kuhusu kuongezeka kwa virusi visivyoweza kutibiwa, likisema: “Tunaelekea wakati ambapo hatutatumia tena dawa za kuua viini, kwa kuwa maambukizo mengi ya kawaida hayataweza kutibiwa na yatawaua watu bila kuzuiwa.”
UNABII WA TANO:
Watu ‘watasalitiana na kuchukiana.
Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.’—Mathayo 24:10, 12.
Utimizo: Mauaji ya jamii nzimanzima yanayochochewa na chuki yamesababisha vifo vya mamilioni ya watu. Mizozo na uhalifu katika nchi nyingi imechangia sana kuongezeka kwa woga na jeuri.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
Serikali ya Nazi iliwaua Wayahudi milioni sita na mamilioni ya wengine. Mwandishi Zygmunt Bauman aliandika hivi akielezea jinsi raia walivyotenda: “Mauaji hayo ya halaiki hayakuwafanya watu wapandwe na ghadhabu, bali walinyamaza kimya kana kwamba hawakujali.”
Kulingana na Shirika la habari la BBC, inakadiriwa kwamba Watutsi na Wahutu ambao hawakuwa na msimamo mkali wapatao 800,000 waliuawa katika muda wa miezi michache. Mchunguzi mmoja anakadiria kwamba watu 200,000 hivi walihusika katika mauaji hayo ya halaiki.
Kila mwaka, zaidi ya watu 740,000 hufa kutokana na uhalifu na vita.
UNABII WA SITA:
“Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasio na upendo wa asili.”—2 Timotheo 3:2, 3.
Utimizo: Enzi yetu imejaa pupa na upotovu wa maadili. Mitazamo ya aina hiyo imetokeza matatizo mengi ya kijamii.
UTHIBITISHO UNAONYESHA NINI?
Ripoti moja ya UNICEF nchini Uingereza kuhusu hali njema ya watoto inasema kwamba wazazi na watoto nchini Uingereza “wanaonekana kuwa hawawezi kujizuia wasinunue vitu.” Watu katika familia hununua vitu vya kimwili ili “wajaribu kurekebisha mahusiano yao yaliyo na matatizo na pia ili wajihisi salama.”
Inakadiriwa kwamba watoto milioni 275 ulimwenguni pote hujionea jeuri inayotokea nyumbani.
“Nchini Marekani pekee, zaidi ya wazee 500,000 wanatendewa vibaya au kupuuzwa kila mwaka.”—Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa ya Kuambukiza.
UNABII WA SABA:
“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” —Mathayo 24:14.
Utimizo: Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi, inayotawala kutoka mbinguni na Yesu ndiye Mfalme. Ufalme huo wa kimbingu “utazivunja na kuzikomesha [serikali zote za wanadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.
USIKOSE SOMO LA PILI: Unabii Mbalimbali Wenye Kustaajabisha.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW