Friday, June 2, 2017

KISA CHA RUTHU NA NAOMI (SEHEMU YA KWANZA)

Image may contain: 1 person, text
UTANGULIZI:
Kitabu cha Ruthu kimefafanuliwa kuwa jiwe dogo lenye thamani, yaani, kazi ndogo ya usanii. Kwa kweli, kitabu hicho hakina habari nyingi kama kitabu kinachokitangulia cha Waamuzi, ambacho kinatusaidia kutambua wakati wa matukio ya kitabu cha Ruthu. (Ruthu 1:1) Inaelekea vitabu hivyo viwili viliandikwa na nabii Samweli. Hata hivyo, unaposoma Biblia, huenda utakubali kwamba kitabu cha Ruthu kiko mahali panapofaa katika orodha ya vitabu vya Biblia. Baada ya kusoma kuhusu vita, uvamizi, na mashambulizi ya kulipiza kisasi yaliyorekodiwa katika kitabu cha Waamuzi, unapata kitabu kidogo ambacho kinatukumbusha kwamba Mungu hawasahau kamwe watu wanaopenda amani ambao wanapambana na matatizo ya kila siku. Tukio hili la kifamilia linatufunza mambo mengi yanayoweza kutunufaisha sote kuhusu upendo, kufiwa, imani, na ushikamanifu.
SEHEMU YA KWANZA:
Ruthu alitembea pamoja na Naomi kwenye barabara iliyopita katika nyanda ndefu za Moabu. Walikuwa peke yao, watu wawili wadogo katika eneo kubwa lisilo na watu. Wazia Ruthu akitambua kwamba ni jioni, kisha anamtazama mama mkwe wake na kuwaza kama ni wakati wa kutafuta mahali pa kupumzika usiku. Alimpenda sana Naomi na alikuwa tayari kufanya lolote ili kumtunza.
Wote wawili walikuwa na huzuni nyingi sana. Tayari Naomi alikuwa mjane kwa miaka kadhaa, lakini sasa alikuwa akiomboleza misiba mingine, vifo vya wanawe wawili Kilioni na Maloni. Ruthu pia alikuwa akiomboleza. Maloni alikuwa mume wake. Ruthu na Naomi walikuwa wakielekea Bethlehemu, mji uliokuwa huko Israeli. Hata hivyo, safari zao zilitofautiana kwa njia fulani. Naomi alikuwa akirudi nyumbani. Naye Ruthu alikuwa akienda mahali asipopajua, huku akiacha watu wake wa ukoo, nchi yake, na tamaduni zake zote, kutia ndani miungu ya nchi hiyo.—Soma Ruthu 1:3-6.
Ni majibu ya maswali gani ambayo yatatusaidia kuiga imani ya Ruthu?
Ni nini kingemchochea mwanamke kijana afanye mabadiliko makubwa hivyo?
Ruthu angeanzaje upya maisha na angewezaje kumtunza Naomi?
Tunapochunguza majibu ya maswali hayo, tutapata mambo mengi tunayoweza kuiga kuhusu imani ya Ruthu Mmoabu. Kwanza, acheni tuone jinsi wanawake hao wawili walivyojipata kwenye barabara hiyo ndefu ya kwenda Bethlehemu.
Familia Iliyovunjwa na Misiba
(a) Kwa nini familia ya Naomi ilihamia Moabu?
(b) Naomi alikabiliana na matatizo gani huko Moabu?
Ruthu alilelewa huko Moabu, nchi ndogo iliyokuwa upande wa mashariki wa Bahari ya Chumvi. Nchi hiyo ilikuwa na maeneo yaliyoinuka yenye miti michache na mabonde yenye kina kirefu. Mara nyingi, “nchi ya Moabu” ilikuwa na mazao mengi, hata nchi ya Israeli ilipokumbwa na janga la njaa. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Ruthu akutane na Maloni na familia yao.—Ruthu 1:1.
Janga la njaa katika nchi ya Israeli lilikuwa limefanya mume wa Naomi, Elimeleki, amchukue mkewe na wanawe wawili kutoka nchi yao na kwenda kuishi Moabu wakiwa wakaaji wageni. Ni lazima hatua hiyo ilijaribu imani ya kila mshiriki wa familia, kwa kuwa Waisraeli walihitaji kwenda kwa ukawaida mahali patakatifu ambapo Yehova alikuwa amechagua ili kuabudu. (Kumbukumbu ya Torati 16:16, 17) Naomi alifaulu kushikilia imani yake. Hata hivyo, bado aliomboleza baada ya mumewe kufa.—Ruthu 1:2, 3.
(a) Kwa nini huenda Naomi alihangaika wanawe walipooa wanawake Wamoabu?
(b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Naomi aliwatendea wake za wanawe kwa njia nzuri?
Huenda Naomi alihuzunika tena wanawe walipooa wanawake Wamoabu. (Ruthu 1:4) Alijua kwamba babu yao, Abrahamu, alijitahidi sana ili kumtafutia mwanawe Isaka mke kutoka kwa watu wake, ambao walikuwa waabudu wa Yehova. (Mwanzo 24:3, 4) Baadaye, Sheria ya Musa iliwaonya Waisraeli wasiwaruhusu wana na binti zao kufunga ndoa na watu wa mataifa ya kigeni, ili watu wa Mungu wasianze kuabudu sanamu.—Kumbu kumbu La Torati 7:3, 4.
Licha ya hayo, Maloni na Kilioni walioa wanawake Wamoabu. Iwe jambo hilo lilimhangaisha Naomi au kumvunja moyo, bado alijitahidi kuwatendea wake za wanawe, Ruthu na Orpa, kwa fadhili ya kweli na upendo. Labda alitazamia kwamba kama yeye, siku moja wangekuwa waabudu wa Yehova. Vyovyote vile, Ruthu na Orpa walimpenda sana Naomi. Uhusiano wao mzuri uliwasaidia walipopatwa na msiba. Hata kabla ya kuzaa watoto, wanawake hao vijana walifiwa na waume zao.—Ruthu 1:5.
Huenda ni nini kilichomfanya Ruthu avutiwe na Yehova?
Je, imani ya kidini ya Ruthu ilimsaidia kukabiliana na msiba?
Huenda haikumsaidia. Wamoabu waliabudu miungu mingi, na Kemoshi ndiye aliyekuwa mungu wao mkuu. (Hesabu 21:29) Inaonekana dini ya Wamoabu ilikuwa pia na ukatili na mambo yenye kutisha yaliyokuwa ya kawaida siku hizo, kutia ndani kutoa watoto kama dhabihu. Kwa kweli, jambo lolote ambalo Ruthu alijifunza kutoka kwa Maloni au Naomi kumhusu Mungu, Mungu wa Israeli mwenye upendo na rehema, lilimfanya aone tofauti kubwa. Mungu alitawala kwa upendo, bali si kwa vitisho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:5.) Baada ya kukabili msiba mkubwa, huenda Ruthu alisitawisha uhusiano wa karibu zaidi na Naomi huku akimsikiliza mwanamke huyo mzee alipozungumza kumhusu Mungu mweza-yote, Mungu, kazi zake za ajabu, na jinsi alivyoshughulika na watu wake kwa upendo na rehema.
(a) Naomi, Ruthu, na Orpa walifanya uamuzi gani?
(b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na misiba iliyowapata Naomi, Ruthu, na Orpa?
Kwa upande mwingine, Naomi alitamani sana kupata habari kutoka nyumbani kwao. Siku moja alisikia, labda kupitia mfanyabiashara anayesafiri, kwamba janga la njaa lilikuwa limekwisha huko Israeli. Mungu alikuwa amewakumbuka watu wake. Sasa mji wa Bethlehemu ulikuwa tena na maana yake kamili, yaani, “Nyumba ya Mkate.” Naomi akaamua kurudi nyumbani.—Ruthu 1:6.
Sasa Ruthu na Orpa wangefanyaje?
(Ruthu 1:7) Walikuwa wamesitawisha uhusiano wa karibu na Naomi kwa sababu ya mambo yaliyowapata. Inaonekana Ruthu alivutiwa na fadhili za Naomi na imani yake thabiti kwa Mungu. Wajane hao watatu waliondoka kuelekea Yuda pamoja.
Simulizi la Ruthu linatukumbusha kwamba misiba huwapata watu wote, wazuri na wabaya. (Mhubiri 9:2, 11) Pia, linatukumbusha kwamba tunapokabiliana na misiba mikubwa, ni jambo la hekima kutafuta faraja na kitulizo kutoka kwa watu wengine, hasa wale ambao wanatafuta kimbilio katika Mungu Mungu ambaye Naomi alimwabudu.—Methali 17:17.
USIKOSE SEHEMU YA PILI - "Upendo Mshikamanifu wa Ruthu"
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW