Saturday, June 3, 2017

SAFARI YA KUSISIMUA YA HANA MAMA YAKE NABII SAMWELI -SEHEMU YA KWANZA-

Image may contain: one or more people, people sitting and text
Je, ni sababu gani Hana ni mwenye huzuni anapotayarisha safari yake?
Je, habari ya Hana inaweza kutufundisha nini?
Hana ana mambo mengi ya kufanya katika kutayarisha safari, anajaribu kufanya hivyo ili asahau matatizo yake. Huo ni wakati ambao kila mutu anapaswa kuwa na furaha; kila mwaka, Elkana, bwana yake, anaipeleka familia yake yote kwenye hema, huko Shilo, ili kuabudu. Yehova alisema kama pindi hizo zinapaswa kuwa pindi zenye kufurahisha. (Soma Kumbukumbu la Torati 16:15.) Na bila shaka, Hana alifurahia sikukuu hizo tangu utoto wake. Lakini, miaka hii ya karibuni, mambo yamemubadilikia sana.
Hana amebarikiwa kuwa na bwana anayemupenda. Lakini, bwana yake Elkana ana bibi wa pili, anayeitwa Penina. Na inaonekana kama Penina anakusudia kabisa kumukosesha Hana amani. Anafanya yake yote ili wakati wa sikukuu hizo, Hana asiwe na furaha hata kidogo. Namna gani? Na jambo la maana zaidi, namna gani imani ya Hana katika Mungu itamusaidia kushinda hali hiyo ambayo kwa kawaida ni nguvu sana kuvumilia? Kama una magumu yanayokukosesha furaha katika maisha, habari hii ya Hana itakutia moyo.
‘Kwa Nini Moyo Wako Una Huzuni?’
Je, Hana anapambana na matatizo makubwa gani mawili, na sababu gani kila tatizo si jepesi?
Biblia inaeleza matatizo mawili makubwa ambayo Hana anapambana nayo. Yeye mwenyewe anaweza kumaliza tatizo la kwanza, lakini kuhusu lile la pili, hana uwezo hata kidogo. Tatizo la kwanza: Bwana ya Hana ana mwanamuke mwengine, na huyo mbandala yake anamuchukia sana. Tatizo la pili: Yeye ni tasa, ni kusema, hawezi kuzaa. Hali hiyo ni tatizo kabisa kwa mwanamuke yeyote anayetaka kuwa na watoto; na katika siku za Hana, katika maisha ya watu, hali hiyo ilihuzunisha sana. Sababu gani? Kwa sababu, kila familia ilitegemea watoto ili kuendelesha jina la familia. Kwa hiyo, mwanamuke kuwa tasa ilionekana ni mukoshi na jambo la haya sana.
Penina hangemusumbua Hana, labda angeweza kuvumilia tatizo hilo. Ndoa ya kuwa na mbanda si rahisi: kwa kawaida utakuta tu mambo ya kushindana, kugombana, na yenye kuhuzunisha moyo. Ni hivyo, kwa sababu ndoa hizo hazipatane na kanuni ambayo Mungu aliweka katika bustani ya Edeni kuhusu ndoa, ni kusema, bwana kuwa na bibi mumoja. (Mwanzo 2:24) Hakuna andiko katika Biblia linaloonyesha kama kuoa wanawake zaidi ya mumoja ni jambo nzuri, na kwa hiyo, hali yenye kuhuzunisha inayopita katika familia ya Elkana inaonyesha wazi kwamba kuoa wanawake wengi si vizuri.
Sababu gani Penina anapenda kumutesa Hana, na anafanya nini ili moyo wa Hana uumie?
Elkana anamupenda Hana sana. Hadisi ya Wayahudi inaonyesha kwamba Hana ndiye bibi yake wa kwanza, na kisha miaka mingi baadaye ndipo anamuoa Penina. Iwe ilikuwa hivyo ao hapana, jambo la hakika ni kwamba, Penina anamusikilia Hana wivu sana, na kwa hiyo, anafanya yake yote ili kumutesa. Penina anajivuna kwa sababu yeye amezaa watoto. Kila mara anapozaa mutoto, kiburi chake kinapanda. Kuliko kumusikilia Hana huruma na kumufariji, yeye anaendelea kuingiza tena kisu katika kidonda cha Hana. Biblia inasema kwamba Penina alimusumbua Hana sana ili ‘kumufanya akasirike.’ (1 Samueli 1:6) Inaonekana kama Penina anafanya hivyo kimakusudi. Anapenda tu kumuumiza mwenzake moyoni, na anamuumiza kabisa.
Hana alihuzunika sana kwa sababu alikuwa tasa, na Penina alifanya yake yote ili kumukosesha amani
(a) Ijapokuwa Elkana anajaribu kumufariji Hana, sababu gani Hana hapendi kumuelezea namna anavyotendewa?
(b) Kwa sababu Hana alikuwa tasa, hilo linamaanisha kwamba Mungu hakuwa anapendezwa naye?
Penina anaona kwamba wakati mzuri kabisa wa kumukosesha Hana amani, ni wakati wanapatikana huko Shilo, kwenye sikukuu za kila mwaka. Penina ana watoto wengi. Elkana anapatia ‘wana na binti’ za Penina, sehemu ya zabihu ili kumutolea Mungu. Lakini, Hana hakuwa na watoto, kwa hiyo anapewa sehemu moja tu, kwa ajili yake mwenyewe. Penina anapandisha kabisa mabega na anamukumbusha Hana kwamba yeye ni tasa; basi, Hana anaanza kulia na anakosa hata hamu ya kula chakula. Elkana anaona kwamba Hana ana huzuni sana na anashindwa kula, kwa hiyo anajaribu kumfariji. Anamuuliza hivi: ‘Hana, kwa nini unalia, na kwa nini haukule chakula, na kwa nini moyo wako unahisi vibaya [ao una huzuni]? Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?’—1 Sam. 1:4-8.
Elkana anatambua kwamba Hana anahuzunika kwa sababu yeye ni tasa. Na bila shaka, Hana anafurahi kusikia maneno hayo yenye fazili ya Elkana, yanayomhakikishia kwamba anampenda. * Lakini, Elkana haseme lolote juu ya ubaya wa Penina, na Biblia haiseme kama Hana alimuelezea bwana yake namna anavyotendewa. Labda anaona kwamba kumuelezea Elkana mambo ya Penina, hilo linaweza tu kufanya mambo yachache zaidi. Je, Elkana atabadilisha kabisa jambo lolote? Je, hilo halitamchochea Penina atende vibaya hata zaidi, na je, hilo halitafanya watoto na watumishi wa Penina wamusaidie katika kumshambulia Hana? Mambo yakiwa hivyo, basi, Hana ataendelea kujisikia kama mutu anayetupiliwa kabisa na watu wa nyumba yake.
Alipotendewa vibaya nyumbani, Hana alimwendea Mungu ili kupata faraja
Iwe Elkana alijua ao hakujua mambo yote ambayo Penina alikuwa anamtendea Hana, Mungu alikuwa anaona yote. Neno lake linasema hivyo, na yale linasema ni onyo kwa wote walio na tabia ya kuwasikilia wengine wivu na kuwachukia, iwe ni wivu kidogo ao chuki kidogo. Kwa upande mwengine, watu wasio na kosa na wenye kufanya amani kama Hana, wanaweza kufarijika kujua kwamba Mungu wa haki atatengeneza hali yao kwa namna yake na kwa wakati wake. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4.) Bila shaka, Hana anajua jambo hilo pia, kwa sababu anamuendea Mungu ili kupata msaada.
‘Uso Wake Hauna Tena Huzuni’
Hana alikuwa tayari kufanya safari ya Shilo ijapokuwa alijua namna mbanda yake atamutendea, mufano wake unaweza kutufundisha nini?
Asubuhi mapema kila mtu anajitayarisha kwa ajili ya safari, hata watoto pia. Familia itafanya safari hiyo ya kilometa 30 ili kufika Shilo, kupitia inchi ya Efraimu yenye milima-milima. * Safari hiyo ni ya mwendo wa siku moja ao siku mbili. Hana anajua namna mbanda yake atamtendea. Hata hivyo, habaki nyumbani. Hana anaachia waabudu wote wa Mungu leo mufano muzuri sana. Si jambo la hekima kuacha kumuabudu Mungu kwa sababu ya mwenendo usiofaa wa wengine. Tukifanya hivyo, tutapoteza baraka ambazo zingetusaidia kuvumilia.
(a) Sababu gani Hana anapopata nafasi mara moja anaenda kwenye hema la ibada?
(b) Namna gani anamufungulia Baba yake wa mbinguni mahangaiko ya moyo wake katika sala?
Kisha kufanya safari ndefu kupitia milima iliyo na njia za lukumba-lukumba, familia hiyo kubwa inakaribia Shilo. Mji huo uko juu ya mlima ambao unazungukwa na milima mingi mirefu. Wanapoendelea kukaribia Shilo, Hana anafikiri sana yale atakayomuelezea Mungu katika sala. Wanapofika tu, familia inakaa pamoja ili kula chakula. Wakati fulani, Hana anawaacha na anajielekeza kwenye hema ya ibada ya Yehova. Kuhani Mukubwa Eli yuko hapo, anakaa pembeni ya nguzo ya mulango wa hema. Lakini Hana hamuone kwa sababu anakazia tu Mungu wake mafikiri. Hapa kwenye hema ya ibada, iko hakika kwamba atasikiwa. Hata kama hakuna mutu anayeweza kuelewa taabu yake, Baba yake wa mbinguni anaweza kufanya hivyo. Anasikia uchungu sana moyoni na anaanza kulia.
Mwili wa Hana unatetemeka kwa sababu ya kulia, anazungumuza na Mungu kimoyo-moyo. Midomo yake inatetemeka, anatafuta maneno ya kumuelezea Mungu ili kumuonyesha uchungu wake. Anasali kwa muda mrefu, anamfungulia Baba yake mahangaiko ya moyo wake. Hana hamuombe tu Mungu amsaidie kuzaa, lakini zaidi ya baraka za Mungu anatamani pia kumtolea Mungu chochote ambacho angeweza. Kwa hiyo, anafanya naziri, anamuambia Mungu kwamba ikiwa anazaa mtoto mwanaume atamtolea Mungu mutoto huyo ili amutumikie.—1 Samueli 1:9-11.
USIKOSE SEHEMU YA PILI.... Kwanini Eli aliwaza kuwa HANA AMELEWA....
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW