Saturday, May 27, 2017

NABII ISAYA NI NANI?

Image may contain: one or more people and text
NABII ISAYA WA KWENYE BIBLIA
Tuendelee kujifunza kuhusu Manabii wa kwenye Biblia. Kwenye hii Makala, tutajifunza kuhusu Nabii Isaya.
UTANGULIZI:
MAANA YA JINA ISAYA: “Wokovu wa Mungu”
FAMILIA YA ISAYA: Mtu aliyeoa, mwenye angalau wana wawili
MAKAO YA ISAYA: Yerusalemu
MIAKA YA UTUMISHI: Angalau miaka 46, kuanzia karibu mwaka wa 778 K.W.K. hadi wakati fulani baada ya mwaka wa 732 K.W.K.
WAFALME WA YUDA WALIOKUWAPO SIKU ZAKE: Uzia, Yothamu, Ahazi, Hezekia
MANABII WALIOKUWAPO SIKU ZAKE: Mika, Hosea, Odedi
Ni nini maana ya jina la Isaya?
Jina la Isaya lamaanisha “Wokovu wa Mungu,” na yaweza kusemwa kuwa hicho ndicho kichwa cha ujumbe wake. Ni kweli, baadhi ya unabii wa Isaya ni wa hukumu. Hata hivyo, kichwa cha wokovu chaonekana wazi. Mara kwa mara Isaya alisimulia namna Mungu, kwa wakati ufaao, angewafungulia Waisraeli kutoka utekwani huko Babiloni, akiwaruhusu mabaki warudi Sayuni na kuirejesha nchi kwa utukufu wake wa hapo awali. Hapana shaka kuwa pendeleo la kunena na kuandika unabii mbalimbali uhusuo kujengwa tena kwa jiji la Yerusalemu alilolipenda kulimpa Isaya shangwe kuu!
Katika mstari wa kwanza wa kitabu chake, Isaya ajitambulisha kuwa “mwana wa Amozi,”* naye atuambia kuwa alitumikia akiwa nabii wa Mungu katika “siku za Uzia na Yothamu na Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda.” (Isaya 1:1) Hii ingemaanisha kwamba Isaya aliendelea kutumikia akiwa nabii wa Mungu kwa taifa la Yuda kwa angalau miaka 46, labda kuanzia mwishoni mwa utawala wa Uzia—wapata mwaka wa 778 K.W.K.
(a) Sababu gani twapendezwa na kitabu cha Isaya leo?
(b) Kitabu cha Isaya huelekezaje uangalifu kwa Mesiya?
Lakini, ujumbe huu mbalimbali wa hukumu na wokovu unatuhusuje?
Kwa kupendeza, Isaya hatoi unabii kwa faida ya ufalme wa Yuda pekee wa makabila mawili. Kinyume cha hilo, ujumbe wake mbalimbali una maana ya pekee kwa siku yetu. Isaya atoa ufafanuzi mtukufu wa jinsi Ufalme wa Mungu utakavyoleta baraka kuu kwa dunia yetu. Kwa hiyo, sehemu kubwa ya maandishi ya Isaya yakazia Mesiya aliyeahidiwa, ambaye angetawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Danieli 9:25; Yohana 12:41) Basi si ajabu kwamba majina Yesu na Isaya yanadokeza jambo lilelile, jina Yesu likimaanisha “Yehova Ni Wokovu.”
Ni wazi kuwa Yesu alizaliwa karne saba hivi baada ya siku ya Isaya. Hata hivyo, unabii mbalimbali unaohusu Mesiya ulio katika kitabu cha Isaya ni wa kinaganaga sana na sahihi kwelikweli hivi kwamba yaonekana kana kwamba ni masimulizi ya mtu aliyejionea kwa macho maisha ya Yesu duniani. Chanzo kimoja kilisema kwamba kwa kuzingatia hilo, mara nyingine kitabu cha Isaya huitwa “Injili ya Tano.” Basi, haishangazi kwamba Yesu na mitume wake walikinukuu mara nyingi zaidi kitabu cha Biblia cha Isaya ili kutambulisha waziwazi Mesiya alikuwa nani.
Isaya atoa ufafanuzi mtukufu juu ya “mbingu mpya na nchi mpya” ambamo “mfalme atamiliki kwa haki [“uadilifu,” NW]” na wakuu watatawala kwa haki. (Isaya 32:1, 2; 65:17, 18; 2 Petro 3:13) Kwa hiyo kitabu cha Isaya huelekeza kwenye tumaini linalosisimua la Ufalme wa Mungu, chini ya Mesiya Yesu Kristo akiwa Mfalme aliyetawazwa. Ni kitia-moyo kilichoje kwetu kuishi kila siku tukitarajia kwa shangwe “wokovu [wa Yehova]”! (Isaya 25:9; 40:28-31) Basi, na tuchunguze kwa hamu ujumbe wenye thamani katika kitabu cha Isaya. Tufanyapo hivyo, tumaini letu katika ahadi za Mungu litaimarishwa sana. Pia tutasaidiwa kusitawisha usadikisho wetu kwamba Yehova kwa kweli ndiye Mungu wa wokovu wetu.
Ni jambo gani ambalo lazima lilikuwa kweli kuhusu maisha ya familia ya Isaya, na kwa nini?
Tukilinganisha yale tujuayo kuhusu manabii wengine, twajua machache juu ya maisha ya kibinafsi ya Isaya. Twajua kuwa alikuwa mwanamume aliyeoa na kwamba alimwita mkewe “nabii mke.” (Isaya 8:3) Kwa mujibu wa kichapo Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature cha McClintock na Strong, jina hilo huonyesha kuwa maisha ya ndoa ya Isaya “yalipatana na kazi yake, na kushikamana nayo vilevile.” Yawezekana kwamba mke wa Isaya, kama vile wanawake wengine wenye kumhofu Mungu katika Israeli ya kale, alikuwa na mgawo wake mwenyewe akiwa nabii mke.—Waamuzi 4:4; 2 Wafalme 22:14.
Isaya na mkewe walikuwa na angalau wana wawili, kila mmoja alipewa jina lenye maana ya unabii. Mzaliwa wa kwanza, Shear-yashubu, aliandamana na Isaya alipowasilisha ujumbe mbalimbali wa Mungu kwa Mfalme Ahazi mwovu. (Isaya 7:3) Ni wazi kwamba Isaya na mkewe waliifanya ibada ya Mungu kuwa jambo muhimu katika familia—kielelezo chema kwa wenzi wa ndoa leo!
Isaya na familia yake waliishi nyakati za ghasia katika historia ya Yuda. Msukosuko wa kisiasa ulikuwa umeenea, rushwa ilifisidi mahakama, na unafiki uliharibu mfumo wa kidini wa jamii. Vilele vya vilima vilijaa madhabahu za miungu isiyo ya kweli. Hata baadhi ya wafalme waliunga mkono ibada ya kipagani. Kwa mfano, Ahazi aliwaruhusu raia zake washiriki katika ibada ya sanamu na hata yeye mwenyewe aliabudu sanamu, “akampitisha mwanawe motoni” katika dhabihu ya tambiko kwa Moleki, mungu wa Wakanaani.* (2 Wafalme 16:3, 4; 2 Mambo ya Nyakati 28:3, 4) Hayo yote nayo yalitendeka miongoni mwa watu waliokuwa katika uhusiano wa agano na Mungu!—Kutoka 19:5-8.
(a) Wafalme Uzia na Yothamu waliweka kielelezo gani, na je, watu walifuata mwongozo wao?
(b) Isaya alionyeshaje ujasiri kati ya watu waasi?
Baadhi ya watu katika siku ya Isaya—pamoja na watawala wachache—walijaribu kuendeleza ibada ya kweli, nao wastahili pongezi. Mfalme Uzia, aliyefanya “yaliyo mema machoni pa BWANA,” alikuwa mmoja wao. Hata hivyo, alipokuwa akitawala, watu “wa[li]endelea kutoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu.” (2 Wafalme 15:3, 4) Mfalme Yothamu pia aliendelea kufanya “yaliyo ya adili machoni pa BWANA.” Lakini “watu waliendelea kufanya maovu.” (2 Mambo ya Nyakati 27:2, Biblia Habari Njema) Naam, kwa muda wote wa huduma ya unabii ya Isaya, hali ya kiroho na ya kiadili ya ufalme wa Yuda ilikuwa yenye kusikitisha. Kwa ujumla, watu walipuuza uvutano wowote mzuri kutoka kwa wafalme wao. Basi ni wazi kuwa haungekuwa mgawo rahisi kuwasilisha ujumbe wa Mungu kwa watu hao wakaidi. Hata hivyo, Mungu alipouliza, “Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu?” Isaya hakusita. Aliitikia kwa sauti: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isaya 6:8.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW