Friday, June 2, 2017

KISA CHA RUTHU NA NAOMI (SEHEMU YA TATU)

Image may contain: 1 person, meme and text
‘Mwanamke Mwema Sana’
1(a) Ruthu anaendelea kufanya kazi ya namna gani?
(b) Ruthu amejifunza nini kuhusiana na Sheria ya Mungu na watu wake?
Ruth anapiga magoti karibu ya fungo la miganda ya nafaka ya shayiri ambayo aliokota mchana mzima. Bethlehemu kunaanza kuwa giza katika mashamba, na wafanyakazi wengi wanaanza kurudi polepole kwenye mlango wa mji mdogo ulio juu ya kilima kilicho karibu. Ruthu ni mwenye kuchoka sana, alifanya kazi ngumu tangu asubuhi; hata hivyo, anaendelea kutumika, anatumia fimbo ao kipande cha mti ili kupiga-piga miganda yake ili kupata mbegu za nafaka. Hata ikiwa kazi ni ngumu, hiyo ni siku nzuri kabisa kwake kuliko alivyowazia.
Inaonekana hali ya mjane huyo kijana inaanza kubadilika. Kama tulivyoona katika sura ya 4, Ruthu aliamua kushikamana na Naomi, mama-mkwe wake, na aliapa kama atabaki naye na kumfanya Mungu, Mungu wa Naomi awe Mungu wake. Wajane hao wawili walitoka katika inchi ya Moabu na sasa wamefika Bethlehemu, na Ruthu, mwanamuke Mmoabu, amejifunza kwamba Sheria ya Mungu ina mipango fulani mizuri, ambayo inawafanya masikini na wageni katika Israeli waonekane kuwa pia watu. Na sasa anajionea mwenyewe kwamba watu wa Mungu wanatii Sheria hiyo na wanaonyesha wema. Jambo hilo linamugusa na kutuliza kabisa moyo wake wenye kuumia.
(a) Namna gani Boazi alimutia Ruthu moyo?
(b) Namna gani mufano wa Ruthu unaweza kutusaidia wakati huu wa matatizo ya feza?
Boazi ni mumoja kati ya watu hao, tajiri mwenye mashamba, na Ruthu anaokota masalio katika shamba lake. Siku hiyo, mwanaume huyo mwenye kuzeeka anamutendea kama Baba. Ruthu anafurahi sana moyoni mwake, anakumbuka maneno mazuri ya kumupongeza ambayo Boazi alimuambia kwa sababu anamushugulikia Naomi na namna alivyoamua kuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Mungu, Mungu wa kweli.—Soma Ruthu 2:11-14.
Hata hivyo, labda Ruthu anajiuliza sana namna ataishi miaka ijayo. Kwa sababu yeye ni mugeni na masikini, hana bwana wala mtoto, yeye na Naomi wataishi namna gani miaka ijayo? Kuokota tu masalio kutawatimizia mahitaji yao yote? Na ni nani atamutunza atakapozeeka? Ikiwa anahangaishwa na mambo hayo, inaeleweka. Leo pia ni vigumu kupata feza, na watu wengi wanajiuliza maulizo kama hayo. Kujifunza namna imani ya Ruthu ilimusaidia kushinda mahangaiko hayo, kunaweza kutusaidia tuige imani yake katika njia nyingi.
Familia Ni Nini?
(a) Kumuhusu Ruthu, sababu gani tunaweza kusema kwamba siku yake ya kwanza ya kuokota masalio ni siku nzuri?
(b) Naomi anajisikia namna gani anapomuona Ruthu?
Ruthu anapomaliza kupiga-piga mbegu zake na kuzikusanya zote, anashangaa kuona kwamba ameokota karibu efa moja ya nafaka ya shayiri, ni kusema, litre 22. Labda mzigo wake una uzito wa kilo karibu 14! Anaufunga mzigo huo labda ndani ya vazi, anaunyanyua na kuutia kwenye kichwa, na kisha anakamata njia yake mupaka Bethlehemu, wakati huo usiku unaanza kuingia.—Ruthu 2:17.
Naomi anafurahi sana kumuona binti wake mkwe, na labda anashituka na kushangaa anapoona mzigo huo mzito wa nafaka ya shayiri. Ruthu analeta pia chakula chake kilichobaki kutokana na chakula walichokula wakati Boazi aliwapatia wafanyakazi chakula cha mchana, na wote wawili wanachangia chakula hicho. Sasa Naomi anamuuliza: “Uliokota masalio wapi leo, nawe ulifanya kazi wapi? Yule aliyekuona na abarikiwe.” (Ruthu 2:19) Naomi ni muangalifu kabisa; anatambua kwamba Ruthu hakupata chakula kingi hivyo kwa nguvu zake mwenyewe, kunapaswa kuwa na mutu fulani aliyemuhangaikia na kumuonyesha wema.
(a) Naomi anaona kwamba wema wa Boazi unatoka wapi, na sababu gani?
(b) Namna gani Ruthu anaonyesha tena upendo mshikamanifu kwa mama-mkwe wake?
Katika mazungumuzo yao, Ruthu anamuelezea Naomi wema ambao Boazi alimuonyesha. Naomi anaguswa moyo, kwa hiyo anasema: ‘Abarikiwe huyo na Mungu, ambaye hakuacha kuonyesha fazili zake zenye upendo kwa walio hai na wafu.’ (Ruthu 2:20) Naomi anaona kwamba ni Mugu aliyemuchochea Boazi ili amuonyeshe Ruthu wema huo. Ni Mungu anayewachochea watumishi wake kuwa wakarimu na anaahidi kwamba atawabariki kwa sababu ya wema wanaoonyesha. *—Soma Methali 19:17.
Naomi anamushauri Ruthu akubali mambo ambayo Boazi alimuambia: aendelee kuokota masalio katika shamba la Boazi na kubaki karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili wanaume waliokuwa wanafanya kazi ya kuvuna wasimusumbue. Ruthu anakubali shauri hilo. Pia, ‘anaendelea kukaa na mama-mkwe wake.’ (Ruthu 2:22, 23) Maneno hayo yanatusaidia tena kuona sifa kubwa ya Ruthu, ni kusema, upendo mshikamanifu. Je, sisi pia tunashikamana na watu wa familia zetu kwa kuwategemeza kwa ushikamanifu na kuwasaidia wanapohitaji musaada? Mungu hakose hata kidogo kuona upendo mshikamanifu kama huo!
Mfano wa Ruthu na Naomi unaweza kutufundisha nini kuhusu familia?
Je, tunaweza kusema kwamba watu hao wawili tu, Ruthu na Naomi, waliunda familia? Katika sehemu zingine, ili familia iitwe kweli familia, kunapaswa kuwa bwana, bibi, mutoto mwanaume, mtoto mwanamuke, tate (nkambo) na wengine. Lakini mfano wa Ruthu na Naomi unatufundisha kwamba familia za watumishi wa Mungu zinaweza kuwa na furaha, kuonyeshana wema na upendo, hata ikiwa ni familia ndogo sana. Je, wewe unapendezwa na watu wa familia yenu, iwe ni wengi ao wachache? Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kwamba hata wale wasio na familia kati yao wanaweza kupata familia katika kutaniko la Kikristo.—Marko 10:29, 30.
Naomi anapenda kumsaidia Ruthu apate nini?
Ruthu anaendelea kuokota masalio katika shamba la Boazi kuanzia mavuno ya shayiri, Mwezi wa 4 hivi, mpaka mavuno ya ngano, Mwezi wa 5 hivi. Majuma yanapita, na bila shaka, Naomi iko anawaza kile anaweza kumufanyia binti-mukwe wake. Walipokuwa katika inchi ya Moabu, Naomi alisema kwa uhakika kwamba hakuwa na tumaini lolote la kumusaidia Ruthu apate bwana. (Ruthu 1:11-13) Lakini, sasa anaanza kuwaza kama jambo hilo linawezekana. Anamuambia Ruthu hivi: ‘Binti yangu, je, sipaswe kukutafutia mahali pa kupumuzika?’ (Ruthu 3:1) Katika siku hizo, wazazi walikuwa na desturi ya kuwatafutia watoto wao bwana ao bibi. Na kwa sababu Ruthu anakuwa kama binti yake, Naomi anapenda kumtafutia Ruthu ‘mahali pa kupumzika,’ ni kusema, usalama na ulinzi ambao mwanamuke anapata katika nyumba ya bwana yake. Lakini sasa Naomi atafanya nini?
(a) Naomi anaposema kama Boazi ni ‘mkombozi,’ anafikiria mpango gani unaopatikana katika Sheria ya Mungu?
(b) Je, Ruthu alikubali ao alikataa shauri la mama-mkwe wake?
Wakati Ruthu anataja tu jina la Boazi, Naomi anasema: ‘Mwanaume huyo ni wa jamaa yetu. Yeye ni mmoja wa wakombozi wetu.’ (Ruthu 2:20) Alipenda kusema nini? Sheria ambayo Mungu aliwapatia Waisraeli ilikuwa na mipango fulani kwa faida ya familia ambazo zilikuwa katika hali mbaya kwa sababu ya umasikini ao kufiwa. Mjane aliyekuwa bila watoto alikuwa katika hali ya taabu sana, kwa sababu jina la bwana yake lingepotea kabisa na hangekuwa na mrithi katika vizazi vinavyokuja. Kwa hiyo, Sheria ya Mungu ilimuruhusu ndugu ya bwana kuoa mujane huyo ili aweze kuzaa mrithi ambaye angeendeleza jina la bwana yake na kuchunga uriti wa familia. *—Kumbukumbu la Torati 25:5-7.
Naomi anamuelezea Ruthu mpango alio nao. Tunaweza kuwazia namna Ruthu anavyofungua macho kwa mshangao, mama-mukwe wake anapomuelezea mpango huo. Sheria hiyo ni jambo jipya kwa Ruthu; na bila shaka, hajue desturi nyingi za Sheria hiyo. Kwa hiyo, Ruthu anasikiliza kwa uangalifu kila neno Naomi anamuambia; Ruthu ni mwenye kumheshimu sana Naomi. Jambo ambalo Naomi anamshauri kufanya ni jipya kwake, ao la haya, ni kusema, linaomba mutu ajishushe sana, hata hivyo, Ruthu anakubali. Kwa upole anasema hivi: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.”—Ruthu 3:5.
Ruthu alikubali shauri kwa unyenyekevu, mfano wake unatufundisha nini kuhusu kukubali shauri la watu waliozeeka? (Soma pia Ayubu 12:12.)
Wakati fulani ni vigumu kwa vijana kukubali mashauri ya watu waliozeeka ao waliokwisha kuona mambo mengi katika maisha. Ni vyepesi kwao kuwaza kwamba watu hao wenye kuzeeka hawaelewe kabisa magumu na hali yao. Mfano wa unyenyekevu wa Ruthu unatukumbusha kwamba kusikiliza hekima ya watu hao wanaotupenda na wanaotaka tuwe vizuri kunaweza kutuletea baraka. (Soma Zaburi 71:17, 18.) Lakini, ni shauri gani Naomi alimupatia Ruthu, na je, Ruthu alibarikiwa kabisa kwa kufuata shauri hilo?
Uwanja wa kupigia -pigia nafaka ni mahali pa namna gani, na namna gani watu walitumia mahali hapo?
Mangaribi hiyohiyo, Ruthu anaenda kwenye uwanja wa kupigia-pigia nafaka: mahali penye kulala vizuri, penye udongo mgumu ambapo watu wenye mashamba wanaleta nafaka zao ili kuzipiga-piga na kuzipepeta (ao kuzipepula). Mara nyingi uwanja huo unapatikana kwenye mlima ao juu ya mlima, mahali ambapo upepo unavuma sana kisha midi na mangaribi. Ili kupepeta nafaka, wafanyakazi wanatumia chombo kama kanya kubwa ao lupao: wanatupa hewani mbegu zenye kuchanganywa na makapi na kisha upepo unapeperusha makapi (ao maganda ya mbegu) na mbegu zinaanguka chini kwa sababu ni nzito kuliko makapi.
(a) Mambo yalikuwa namna gani hapo kwenye mahali pa kupigia-pigia nafaka wakati Boazi anamaliza kazi yake mangaribi.
(b) Namna gani Boazi anafikia kujua kama Ruthu analala kwenye miguu yake?
Kazi inaanza kumalizika, Ruthu anamuchungulia Boazi mahali alipo. Boazi anasimamia kazi ya kupepeta nafaka zake, ambazo sasa ni marundo makubwa. Anapomaliza kula kwa hamu nyingi, anajilaza kwenye rundo moja la nafaka. Wakati huo watu walizoea kufanya hivyo, labda ili kulinda mavuno yao yasiibwe. Ruthu anaona mahali Boazi anajitayarisha kulala. Anaona kwamba sasa huo ndio wakati wa kutumikisha shauri la Naomi.
Ruthu anakaribia sana, moyo wake unapigapiga. Iko hakika kama Boazi ni mwenye kulala kabisa. Anaenda kwenye miguu ya Boazi, anaifunua na kulala hapo pembeni ya miguu yake; anafanya kabisakabisa vile Naomi alivyomuambia. Kisha anangojea. Wakati unapita. Bila shaka, Ruthu anaona kama wakati unakawia sana. Mwishowe, karibu na katikati ya usiku, Boazi anaanza kutikisika. Anaanza kutetemeka kwa sababu ya baridi, anaamuka ili kufunika tena miguu yake. Lakini, anasikia kwamba kuna mtu fulani hapo. Biblia inasema hivi: ‘Tazama! Mwanamuke alikuwa amelala miguuni pake!’—Ruthu 3:8.
Wale wanaosema kwamba Ruthu alikuwa na mawazo yasiyofaa wanasahau mambo gani mawili?
Boazi anamuuliza: “Wewe ni nani?” Labda kwa sauti yenye kutetemeka, Ruthu anamujibu hivi: ‘Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mfunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mkombozi.’ (Ruthu 3:9) Watu fulani wanaofasiria mambo ya Biblia leo wanasema kwamba tendo na maneno ya Ruthu vilikuwa na kusudi la kumshawishi Boazi ili alale naye. Lakini, watu hao wanasahau mambo mawili: Kwanza, Ruthu alitenda kulingana na desturi za siku hizo ambazo kwa leo zinaweza kueleweka vibaya. Kwa hiyo, ni kosa kumhukumu Ruthu kulingana na namna tunavyoona mambo leo. Ni kweli, leo mwanamuke akifanya hivyo ataonekana kuwa ni kahaba (ao malaya). Jambo la pili, jibu la Boazi linaonyesha waziwazi kama aliona mwenendo wa Ruthu kuwa safi na wenye kusifika sana.
Boazi anasema nini ili kumufariji Ruthu, na namna gani Ruthu alionyesha fazili zenye upendo mara mbili?
Sauti pole ya Boazi na yenye kutuliza inamfariji Ruthu sana. Anamuambia hivi: ‘Yehova na akubariki, binti yangu. Umeonyesha fazili zako zenye upendo kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza. Haukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini ao matajiri.’ (Ruthu 3:10) Ruthu alionyesha upendo mshikamanifu kwa “mara ya kwanza,” kwa kukubali kumsindikiza Naomi aliporudi Israeli na kumshugulikia. Amefanya hivyo “mara hii ya mwisho” kwa kitendo anachofanya sasa. Boazi anajua kwamba kijana mwanamuke kama Ruthu angeweza kutafuta zaidi bwana aliye kijana, awe masikini ao tajiri. Lakini, anataka tu kumtendea Naomi mema na pia baba yake mukwe aliyekufa, ili jina lake lisiondolewe katika inchi. Mwanamuke huyo kijana hatafute faida zake mwenyewe, ndio sababu Boazi anavutiwa naye.
(a) Sababu gani Boazi hamuoe Ruthu mara moja?
(b) Ni nini inayoonyesha kama Boazi anamutendea Ruthu kwa wema na kwamba anamuelewa, pia hatake Ruthu asemwe vibaya?
Boazi anaendelea kumambia: ‘Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia, kwa maana kila mutu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamuke bora [ao mwema] sana.’ (Ruthu 3:11) Wazo la kumuoa Ruthu linamufurahisha Boazi sana; labda hashangazwe kabisa Ruthu anapomuomba awe mkombozi. Hata hivyo, Boazi ni mutu mwenye haki, na kwa hiyo, hataki kutenda kama anavyopenda. Anamuambia Ruthu kama kuna mtu aliye ndugu zaidi katika jamaa ya bwana ya Naomi ambaye ana haki ya kwanza ya kuwa mukombozi; Boazi anapaswa kwanza kumuona mwanaume huyo na kumupatia nafasi ya kuwa bwana ya Ruthu.
Boazi anamuambia Ruthu aendelee kulala mupaka asubuhi mapema; kisha ataondoka bila mtu kumuona. Hapendi watu waseme vibaya juu yake na juu ya Ruthu, kwa sababu wanaweza kuwaza kama walifanya jambo fulani mbaya. Ruthu anaendelea kulala kwenye miguu ya Boazi, inawezekana yeye ni mwenye kutulia sasa kwa sababu Boazi anamujibu vizuri. Sasa usiku unaanza kucha, Ruthu anaamuka. Boazi anajaza kwa ukarimu vazi la Ruthu nafaka nyingi. Ruthu anarudi, anashi ka njia yake mpaka Bethlehemu.—Soma Ruthu 3:13-15.
Ni nini inayofanya Ruthu ajulikane sana kuwa ‘mwanamuke mwema sana,’ na namna gani tunaweza kumuiga?
Ruthu anafurahi sana anapofikiria maneno ambayo Boazi alimuambia, kama yeye anajulikana kuwa ‘mwanamuke mwema sana’! Bila shaka, alijulikana hivyo sanasana kwa sababu alitaka kumjua Mungu na kumtumikia. Pia, alimuonyesha Naomi na watu wake upendo mwingi; kwa sababu bila kulazimishwa alijipatanisha na desturi ambazo hakujua hapo mbele. Tukiiga imani ya Ruthu, tutawaheshimu wengine sana hata ikiwa hali yao ya maisha iko namna gani ao desturi zao. Tukifanya hivyo, sisi pia tunaweza kujulikana kuwa watu wazuri.
(a) Vipimo sita ambavyo Boazi anamupatia Ruthu vinaweza kumaanisha nini? (Soma pia maelezo yaliyo chini.)
(b) Sasa Naomi anamupatia Ruthu shauri gani?
Ruthu anafika nyumbani, Naomi anamuuliza: “Wewe ni nani, binti yangu?” Labda Naomi anauliza hivyo kwa sababu kungali bado giza na hivyo hamuone vizuri, ao anapenda kujua ikiwa mambo yamemuendea Ruthu vizuri na kwa hiyo kuna tumaini la kuolewa. Mara moja Ruthu anamuelezea jinsi mambo yalivyopita kati yake na Boazi. Pia anamuonyesha zawadi ya ukarimu, ni kusema, nafaka ambayo Boazi alimtumia Naomi. *—Ruthu 3:16, 17.
Naomi anampatia Ruthu shauri la hekima: kubaki nyumbani siku hiyo kuliko kuenda kuokota masalio katika shamba. Anamuhakikishia Ruthu hivi: ‘Mwanaume huyo hatapumuzika mpaka amalize jambo hilo leo.’—Ruthu 3:18.
(a) Namna gani Boazi anaonyesha kama yeye ni mutu wa haki na asiyetafuta faida zake mwenyewe?
(b) Ruthu anabarikiwa namna gani?
Naomi hadanganyike. Siku hiyohiyo, Boazi anaenda kwenye mlango wa mji, mahali ambapo wazee wa mji wanazoea kukutana, na anangojea mupaka yule mwanaume wa jamaa ya karibu ya Elimeleki anapopita hapo. Mbele ya mashahidi, Boazi anampatia nafasi ya kuwa mkombozi na kumuoa Ruthu. Lakini, mwanaume huyo anakataa, anaonyesha kwamba akifanya hivyo atapoteza uriti wake mwenyewe. Kisha, mbele ya mashahidi hao wanaokusanyika kwenye mlango wa muji, Boazi anaonyesha kwamba yeye atakuwa mkombozi huyo; atanunua shamba la Elimeleki, bwana ya Naomi, na kumuoa Ruthu, bibi ya Maloni, mtoto wa Elimeleki. Boazi anaonyesha sababu: Anataka ‘kumuinulia mwanaume aliyekufa jina katika uriti wake.’ (Ruthu 4:1-10) Kwa kweli, Boazi ni mwanaume mwenye haki na asiyetafuta faida zake mwenyewe.
Boazi anamuoa Ruthu. Kisha, Biblia inasema hivi: ‘Mungu akamuwezesha kupata mimba naye akazaa mwana.’ Wanawake wa Bethlehemu wanamubariki Naomi na kumusifu Ruthu kwa sababu alimufaa Naomi kuliko watoto saba wanaume. Mwishowe, mutoto wa Ruthu akawa nkambo ao tate wa Mfalme Daudi. (Ruthu 4:11-22) Na kisha Yesu Kristo akatokea katika uzao wa Daudi.—Mt. 1:1. *
Mifano ya Ruthu na Naomi inatukumbusha nini?
Ruthu alibarikiwa kweli, na Naomi pia, ambaye alisaidia kumlea mtoto huyo kama mtoto wake. Maisha ya wanawake hao wawili yanatukumbusha kabisa kwamba Mungu anaona wale wote, ambao kwa unyenyekevu, wanatumika kwa bidii ili kutegemeza familia zao na pia wanatumika kwa uaminifu pamoja na watu wake. Mungu hakose kamwe kuwabariki watu waaminifu, kama vile Boazi, Naomi, na Ruthu.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW