Sunday, January 19, 2014

TABIA NA KAZI ZA ROHO MTAKATIFU

Katika mistari hii, tunajifunza kuhusu tabia na kazi za Roho Mtakatifu. Ingawa Roho Mtakatifu ana tabia na kazi nyingi zaidi kuliko zile zilizoorodheshwa hapa, hata hivyo, katika mistari hii, tunajifunza tabia na kazi zake za msingi. Zifuatazo ni kazi za Roho Mtakatifu zinazotajwa katika mistari hii:-

KUUHAKIKISHIA ULIMWENGU KWA HABARI YA DHAMBI: – 
Watu wote ambao hawamwamini Yesu, wanafanya dhambi (MST. 9). Watu wengi ingawa hawamwamini Yesu, hujihesabia haki kutokana na amtendo yao kama Farisayo yule katika LUKA 18:9-14. Watu wengi hujihesabia haki na kujiona kwamba hawana dhambi, kwa kuwa wanashika taratibu zote za dini zao, kama walivyofundishwa (MATENDO 26:4-5; WAGALATIA 1:14). Kutokana na msingi huu, Sauli alijihesabia haki na kuona kwamba yeyote ambaye alikuwa hafuati taratibu zote za dini yake, ndiye mwenye dhambi na alifaa hata kuuawa. Aliposikia sauti ya Yesu ikisema, Sauli! Sauli! Mbona waniudhi? Alishangaa, maana aliona anatenda haki yote. Tukitoka na kwenda kuwahubiria watu wa jinsi hii ya Farisayo na Sauli, na kutaka waokolewe, bila msaada wa Roho Mtakatifu, hatuwezi kufanikiwa, kwa sababu wao watajiona kuwa hawana dhambi na kutuona sisi ndiyo tuliopotea kwa sababu hatuko katika dini zao! Mtu ambaye havuti sigara, hanywi pombe, haibi, hafanyi ushirikina, haui au hatukani matusi, mtu wa namna hii ni vigumu kumshawishi kwamba ana dhambi, na kumtaka atubu na kuokolewa, kwa kumfundisha tu kwamba, sisi sote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu tangu kuzaliwa (ZABURI 51:5; WARUMI 3:10-12, 23; 1 YOHANA 1:8-10). Sasa basi, ni kazi ya Roho Mtakatifu kumfanya kila mtu wa namna hii, anayejihesabia haki, kushtakiwa na dhamiri yake na kujiona hafai na ni mwenye dhambi (YOHANA 8:3-9). Ndiyo maana, tukitoka kuwahubiri watu na kutegemea ujuzi wetu tu wa maandiko bila msaada wa Roho Mtakatifu, hatuwezi kupata matokeo makubwa. Hatuna budi wakati wote kuitambua kazi hii ya roho Mtakatifu, na kumkaribisha aambatane pamoja nasi kila tunaposimama kuhubiri au kufundisha ili ashuhudie pamoja nasi (YOHANA 15:26-27). Tukifanya hivi, huduma zetu zitakuwa na mafanikio makubwa. Hatuna budi kupokea uwezo utokao juu, Nguvu ya Roho Mtakatifu ili tuwe mashahidi wa Yesu wenye uwezo wa kuwaleta wenye dhambi wengi kwa Yesu (LUKA 24:48-49; MATENDO 1:4,8).

KUUHAKIKISHIA ULIMWENGU KWA HABARI YA HAKI: – Ni kazi ya Roho Mtakatifu kumhakikishia kila tunayemhubiri kwamba Yesu Kristo pekee ndiye mwenye haki na tunahesabiwa haki kwa kumwamini Yeye tu (1 YOHANA 2:1). Roho Mtakatifu akitenda kazi hii humfanya mtu akiri kwamba Yesu ndiye mwenye haki, kama ilivyokuwa kwa akida katika LUKA 23:47. Vivyo hivyo, Roho Mtakatifu huwahakikishia watu tunaowahubiria kwamba maneno yale tunayoyasema ndiyo ya haki, na kweli., kuliko yale waliyojifunza katika dini zao. Tukiwa na Roho Mtakatifu, hatuna haja ya kutumia Misahafu ya dini nyingine kuwahakikishia watu tunavyowahubiri. Kufanya hivyo, ni ubatili, maana ni kuvithibitisha vitabu hivyo kwamba vina ukweli, na hilo haliwezi kuleta matokeo.


KUUHAKIKISHIA ULIMWENGU KWA HABARI YA HUKUMU: – 


Watu wengi wenye dhambi, hawaamini kwamba kuna hukumu ya kutupwa motoni baada ya kufa, na kuona kama ni mbinu za kuwaanya waache starehe za dunia. Watu wengi pia hawaamini kwamba wanaweza kusamehewa dhambi zao kabisa na kufutiwa hukumu, na hudhani kwamba hata wafanyeje kama wameandikiwa motoni basi. Kazi ya roho Mtakatifu, ni kumhakikishia mtu tunayemhubiria kwamba ni kweli kuna hukumu baada ya kufa na Mhukumu wa Ulimwengu huu ni Yesu. Vilevile humhakikishia kwamba Mkuu wa Ulimwengu Shetani, yeye amekwisha kuhukumiwa kutupwa katika moto wa milele, na hana nafasi ya kusamehewa, laki8ni sisi tuna nafasi ya kufutiwa hukumu tukimwamini Yesu (WAEBRANIA 9:27; MATHAYO 25:41; YOHANA 3:18, 36). Kwa msaada wa Roho Mtakatifu ndipo mtu anapoweza kusema kama mhalifu msalabani katika LUKA 23:39-42.

KUWAONGOZA WATU NA KUWATIA KWENYE KWELI YOTE: – Roho Mtakatifu, huwaongoza watu na kuwaonyesha njia ya kweli. Anaweza hata kusema na watu kwa njia ya ndoto kama mkewe Pilato (MATHAYO 27:19), na kuwaelekeza waende kusali Kanisa fulani, waende katika mkutano fulani wa Injili n.k. Roho Mtakatifu huwapeleka watu kwenye kweli. Ndiyo maana tukiwa hatuhubiri kweli katika makanisa yetu, tutaona watu wengi wanachomoka na kuhama wakiongozwa na Roho Mtakatifu kwenye kweli yote, na kwa kukosa ufahamu, tutalalamika kwemba watu wetu WANAIBIWA! Roho Mtakatifu hawaibi! Ni watu wake! Roho Mtakatifu huwaongoza watu kwa wingu na moto (HESABU 9:15-23). Tabia za Roho Mtakatifu, ni pamoja na hizi zifuatazo tunazojifunza katika mistari hii:

HANENI KWA SHAURI LAKE MWENYEWE: – Maneno ya Roho Mtakatifu SIKU ZOTE hufanana na maneno ya Yesu, hayatofautiani kamwe maana Roho Mtakatifu hutwaa katika yaliyo ya Yesu na kutupasha habari (MST. 13-15). Yeye ni roho wa kweli, na Yesu ndiye Kweli, hivyo ni sawa pia kusema Yeye ni Roho wa Yesu (MATENDO 16:7). Roho Mtakatifu, hushuhudia pamoja na Baba na Mwana (1 YOHANA 5:8). Hivyo mtu akisema ameongozwa na Roho Mtakatifu kumwacha mkewe na kumwoa mke mwingine, ni dhahiri kwamba huyo siyo Roho Mtakatifu, maana Yesu alisema amwachaye mkewe na kumwo mwingine azini, na Baba anachukia kuachana (LUKA 16:18; MALAKI 2:15-16). Ujumbe au unabii wowote unaodaiwa kwamba unatokana na Roho Mtakatifu, kwa msingi huu, lazima tuupime kwa Neno la Mungu.

NI ROHO WA KWELI: – Hasemi uongo, hivyo ujumbe unaotokana na Roho Mtakatifu unaotupasha habari ya mambo yajayo, hauna budi kutimia. Hata hivyo, hata ukitimia, lakini unatutoa mbali na kweli ya Neno la Mungu, tujue pia siyo wa Roho Mtakatifu (KUMBUKUMBU 13:1-4). Inatupasa kuwa waangalifu nyakati za leo kuweka mawazo yetu katika unabii, Roho hutumia njia hii leo mara chache sana, maana anasema nasi leo katika Neno la Mwana wa Mungu Yesu (WAEBRANIA 1:1-2).

Katika Matendo ya Mitume, tunaona jumbe chache sana za Roho Mtakatifu kwa miaka mingi!

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW