Friday, June 2, 2017

KISA CHA RUTHU NA NAOMI (SEHEMU YA PILI)

Image may contain: 2 people, people sitting and text
Upendo Mshikamanifu wa Ruthu
Kwa nini Naomi alitaka Ruthu na Orpa warudi nyumbani kwao badala ya kuandamana naye, na mwanzoni wanawake hao wawili walitendaje?
Wajane hao watatu walipokuwa wakiendelea na safari yao, Naomi alianza kuhangaishwa na jambo lingine. Aliwafikiria wanawake hao wawili waliokuwa wakiandamana naye na upendo waliokuwa wamemwonyesha yeye na wanawe. Hakutaka kuwaongezea mizigo mingine. Ikiwa wangeacha nchi yao na kumfuata, angewasaidiaje huko Bethlehemu?
Mwishowe, Naomi akawaambia hivi: “Nendeni, rudini, kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Mungu na awaonyeshe fadhili zenye upendo, kama vile tu mlivyowaonyesha wanaume hawa ambao sasa wamekufa na mimi pia.” Alionyesha pia kwamba alitumaini Mungu angewabariki kwa kuwapa waume wengine na waanze maisha mapya. “Kisha akawabusu,” simulizi hilo linasema, “nao wakaanza kupaaza sauti zao na kulia.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Ruthu na Orpa walikuwa na uhusiano wa karibu na mwanamke huyo mwenye fadhili na asiye na ubinafsi. Wote wawili waliendelea kusisitiza hivi: “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.”—Ruthu 1:8-10.
(a) Ni sababu gani iliyomfanya Orpa arudi?
(b) Naomi alijaribuje kumshawishi Ruthu arudi pia?
Hata hivyo, Naomi hakushawishiwa kwa urahisi. Aliwasadikisha kwamba hangeweza kuwasaidia huko Israeli, kwa sababu hakuwa na mume wa kumwandalia, wala wana ambao wangewaoa, wala tumaini lolote. Aliwaambia kwamba alikuwa na uchungu mwingi kwa sababu hakuwa na uwezo wa kuwaandalia. Orpa alikubaliana na Naomi. Huko Moabu alikuwa na mama, watu wa familia, na makao. Lilikuwa jambo linalopatana na akili kwake kubaki Moabu. Hivyo, kwa shingo upande alimbusu Naomi, akamwambia kwaheri na kuondoka.—Ruthu 1:11-14.
Namna gani Ruthu? Maneno ya Naomi yalimhusu pia. Hata hivyo, tunasoma hivi: “Bali Ruthu akashikamana naye.” Labda Naomi alikuwa ameanza kutembea tena barabarani alipotambua kwamba Ruthu alikuwa akimfuata. Akamwambia hivi: “Tazama! Shemeji yako amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja naye.” (Ruthu 1:15) Maneno ya Naomi yanatufunulia jambo fulani muhimu. Orpa hakuwa tu amerudi kwa watu wake, bali pia kwa “miungu yake.” Alikuwa tayari kuendelea kumwabudu Kemoshi na miungu mingine ya uwongo. Je, Ruthu alihisi hivyo pia?
(a) Ruthu alionyeshaje upendo mshikamanifu?
(b) Tunajifunza nini kutoka kwa Ruthu kuhusu upendo mshikamanifu?
(Ona pia picha za wanawake hao wawili.)
Huku akimtazama Naomi wakiwa kwenye barabara hiyo isiyo na watu, Ruthu alikuwa na uhakika na utulivu moyoni. Alimpenda sana Naomi, na Mungu ambaye Naomi aliabudu. Hivyo Ruthu akasema: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. Pale utakapokufa nitakufa nami, na hapo ndipo nitakapozikwa. Mungu na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.”—Rut. 1:16, 17.
Ruthu akimwambia Naomi, “Uendako Nitaenda”
“Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu”
Maneno ya Ruthu yalikuwa ya pekee sana, hivi kwamba bado yanakumbukwa hata baada ya miaka elfu tatu kupita. Maneno yake yanafunua vizuri sifa yenye thamani, yaani, upendo mshikamanifu. Ruthu alikuwa na upendo wenye nguvu na wenye ushikamanifu sana hivi kwamba alikuwa tayari kushikamana na Naomi na kwenda naye popote pale. Wangetenganishwa tu na kifo. Watu wa Naomi wangekuwa watu wake, kwa kuwa Ruthu alikuwa tayari kuacha kila kitu alichokijua huko Moabu, hata miungu ya Wamoabu. Tofauti na Orpa, Ruthu alisema kwa moyo wote kwamba alitaka Mungu, Mungu wa Naomi, awe Mungu wake pia. *
Basi, wakaendelea na safari wakiwa wawili tu, kwenye barabara ndefu ya kwenda Bethlehemu. Inakadiriwa kwamba huenda safari hiyo ilichukua juma moja. Bila shaka, ingawa walikuwa na majonzi walifarijiana kwa kiasi fulani.
Unafikiri tunawezaje kuiga upendo mshikamanifu wa Ruthu katika mahusiano ya kifamilia, kirafiki, na kutanikoni?
Hata leo, watu wengi ulimwenguni wana majonzi. Katika Biblia, siku zetu zinaitwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na hivyo tunakabili misiba na majonzi ya aina mbalimbali. (2 Timothy 3:1) Kwa hiyo, sifa aliyoonyesha Ruthu ni muhimu hata zaidi leo. Upendo mshikamanifu, yaani, upendo ambao hushikamana na mtu au kitu bila kuacha, ni sifa muhimu katika ulimwengu huu wenye misukosuko. Tunahitaji sifa hiyo katika ndoa, uhusiano wa familia, urafiki, na pia katika kutaniko la Kikristo. (Soma 1 Yohana 4:7, 8, 20.) Tunapoendelea kusitawisha upendo kama huo, tunaiga mfano bora wa Ruthu.
Ruthu na Naomi Huko Bethlehemu
(a) Naomi alipatwa na hali gani huko Moabu?
(b) Naomi alikuwa na maoni gani yasiyofaa kuhusu matatizo yake? (Ona pia Yakobo 1:13.)
Bila shaka, ni rahisi kuzungumza kuhusu upendo mshikamanifu, lakini ni vigumu kuonyesha sifa hiyo kwa vitendo. Ruthu hakuwa tu na nafasi ya kumwonyesha Naomi upendo mshikamanifu bali pia Mungu aliyechagua kumwabudu, Mungu.
Hatimaye, wanawake hao wawili waliwasili Bethlehemu, kijiji kilichokuwa karibu kilomita 10 upande wa kusini wa Yerusalemu. Inaonekana Naomi na familia yake walijulikana sana katika mji huo mdogo, kwa kuwa habari za kurudi kwake zilisambaa kila mahali. Wanawake katika eneo hilo walimtazama na kuulizana, “Je, huyu ni Naomi?” Bila shaka, alikuwa amebadilika baada ya kuishi Moabu; kwa kumtazama, watu waliona kwamba alikuwa amekabiliana na matatizo na majonzi kwa miaka mingi.—Ruthu 1:19.
Naomi aliwafunulia wanawake hao wa ukoo na majirani wa zamani jinsi maisha yalivyokuwa machungu kwake. Hata alihisi kwamba jina lake lilipaswa kubadilishwa kutoka Naomi, linalomaanisha “Uzuri Wangu,” na kuwa Mara, linalomaanisha “Uchungu.” Maskini Naomi! Kama Ayubu aliyeishi kabla yake, alifikiri kwamba Mungu Mungu alikuwa amemletea matatizo.—Ruthu 1:20, 21; Ayubu 2:10; 13:24-26.
Ruthu alianza kufikiria nini, na Sheria ya Musa ilitoa maandalizi gani kwa ajili ya maskini? (Ona pia maelezo ya chini.)
Wanawake hao walipoanza maisha mapya huko Bethlehemu, Ruthu alianza kufikiria jinsi ambavyo angetimiza mahitaji yake na pia ya Naomi. Alijifunza kwamba Sheria ambayo Mungu alikuwa amewapa watu wake huko Israeli ilitia ndani mpango wenye upendo kwa ajili ya maskini. Waliruhusiwa kwenda mashambani wakati wa mavuno na kuwafuata wavunaji, huku wakikusanya masalio na vilevile kuvuna nafaka kwenye kingo za mashamba. *—Lawi 19:9, 10; Kumbukumbu 24:19-21.
Ruthu alifanya nini alipoingia katika mashamba ya Boazi, na kazi ya kukusanya masalio ilikuwaje?
Ulikuwa wakati wa kuvuna shayiri, inaelekea mwezi wa Aprili kulingana na kalenda ya kisasa, na Ruthu alienda mashambani ili kuona kama kuna mtu ambaye angemruhusu akusanye masalio. Aliingia katika shamba la mwanamume aliyeitwa Boazi, tajiri mwenye mashamba ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wa Naomi aliyekuwa amekufa. Ingawa Sheria ilimruhusu kukusanya masalio, hakutumia maandalizi hayo vibaya, alimwomba ruhusa mwanamume aliyewasimamia wavunaji ili aanze kukusanya. Alimruhusu, na Ruthu akaanza kazi.—Ruthu 1:22–2:3, 7.
Wazia Ruthu akiwafuata wavunaji. Walipokuwa wakikata shayiri kwa miundu yao, aliinama ili aokote masuke waliyoangusha au kubakisha, akayakusanya katika miganda, na kuibeba mpaka mahali ambapo angeipiga-piga na kupata nafaka baadaye. Ilikuwa kazi ya polepole, yenye kuchosha, na ilizidi kuwa ngumu kadiri jua lilivyoendelea kuwa kali. Hata hivyo, Ruthu aliendelea kukusanya, akisimama kidogo tu ili kupangusa jasho usoni na kula chakula chepesi cha mchana katika “nyumba”—inaelekea ni kibanda kilichotengenezwa ili kuwapa wafanyakazi kivuli.
Ruthu akikusanya shayiri kwa unyenyekevu nyuma ya wavunaji shambani:
Ruthu alikuwa tayari kufanya kazi ngumu na ya hali ya chini ili atimize mahitaji yake na pia ya Naomi:
Boazi alikuwa mtu wa aina gani, na alimtendeaje Ruthu?
Inaelekea Ruthu hakutazamia mtu yeyote amtambue, lakini kuna mtu aliyemtambua. Boazi alimwona na kumwuliza msimamizi fulani kijana kuhusu mwanamke huyo. Boazi, mwanamume mwenye imani thabiti, aliwasalimu wafanyakazi wake—huenda wengine walikuwa vibarua wa siku moja au hata watu wa mataifa ya kigeni—akiwaambia: “Mungu na awe pamoja nanyi.” Nao wakamjibu kwa maneno kama hayo. Mwanamume huyo mwenye umri mkubwa aliyempenda Mungu alimtendea Ruthu kama bintiye.—Ruthu 2:4-7.

Huku akimwita “binti yangu,” Boazi alimshauri Ruthu aendelee kukusanya masalio kwenye mashamba yake na afanye kazi karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili asisumbuliwe na wafanyakazi wa kiume. Alihakikisha kwamba alipata chakula cha mchana. (Soma Ruthu 2:8, 9, 14.) Zaidi ya hayo, alitafuta nafasi ya kumpongeza na kumtia moyo. Jinsi gani?
(a) Ruthu alijulikana kuwa mtu wa aina gani?
(b) Kama Ruthu, unawezaje kupata kimbilio katika Mungu?
Ruthu alipomwuliza Boazi kwa nini alimtendea kwa fadhili hivyo ingawa hakuwa Mwisraeli, Boazi alimwambia alikuwa amesikia yote aliyokuwa amemfanyia Naomi, mama-mkwe wake. Inaelekea Naomi alikuwa amemsifu Ruthu aliyempenda mbele ya wanawake wa Bethlehemu, na habari hizo zilikuwa zimemfikia Boazi. Pia, alijua kwamba Ruthu alikuwa ameanza kumwabudu Mungu, kwa kuwa alisema: “Mungu na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”—Ruthu 2:12.
Kwa kweli, maneno hayo yalimtia moyo sana Ruthu! Alikuwa ameamua kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Mungu, kama ndege mdogo anavyojificha kando ya mama yake. Alimshukuru Boazi kwa kumtia moyo. Naye akaendelea kufanya kazi mpaka jioni.—Ruthu 2:13, 17.
Tunajifunza nini kutokana na Ruthu kuhusu mazoea mazuri ya kazi, uthamini, na upendo mshikamanifu?
Leo, sote tunaopambana na hali ngumu za kiuchumi tunaweza kuiga imani ya Ruthu. Hakutazamia kwamba watu wengine walipaswa kumtunza, hivyo alithamini kila jambo alilofanyiwa. Hakuaibika kufanya kazi ngumu kwa saa nyingi ili kumtunza mtu aliyempenda, ingawa ilikuwa kazi ya hali ya chini. Alifanya kazi hiyo na akafuata mashauri yenye hekima ya kufanya kazi akiwa salama na kushirikiana na watu wazuri. Jambo la maana zaidi ni kwamba hakusahau kamwe kimbilio lake la kweli, yaani, Baba yake aliyemlinda, Mungu.
Tukionyesha upendo mshikamanifu kama wa Ruthu na kuiga mfano wake wa unyenyekevu, bidii, na kuonyesha uthamini, imani yetu pia itaigwa na wengine. Hata hivyo, Mungu aliwaandaliaje Ruthu na Naomi? Tutazungumzia jambo hilo katika sura inayofuata.
USIKOSE SEHEMU YA TATU: (a) Ruthu alikuwa akifanya kazi gani? (b) Ruthu alitambua mambo gani mazuri kuhusu Sheria ya Mungu na watu wake?
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW