Saturday, May 13, 2017

NABII DEBORA SEHEMU YA KWANZA





JE, UNAMJUA NABII WA KIKE DEBORA WA KWENYE BIBLIA?
SEHEMU YA KWANZA
Biblia inapomtaja kwa mara ya kwanza Debora, inamrejelea kuwa “nabii wa kike.” Cheo hicho kinamfanya Debora awe wa pekee katika masimulizi ya Biblia ingawa haimaanishi kwamba ni yeye tu aliyekuwa na cheo kama hicho. * Debora alikuwa na daraka lingine pia. Inaonekana kwamba alitatua migogoro kwa kutoa majibu ya Mungu, matatizo yalipotokea.—Waamuzi 4:4, 5.
Debora aliishi katika eneo lenye milima la Efraimu, lililokuwa kati ya mji wa Betheli na Rama. Alikuwa na kawaida ya kukaa chini ya mtende na kutumikia watu kulingana na mwongozo wa Mungu. Ni wazi kwamba mgawo wake ulikuwa na changamoto, hata hivyo, Debora hakuruhusu hilo limvunje moyo. Kazi yake ilikuwa muhimu sana. Alishiriki kutunga wimbo ulioandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu ambao ulitia ndani maneno haya kuhusu watu wake waliokosa kuwa waaminifu: “Wakaanza kuchagua miungu mipya. Ndipo kukawa na vita malangoni.” (Waamuzi 5:8) Kwa kuwa Waisraeli walimwacha Mungu na kutumikia miungu mingine, Mungu aliacha washambuliwe na adui zao. Mfalme wa Kanaani, Yabini, aliwatawala kupitia Sisera, mkuu wa majeshi mwenye nguvu.
Sisera! Jina hilo lilipotajwa katika Israeli lilifanya watu waogope na kushtuka. Dini na utamaduni wa Wakanaani ulikuwa wenye ukatili, kwa kuwa walitoa watoto wao kuwa dhabihu na walifanya ukahaba hekaluni. Hali ilikuwaje mkuu huyo wa jeshi la Kanaani na jeshi lake walipotawala nchi hiyo? Wimbo wa Debora unaonyesha kwamba ilikuwa vigumu kusafiri nchini na maisha katika maeneo ya vijijini yalikuwa magumu, hivyo watu walihama. (Waamuzi 5:6, 7) Tunaweza kuwazia jinsi ambavyo watu walikuwa wakiogopa na kujificha katika mapori na vilima, wakiogopa kulima au kuishi katika vijiji ambavyo havikuwa na ukuta na wakiogopa sana kushambuliwa kwa sababu ya kusafiri barabarani, watoto wao kutekwa, na wanawake wao kubakwa. *
Hofu ilitawala nchini kwa miaka 20 mpaka Yehova alipoona wazi kwamba watu wake wakaidi walikuwa tayari kubadilika au, kama wimbo ulioandikwa na Debora na Baraka kwa mwongozo wa roho ya Mungu unavyosema, “Mpaka mimi, Debora, niliposimama, mpaka niliposimama kama mama katika Israeli.” Hatujui ikiwa Debora, mke wa Lapidothi, alikuwa na watoto, lakini usemi huo ulikuwa lugha ya mfano. Ni kana kwamba Yehova alimpa Debora mgawo wa kulinda taifa hilo kama vile mama angefanya kwa watoto wake. Alimwagiza amwambie Mwamuzi Baraka, mwanamume mwenye imani yenye nguvu, aende kupigana na Sisera.—Waamuzi 4:3, 6, 7; 5:7.
Mungu alitoa agizo hili kupitia Nabii Debora: “Nenda, usambae katika Mlima Tabori.” Baraka alipaswa kukusanya wanaume 10,000 kutoka makabila mawili ya Israeli. Debora alitaja ahadi ya Mungu kwamba wanaume hao wangemshinda Sisera mwenye nguvu na magari yake 900 ya vita! Bila shaka ahadi hiyo ilimfanya Baraka astaajabu. Waisraeli hawakuwa na jeshi wala silaha. Licha ya hali hiyo, Baraka alikubali kwenda vitani ikiwa tu Debora angeenda pamoja naye katika Mlima Tabori.—Waamuzi 4:6-8; 5:6-8.
Kwa sababu ya ombi hilo, watu fulani hudai kwamba Baraka hakuwa na imani, lakini jambo hilo si kweli. Baraka hakumwomba Mungu ampe silaha zaidi. Akiwa mwanamume mwenye imani, Baraka aliona umuhimu wa kuandamana na mwakilishi wa Mungu ili kumwimarisha na kuimarisha watu wake. (Waebrania 11:32, 33) Mungu alikubali ombi lake. Alimruhusu Debora kwenda na Baraka kama alivyoomba. Hata hivyo, Mungu alimwezesha Debora kutabiri kwamba ushindi wa pigano hilo usingetokana na mwanamume. (Waamuzi 4:9) Mungu aliamua kwamba mwanamke ndiye atakayemuua Sisera aliyekuwa mwovu!
Katika ulimwengu wa leo, wanawake wanakabili matendo mengi ya ukosefu wa haki, jeuri, na kutendewa vibaya. Ni mara chache sana wanatendewa kwa heshima kama Mungu anavyotaka watendewe. Hata hivyo, machoni pa Mungu, wanawake na wanaume wana haki sawa na wanaweza kupata kibali chake. (Waroma 2:11; Wagalatia 3:28) Mfano wa Debora unatukumbusha kwamba Mungu huwabariki wanawake kwa kuwapa mapendeleo na hilo linaonyesha kwamba anawatumaini na kuwapa kibali chake. Ni muhimu kwamba tuepuke kuwa na maoni yasiyofaa kuelekea wanawake yaliyoenea ulimwenguni leo.
USIKOSE SEHEMU YA PILI YA NABII DEBORA: DUNIA ILITIKISIKA, MBINGU PIA ZIKATIRIRIKA MAJI...
Baraka alikusanya jeshi lake. Alikusanya wanaume 10,000 jasiri ili kupambana na jeshi la Sisera lenye kutisha...........
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW