Saturday, April 15, 2017

KWA NINI WAISRAELI WANASHEREHEKEA PASAKA KWA ZAIDI YA MIAKA 3500?

Image may contain: one or more people, crowd, outdoor and text
“Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova.”— Kutoka 12:14.
Ni sherehe ya Pasaka. Ilikuwa sherehe ya kukumbuka kukombolewa kwa taifa la kale la Israeli kutoka utumwani huko Misri. Tukio hilo linapaswa kuwa muhimu kwako. Kwa nini? Kwa sababu linahusiana na mambo fulani muhimu maishani mwako.
Hata hivyo, huenda ukasema: ‘Wayahudi ndio wanaosherehekea Pasaka, lakini mimi si Myahudi. Inanihusuje?’
Maneno haya muhimu yanajibu swali hilo: “Kristo pasaka yetu ametolewa dhabihu.” (1 Korintho 5:7) Ili tuelewe vizuri umuhimu wa maneno hayo ya kweli, tunahitaji kuijua Pasaka ya Wayahudi na kuona jinsi inavyohusiana na amri fulani waliyopewa Wakristo wote.
Ni nini kilichotukea kabla ya Pasaka ya kwanza?
Baada ya Waisraeli kuwa watumwa kwa miaka mingi huko Misri, Mungu alimtuma Musa na Haruni ndugu yake, wakamwambie Farao awaachilie huru watu Wake. Mtawala huyo wa Misri mwenye kiburi alikataa kuwaruhusu Waisraeli waende zao, hivyo Mungu akaipiga nchi ya Misri kwa mfululizo wa mapigo yenye kuangamiza. Mwishowe, Mungu alileta pigo la kumi lililoua wazaliwa wote wa kwanza Wamisri, na hivyo Farao akawaacha Waisraeli waende zao.— Kutoka 1:11; 3:9, 10; 5:1, 2; 11:1, 5.
Hata hivyo, Waisraeli walipaswa kufanya nini kabla ya kuachiliwa huru?
Ulikuwa wakati wa majira ya kuchipua ya mwaka wa 1513 K.W.K., katika mwezi wa Kiebrania wa Abibu, uliokuja kuitwa Nisani, wakati ambapo saa za mchana hulingana kwa urefu na saa za usiku. * Mungu alisema kwamba katika siku ya kumi ya mwezi huo, Waisraeli walipaswa kuanza kujitayarisha kufanya mambo fulani Nisani 14. Siku hiyo ilianza jua lilipotua kwa kuwa kulingana na Waebrania, siku ilianza na kwisha jua lilipotua. Katika Nisani 14, kila familia ilipaswa kuchinja kondoo dume (au mbuzi), kuchukua sehemu ya damu na kuipaka juu ya miimo ya mlango na sehemu ya juu ya mlango wa nyumba. (Kutoka 12:3-7, 22, 23) Kila familia ilipaswa kumla mwana-kondoo aliyechomwa kwa moto, mboga, na mkate usiotiwa chachu. Malaika wa Mungu angepita katikati ya nchi na kumchinja kila mzaliwa wa kwanza wa Misri, lakini Waisraeli waliotii wangelindwa, kisha Farao angewaruhusu waende zao.—Kutoka 12:8-13, 29-32.
Hivyo ndivyo ilivyotukea, na Waisraeli walipaswa kuendelea kukumbuka ukombozi wao.
Mungu aliwaambia hivi: “Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote.
Nanyi mtaisherehekea kama sheria mpaka wakati usio na kipimo.” Mwadhimisho huo uliofanywa siku ya 14 ulifuatiwa na sherehe ya siku saba. Nisani 14 ndiyo iliyokuwa siku ya Pasaka, lakini siku zote nane za sherehe hiyo ziliitwa pia Pasaka. (Kutoka 12:14-17; Luka 22:1; Yohana 18:28; 19:14) Pasaka ilikuwa mojawapo ya sherehe rasmi (Sikukuu) ambazo Wayahudi walipaswa kusherehekea kila mwaka.—2 Nyakati 8:13.
Acheni tufikirie tena kilichotukia Misri. Musa alisema kwamba watu wa Mungu wangeendelea kusherehekea Pasaka; ilipaswa kuwa sharti “mpaka wakati usio na kipimo.” Wakati wa sherehe hiyo ya kila mwaka, watoto waliwauliza wazazi wao maana ya tukio hilo. (Soma Kutoka 12:24-27; Kumbukumbu 6:20-23) Kwa hiyo, Pasaka ingekuwa “ukumbusho” hata kwa watoto.—Kutoka 12:14.
Wakristo wa kweli hawasherehekei Pasaka ya Kiyahudi. Sherehe hiyo ilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa, na hatuko chini ya Sheria hiyo. (Roman 10:4; Kolosai 2:13-16) Hata hivyo, tunakumbuka kwa uthamini kifo cha Mwana wa Mungu. Lakini kuna mambo fulani katika sherehe ya Pasaka iliyoanzishwa huko Misri yaliyo na maana kwetu.
Mwana-kondoo alipochinjwa kwa ajili ya mlo wa Pasaka, Waisraeli hawakupaswa kuvunja mfupa wake wowote. (Kutoka 12:46; Hesabu 9:11, 12)
Namna gani YESU “Mwana-Kondoo wa Mungu” aliyekuja kutoa fidia?
(Yohana 1:29) Alitundikwa mtini katikati ya wahalifu wawili. Wayahudi walimwomba Pilato aagize mifupa ya wanaume hao waliotundikwa ivunjwe. Hilo lingefanya wafe haraka na hivyo kuondolewa juu ya miti kabla ya Nisani 15, siku ya Sabato kuu. Askari-jeshi walivunja miguu ya wahalifu wawili waliotundikwa, “lakini walipokuja kwa Yesu, kwa kuwa waliona kwamba tayari alikuwa amekufa, hawakuivunja miguu yake.” (Yohana 19:31-34) Vivyo hivyo, mwana-kondoo wa Pasaka hakuvunjwa miguu. Kwa njia hiyo, mwana-kondoo huyo alikuwa “kivuli” cha jambo ambalo lingetukia Nisani 14, mwaka wa 33 W.K. (Ebrania 10:1) Isitoshe, mambo hayo yalitimiza Zaburi 34:20, na hilo linapaswa kuimarisha uhakika wetu katika unabii.
Ndio maana hii leo, sisi Wakristo tunasherekea Pasaka kwasabau Yesu ni dhabihu bora zaidi inayoweza kuokoa uhai milele.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW