Saturday, August 22, 2015

YESU NI UPENDO (SEHEMU YA KWANZA)

Shetani anataka tuamini nini kuhusu jinsi Yesu anavyotuona, lakini Yesu anatuhakikishia nini?
Hata hivyo, swali muhimu linazuka: Je, Mungu anampenda kila mmoja wetu?
Baadhi ya watu wanakubali kwamba Mungu anawapenda wanadamu kwa ujumla kama andiko la Yohana 3:16 linavyosema. Lakini wanahisi hivi: ‘Mungu hawezi kamwe kunipenda mimi.’ Shetani Ibilisi anataka sana tuamini kwamba Yesu hatupendi wala hatuthamini. Kwa upande mwingine, Yesu anatuhakikishia kuwa anamthamini kila mmoja wa watumishi wake waaminifu hata kama tunafikiri hatupendwi au hatuthaminiwi.

Kwa mfano, fikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:29-31. Yesu alitoa mfano huu ili kuonyesha kwamba wanafunzi wake wana thamani: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” Hebu fikiria jinsi wasikilizaji wa Yesu katika karne ya kwanza walivyoyaelewa maneno hayo.

Katika siku za Yesu, shore alikuwa ndege wa bei rahisi sana aliyenunuliwa ili kuliwa. Mtu aliyelipa sarafu moja ya thamani ndogo sana, alipewa shore wawili. Lakini kulingana na andiko la Luka 12:6, 7, baadaye Yesu alisema kwamba mtu aliyelipa sarafu mbili, alipewa shore watano badala ya shore wanne. Shore mmoja aliongezwa kana kwamba hakuwa na thamani yoyote. Huenda ndege hao hawakuwa na thamani machoni pa wanadamu, lakini Muumba aliwaonaje? Yesu alisema: “Hakuna hata mmoja wao [hata yule aliyeongezwa] hupata kusahaulika mbele ya Mungu.” Sasa huenda tumeanza kuelewa alilomaanisha Yesu. Ikiwa Mungu anamthamini sana shore mmoja, namna gani mwanadamu! Kama Yesu alivyosema, Mungu Baba anatujua vizuri sana. Kwani, hata nywele za kichwa chetu zimehesabiwa zote!

Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hakutia chumvi aliposema kwamba nywele za kichwa chetu zimehesabiwa?
Huenda wengine wakafikiri kwamba Yesu alitia chumvi. Hata hivyo, hebu fikiria ufufuo. Ni lazima Mungu Baba awe anatujua vizuri sana ili aweze kutuumba upya! Anatuthamini sana hivi kwamba anakumbuka kila jambo, hata chembe zetu za urithi, kumbukumbu, na ujuzi wetu wote. Kichwa cha mtu huwa na nywele 100,000 hivi, kwa hiyo kuhesabu nywele za vichwa vyetu ni jambo rahisi sana ikilinganishwa na kukumbuka mambo hayo yote. Bila shaka, maneno hayo ya Yesu yanatuhakikishia kabisa kwamba Mungu Baba anamjali kila mmoja wetu.

Kisa cha Mfalme Yehoshafati kinaonyeshaje kwamba Mungu hutafuta mema ndani yetu ingawa sisi si wakamilifu?
Biblia hufunua jambo lingine linalotuhakikishia kwamba Mungu anatupenda. Yeye hutafuta na huthamini mema yaliyo ndani yetu. Kwa mfano, fikiria Mfalme Yehoshafati aliyekuwa mwema. Mfalme huyo alipotenda jambo la kipumbavu, nabii wa Mungu alimwambia hivi: “Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa BWANA.” Ulikuwa ujumbe wenye kuogofya kama nini! Lakini ujumbe wa Mungu haukukomea hapo. Uliendelea kusema hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:1-3) Kwa hiyo, hasira adilifu ya Mungu haikumzuia asione “mema” yaliyokuwa ndani ya Yehoshafati. Inatia moyo sana kujua kwamba Mungu wetu hutafuta mema ndani yetu hata ingawa sisi si wakamilifu.

Kumbuka kuwa Yesu anakupenda.

Max Shimba

Max Shimba Ministries @ 2015

YESU NI UPENDO (SEHEMU YA PILI)

Huruma ni sehemu nyingine ya upendo wa Yesu.

Huruma ni nini? Katika Biblia, huruma na rehema zinahusiana sana. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, mara nyingi kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ hutafsiriwa “onyesha rehema” au “sikitikia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yesu anatumia kujihusu, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” linaloweza kufasiriwa kuwa “huruma ya mama.”

Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yesu. Andiko la Isaya 49:15 linasema: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie [ra·chamʹ] mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwa kweli, mtoto mchanga ni dhaifu; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Ingawa hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika ‘nyakati hizi za hatari.’ (2 Timotheo 3:1, 3) “Lakini mimi sitakusahau wewe,” atangaza Mungu. Huruma nyororo ya Yesu ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga.

Waisraeli walipatwa na nini katika nchi ya Misri ya kale, naye Mungu aliitikiaje kilio chao?
Mungu huonyeshaje sifa ya huruma akiwa kama mzazi mwenye upendo? Sifa hiyo ya huruma inaonekana wazi kutokana na jinsi alivyolitendea taifa la Israeli la kale. Kufikia mwisho wa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa huko Misri. (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Mungu awasaidie walipokuwa wakiteseka. Je, Mungu mwenye huruma nyororo aliitikiaje?

Mungu aliwahurumia. Akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao . . . maana nayajua maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Mungu hangeweza kuwatazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao na asiwahurumie. Yehova ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Nayo hisia-mwenzi, yaani, sifa ya kuguswa moyo na uchungu wa wengine, inahusiana sana na huruma. Lakini Mungu hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 linasema: “Kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” Mungu wa Israel aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri kwa “mkono hodari.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.

(a) Maneno ya mtunga-zaburi yanatuhakikishiaje kwamba Mungu anamjali sana kila mmoja wetu? 
(b) Mungu hutusaidia katika njia gani mbalimbali?
Mungu hawahurumii watumishi wake tu wakiwa kikundi. Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Anajua kabisa mateso yoyote yanayoweza kutupata. Mtunga-zaburi alisema: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:15, 18) Mungu anamsaidiaje kila mmoja wetu? Si lazima aondoe jambo linalofanya tuteseke. Lakini yeye amewapa maandalizi tele wale wanaomwomba msaada. Neno lake lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kutusaidia sana. Katika kutaniko, Mungu ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao hujitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” Mungu huwapa “Roho Mtakatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2, NW; Luka 11:13) Maandalizi hayo yote ni uthibitisho wa “huruma nyororo ya Mungu wetu.”—Luka 1:78.

Utaitikiaje upendo wa Yesu?
Je, si jambo lenye kusisimua kutafakari juu ya upendo wa Baba yetu wa mbinguni? Katika makala iliyotangulia, tulikumbushwa kwamba Baba Mungu ameonyesha nguvu, haki, na hekima yake kwa njia ya upendo ili kutunufaisha. Na katika makala hii tumeona kwamba kwa njia ya pekee, Mungu ameonyesha upendo wake moja kwa moja kwa kila mmoja wetu na kwa wanadamu kwa ujumla. Sasa kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Nitaitikiaje upendo wa Yesu?’ Na uitikie kwa kumpenda kwa moyo wako wote, kwa nafsi yako yote, kwa akili yako yote, na kwa nguvu zako zote. (Marko 12:29, 30) Maisha yako ya kila siku na yaonyeshe kwamba una tamaa ya kutoka moyoni ya kumkaribia Mungu hata zaidi. Na Yesu, Mungu ambaye ni upendo, na akukaribie hata zaidi—milele!—Yakobo 4:8.
Mungu awabariki sana.

Yesu anakupenda.

Max Shimba

Max Shimba Ministries @ 2015.

YESU NI UPENDO (SEHEMU YA TATU)

Yesu ni Mungu Aliye “Tayari Kukusamehe Dhambi”
Tunapofanya dhambi tunakuwa na hisia gani zenye kulemea, lakini tunaweza kunufaikaje na msamaha wa Yesu?

Tunapofanya dhambi, sisi huona aibu, hukata tamaa, na kuhisi hatia na huenda hali hiyo ikafanya tufikiri kwamba hatustahili kabisa kumtumikia Mungu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Mungu ‘amekuwa tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Naam, Yesu anaweza kutusamehe dhambi zetu tunapotubu na kujitahidi kabisa kutozirudia. Ona jinsi Biblia inavyofafanua sehemu hiyo yenye kuvutia ya upendo wa Yehova.

Yesu Kristo anayo amri na mamlaka ya kusamehe dhambi

Kuna jambo lililowahi kutokea hadi likawashangaza watu; hebu fatilia kisa hiki. Biblia Takatifu inasema kwamba:

“Wakaja watu wakimleta mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne. Na walipokuwa hawawezi kumkaribia (Yesu) kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo; na wakiisha kuivunja wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza. Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako. Na baadhi ya waandishi waliokuwako huko, wameketi, wakifikiri mioyoni mwao, Mbona huyu anasema hivi? Anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu?

Mara Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu? Vyepesi ni vipi, kumwambia mwenye kupooza, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, ujitwike godoro lako, uende?

Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi – Akamwambia yule mwenye kupooza,

Nakuambia, Ondoka, ujitwike godoro lako uende nyumbani kwako.
Mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote; hata wakastajabu wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Namna hii hatujapata kuiona kamwe.” (Marko 2:3-12)

Kwa Wayahudi uponyaji haukuwa kitu kigeni kwao kwani hata manabii enzi za Agano la Kale nao walitumia nguvu za Mungu kuponya wagonjwa; lakini, jambo lililoonekana geni kwa Wayahudi ni kusikia Yesu amesema 
“...Umesamehewa dhambi zako...” (Marko 2:5) Kauli hiyo ya Yesu iliwafanya waone kwamba Yesu AMEKUFURU kwa maana mwenye mamlaka ya kusamehe dhambi ni Mungu pekee. Watu hao walidhani Yesu amekufuru kwa sababu hawakujua kuwa Yesu ni Mungu ingawa alikuwa ameuvaa mwili wa kibinadamu kama sisi.

Ukimpokea Yesu; anakusamehe dhambi zako zote. Haijalishi umetenda dhambi nyingi kiasi gani; haijalishi hali uliyonayo hivi sasa. Fahamu kwamba Yesu anakupenda. Neno la Mungu linasema kwamba:

“...asema BWANA. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji...” (Isaya 1:18)

Mungu huweka dhambi zetu mbali nasi kadiri gani?
Mtunga-Zaburi Daudi alitumia usemi mwingine ulio wazi zaidi kufafanua msamaha wa Mungu: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.” (Zaburi 103:12, italiki ni zetu.) Mashariki ni mbali kadiri gani kutoka magharibi? Katika maana fulani, sikuzote mashariki huwa mbali kabisa na magharibi; pande hizo mbili haziwezi kamwe kukutana. Msomi mmoja anasema kwamba usemi huo unamaanisha “mbali iwezekanavyo; mbali kabisa.” Maneno ya Daudi yaliyoongozwa na Roho ya Mungu yanatuambia kwamba Mungu anapotusamehe, anaweka dhambi zetu mbali kabisa nasi.

Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu hutuona kuwa safi baada ya kutusamehe dhambi zetu?
Je, umewahi kujaribu kuondoa doa katika nguo nyeupe? Huenda hukufaulu kuondoa doa hilo ingawa ulijitahidi kadiri unavyoweza. Ona jinsi Mungu anavyoeleza msamaha wake: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18, italiki ni zetu.) Usemi “nyekundu sana” unaonyesha kwamba rangi hiyo ni nyangavu.* Rangi “nyekundu” ilikuwa mojawapo ya rangi zilizotiwa kwenye nguo. Hatuwezi kamwe kuondoa doa la dhambi kwa jitihada zetu. Lakini Yesu anaweza kuondoa dhambi ambazo ni nyekundu sana na kuzifanya kuwa nyeupe kama theluji au sufu isiyotiwa rangi. Kwa hiyo, Yesu anapotusamehe dhambi zetu, hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote.

Ni katika maana gani Mungu hutupa dhambi zetu nyuma yake?
Hezekia alimwambia Mungu hivi katika wimbo wa shukrani wenye kugusa moyo ambao alitunga baada ya kuponywa ugonjwa wa kufisha: “Umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako.” (Isaya 38:17, italiki ni zetu.) Ni kana kwamba Mungu anachukua dhambi za mtenda-dhambi mwenye kutubu na kuzitupa nyuma Yake ambako Hawezi tena kuziona wala kuzikazia fikira. Kichapo kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba andiko hilo linaweza kuelezwa hivi: ‘Umefanya iwe ni kana kwamba sikufanya dhambi.’ Je, hilo si jambo lenye kufariji?

Nabii Mika anaonyeshaje kwamba Mungu anapotusamehe Anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu?
Katika ahadi ya urudisho, nabii Mika alieleza usadikisho wake kwamba Mungu Yehova angewasamehe watu wake wenye kutubu: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye . . . kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? . . . Nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.” (Mika 7:18, 19, italiki ni zetu.) Hebu fikiria maana ya maneno hayo kwa watu walioishi nyakati za Biblia. Haingewezekana kupata tena kitu kilichotupwa “katika vilindi vya bahari.” Kwa hiyo maneno ya Mika yanamaanisha kwamba Yesu anapotusamehe, anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu.

Yesu ni Mungu, endapo ukimpokea atakusamehe dhambi zote ulizozitenda. Yesu anakupenda sana. Hebu leo mpe Yesu maisha yako ayatawale; Yesu ataiondoa kiu hiyo ya kutenda dhambi ikufanyayo ushindwe kujizuia kuwaka tamaa mbaya za mwili wako; Yesu atakupatia ulinzi ambao utazuia pepo wachafu wasiingilie maisha yako; Yesu atakubariki na kufungua tumbo lako lililokosa mtoto kwa muda mrefu wote huo unaotaabika hata sasa; Yesu atawarejesha kwako watoto wako ambao wamekataa kukutii hata wametoweka kwako; Yesu atakupatia uzima na kuyaondoa magonjwa yote hayo yanayokutesa hata sasa; Yesu atakubariki na kukupatia uzima wa milele.

Kwa kweli nashindwa kuuelezea kwa ufasaha zaidi upendo wa Yesu juu yako kwa maana wewe ni wathamani kubwa sana mbele za Mungu. Mimi nachoweza kukwambia ni kwamba: Yesu anakupenda tena hataki upotee. Mpe Yesu maisha yako sasa ili ufurahie uzuri wa pendo Lake.

Damu ya Yesu inamamlaka ya kusafisha dhambi zako zote.

Mpokee Yesu sasa na upate msamaha wa dhambi.

Yesu anakupenda.

Max Shimba

Max Shimba Ministries @2015.

YESU NI UPENDO (SEHEMU YA NNE)


Ndugu yangu, wajua yakwamba Yesu Kristo anakupenda ? Wajuwa yakwamba alisulubiwa kwa ajili ya watu wote: Wanaume na Wanawake, Watoto, Vijana na Wazee?  Yesu Kristo alikufa kwa ajili yako.

Yesu anakupenda sana, inawezekana kuna mtu anakupenda sana ila Yesu anakupenda zaidi ya wote duniani hivyo nakushauri ukate shauri umfuate yeye maana atakupa kustarehe milele na kuurithi ufalme wa mbinguni pamoja naye.

TAFAKARI: “Yesu anakupenda upeo, amepoteza kila kitu, na kufa kifo cha aibu ili asikupoteze.”


JE, WEWE UPO KATIKA KUNDI HILI?
…Wewe ni mnyanganyi, mwizi, mwongo, muuaji, usiye kuwa na ukweli? Yesu anakupenda na anataka kukuponya.


JE, WEWE UPO KATIKA KUNDI HILI?
…Wewe ni mlozi mkubwa mwenye kutumikia Shetani, tangu ujana wako unazuru wanadamu wengine, unaua watoto, wanawake hata wanaume, unaharibu mavuno, unatawanya magonjwa toka jamaa kwa ingine, unaua hapa na pale.Unapopita ni woga mtupu na kukimbia mbali sababu ya mapepo mabaya yako. Mara na mara unajiuliza nini ulikuja kufanya hapa duniani, ukitafuta kujua sababu ya mabaya yote unayoyatenda. Unajiuliza namna gani uliweza kufikia hapo. Fahamu neno moja tu, hata unaishi mabaya haya yote : Yesu anakupenda na anataka kukuponya.


JE, WEWE UPO KATIKA KUNDI HILI?
…Wewe ni mkoma,tangu miguu hadi kichwani. Ulipoteza vidole, sikio, pua, ukageuka kilema kwa namna fulani; fahamu jambo hili: Yesu anakupenda na anataka kukuponya.


JE, WEWE UPO KATIKA KUNDI HILI?
… Wewe ni msichana, waonekana kuwa ni mrembo sana na wakati wako wote unavunja jamaa za wengine. Unapotosha rafiki zako za darasa, za shule lako, za ofisi ao za mtaa wako. Mara nyingine ulitoa mimba, ulitafuta kupatia wengine sumu, ao uligonganisha wapenzi wako: wamoja wafariki ao wangali wagonjwa sana sababu yako, sababu ya unyofu wako, na sura yako nzuri sana. Sasa wajiuliza mengi kuhusu maisha yako: uliweza kutambua mabaya yote uliyotenda na unajiuliza nini Mungu atakayokutendea.

 Unapatwa na woga wakati unawaza haya yote sababu unaambiwa yakuwa siku moja Mungu atahukumu matendo ya watu.Unaishi katika uasi, unajua ya kwamba JEHENAMU ndiyo inakungojea na unajifariji ukisema kwamba ni maneno yasiyokuwa na msingi hata unasema : Mungu hayuko!



…Wewe ni kijana uliyetenda mambo sawasawa na yale na mwisho ukafikia kusema hivyo. Unajitia kwa mstari ya wale wasiosadiki kuwa Mungu yuko, ili ujitulize.

Ndugu yangu, rafiki yangu, Shetani anakupoteza. Unajuwa ni nini inayokungojea. Hata ikiwa hivyo, ninataka kukujulisha ya kwamba wakati ungali wa kugeuza yale yote, kwani katika upendo wake Mungu alituma Mwana wake wa pekee ili akuondoshe katika maisha yale. Yesu anakupenda, anataka akuokowe kwa damu yake na uwe safi mbele ya Mungu.

…Wewe ni mwanaume, mwanamke, mtoto unayelala kitandani katika hospitali sababu ya ugonjwa, ya msiba wa barabarani, ya ulozi; ili ujue neno hili: Yesu ni karibu yako na anakupenda na anataka akuponye.

… Ulifanya kosa fulani na kwa sasa unapatikana katika mateso ya gereza: Yesu anapatikana hapo kwa kukuponya.
…Wewe ni mtumishi, kiongozi, uliyepata cheo kikubwa kwa njia ya madawa na ulozi, kuua na kusengenya, uongo na vibaruwa vya uongo: ulipita juu ya wengine ili ufikiye pahali ulipo, sasa maneno haya ni mkononi mwako: usifikiliye ni kwa bahati tu. Yesu anakuambia ya kwamba anakupenda hata ulipitia kwa njia hizo. Ulisoma mistari hii na unashangaa ukigundua kwamba hata ukiwa mwenye kutenda mabaya kama hayo, Yesu anakupenda pia.
Sikiliza anayosema Mwokozi wako:


“Watu wenye afia njema hawahitaji muganga, ila wenye ugonjwa tu.. Sikuja kuita wenye haki bali wenye zambi”( Marko 2.17) .
Unasikia hayo? Yesu anasema ya kwamba alikuja kwa ajili ya watu kama wewe.Unaona mlango wa kutoka mahali ulipo sasa, ni Yesu Kristo mwenyewe.


…Mara nyingine wasema: mimi si Muisraeli anayeambiwa maneno hayo ya Yesu ! Mimi ni Muafrika, Muasia,Muamerika…jua ya kwamba maneno hayo ni kwako pia na usikilize asemayo:
“Muniangalie, na muokolewe, miisho yote ya dunia;kwani mimi ni Mungu,na hapana mwengine.” ( Isaya 45:22).


Wasikia zaidi ya hayo? Ulizani kwamba ulifikia mwisho, ukitesa wanadamu wengine, unajisikia hakuna tena kukaribia Mungu. Ulisema haya na yale kuhusu zambi zako. Na Yesu anakuambia:
“Leo kama mtasikia sauti yangu, msifanye migumu mioyo yenu.”( Waebrania 4.7).


Una maneno haya mkononi mwako, jua ya kwamba ndiyo “leo” yako hii na Mungu anasema: Usifanye moyo wako kuwa mgumu.
Kwa kumaliza, Roho Mtakatifu anakupa ujumbe huu:


“Basisisi,! Tutapona namna gani, tusipochunga wokovu mkubwa namna huu?” (Waebrania 2.3).


Ndugu, rafiki, wajua sasa ya kwamba Mungu anakupenda, wajuwa kuwa Mwana wake Yesu ni tayari kukuponya. Haupatikane tena katika kutokujua. Mungu anataka kukufungua macho kwa maneno haya na anasema:


“Kwa maana Mungu alivyopenda ulimwengu, hata kutoa Mwana wake wa pekee, ili kila mtu akimwamini asipotee, bali apate uzima wa milele” (Yoane 3.16).


Chaguo ni lako: amini na uokolewe ao kutoamini na kuhukumiwa. Ndiyo, katika neema yake kubwa, Mungu anakuonyesha wazi njia ya kupitia. Anasema:


“Nimeweka mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; kwa hivi chagua uzima ili uwe hai.” (Kumbukumbu la torati 30.19).
Unapenda kumusikia Mungu? Ama kama asemavyo mtume Paulo:
“Ao unazarau utajiri wa wema wake na saburi na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu unakupeleka kwa toba? Lakini kwa ugumu wako, na kwa moyo wako usio na toba, wajiwekea akiba ya asira kwa siku ile ya asira na ufunuo wa hukumu ya haki ya Mungu” (Warumi 2.4-5), na inaandikiwa tena “Basi, zamani wakati huu wa ujinga, Mungu hakuangalia ; lakini sasa anaamuru watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki,kwa mtu yule aliyemuweka kwa kazi hii; naye amewapa watu wote hakika ya mambo haya kwa kumfufua toka wafu” (Matendo ya mitume 17.30-31).


Pamoja na mtume Paulo:
“Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kama kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu” (2 Wakorintho 5.20) kabla wakati haujapita.


Pokea upatanishi unaopewa na Mungu. Kwa hivyo unaombwa kukiri makosa yako, ukitambua ya kwamba wewe ni mwenye zambi.

Kumbuka kuwa Yesu anakupenda,

Max Shimba 

Max Shimba Ministries 2015

Tuesday, August 18, 2015

Ubatizo Wa Roho Mtakatifu






Mtu anaposoma kitabu cha Matendo ya Mitume, utendaji wa Roho Mtakatifu katika kanisa la kwanza ni dhahiri kwenye kila ukurasa. Ukiondoa kazi ya Roho Mtakatifu katika kitabu cha Matendo, huna kitu kilichobaki. Kweli, aliwatia nguvu wanafunzi wa kwanza ili “kuupindua ulimwengu” (tazama Matendo 17:6).


Siku hizi katika dunia yetu, mahali ambapo kanisa linakua kwa haraka ni pale ambapo wafuasi wa Yesu wmejitoa kwa Roho Mtakatifu kabisa na kuwezeshwa Naye. Hili lisitushangaze. Roho Mtakatifu anaweza kufanikisha mambo mengi kwa muda wa nukta kumi kuliko tunayoweza kufanikisha sisi kwa muda wa miaka elfu kumi, kwa juhudi zetu. Kwa hiyo, ni kitu muhimu sana kwamba mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi aelewe Maandiko yanafundisha nini juu ya kazi ya Roho Mtakatifu katika maisha na huduma za waamini.

Mara kwa mara katika kitabu cha Matendo ya Mitume tunapata mifano ya waamini wakibatizwa kwa Roho Mtakatifu na kuwezeshwa kufanya huduma. Tuwe na busara kujifunza somo hili ili ikiwezekana, hata sisi tupate walichopata na kufurahia msaada wa kimuujiza waliopata wao kutoka kwa Roho Mtakatifu. Ingawa kuna wanaodai kwamba matendo hayo ya miujiza ya Roho Mtakatifu ilikuwa ni kwa ajili ya wakati wa mitume wenyewe tu, mimi sipati hoja ya kiMaandiko, kihistoria wala ya kiakili, yenye kuunga mkono maoni hayo. Wale wanaoamini kinachoahidiwa katika Neno la Mungu watapata baraka zilizotajwa. Sawa na Waisraeli ambao hawakuamini, walioshindwa kuingia katika Nchi ya Ahadi, wale wasioamini ahadi za Mungu kwa leo watashindwa kuingia katika yote ambayo Mungu amewaandalia. Je, wewe uko kundi gani? Mimi niko miongoni mwa wenye kuamini!

Kazi Mbili Za Roho Mtakatifu

Kila mtu aliyemwamini Bwana Yesu Kristo kabisa amefanyiwa kazi na Roho Mtakatifu maishani mwake. Utu wake wa ndani – au roho – umezaliwa upya kwa Roho Mtakat ifu (ona Tito 3:5), na Roho Mtakatifu anaka andani yake (ona Warumi 8:9; 1Wakor. 6:19). Yeye “amezaliwa kwa Roho” (Yohana 3:5).
Kwa kutoelea hili, Wakristo wengi wa Pentekoste na Karizmatiki wamekosea kwa kuwaambia waamini fulani kwamba hawakuwa na Roho Mtakatifu kama hawakuwa wamebatizwa kwa Roho Mtakat ifu na kunena kwa lugha. Hili ni kosa kutokana na Maandiko na hata ujuzi halisi wa maisha. Waamini wengi wasiokuwa WaPentekoste au WaKarizmatiki wana ushuhuda zaidi kwamba Roho anakaa ndani yao kuliko baadhi ya waamini wa KiPentekoste au KiKarizmatiki! Wanaonyesha matunda ya Roho yaliyotajwa na Paulo katika Wagalatia 5:22-23 kwa kiwango kikubwa sana, kitu ambacho kisingewezekana bila kuwa na Roho Mtakatifu ndani.

Kwa kuwa tu mtu amezaliwa na Roho si uhakikisho kwamba amebatizwa pia kwa Roho Mtakatifu. Kulingana na Biblia, kuzaliwa na Roho Mtakatifu na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ni vitu viwili tofauti.

Tunapoanza kuchambua mada hii, hebu kwanza tutazame yale ambayo Yesu aliyasema wakati fulani kuhusu Roho Mtakatifu, kwa mwanamke asiyeokoka, huko kisimani Samaria.
Kama ungeliijua karama ya Mungu naye ni nani akuambiaye, ‘Nipe maji ninywe’, ungalimwomba yeye naye angelikupa maji yaliyo hai. … Kila anywaye maji haya [kutoka kisimani] ataona kiu tena; walakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele (Yohana 4:10, 13-14).
Ni halali kufikiri kwamba yale maji yanayokaa ndani ya mtu ambayo Yesu alizungumzia ni Roho Mtakatifu, anayekaa ndani ya wale wanaoamini. Baadaye katika Injili ya Yohana, Yesu alitumia tena maneno “maji yaliyo hai”, na hapo hakuna shaka kwamba alikuwa anazungumza juu ya Roho Mtakatifu.
Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama na kupaza sauti yake, akasema hivi: ‘Mtu akiona kiu na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.’ Na neno hilo alilisema kwa habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa (Yohana 7:37-39, TLR. Maneno mepesi kukazia).
Hapa, Yesu hakuzungumza juu ya maji yaliyo hai kuwa “chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele”. Badala yake, hayo maji yaliyo hai yanafanyika mito ibubujikayo kutoka ndani ya mwenye kupokea.

Mafungu haya mawili ya Maandiko kutoka Injili ya Yohana huonyesha vizuri sana tofauti kati ya kuzaliwa kwa Roho na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu. Kuzaliwa kwa Roho ni kwa faida ya yule aliyezaliwa upya, ili aweze kufurahia uzima wa milele. Mtu anapozaliwa tena kwa Roho, anapata hifadhi ya Roho ndani yake yenye kumpa uzima wa milele.

Lakini kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ni kwa faida ya wengine, maana inawawezesha waamini kuwahudumia watu wengine kwa nguvu za Roho. “Mito ya maji yaliyo hai” itabubujika kutoka ndani yao, ikileta baraka za Mungu kwa wengine kwa nguvu za Roho Mtakatifu.


Ubatizo Wa Roho Mtakatifu Unahitajika Kwa Nini?

Tunahitaji sana msaada wa Roho Mtakatifu ili tuweze kuwahudumia wengine! Bila msaada Wake, hatuwezi kutumaini kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi. Hiyo ndiyo sababu hasa iliyomfanya Yesu kuahidi kuwabatiza waamini kwa Roho Mtakatifu – ili dunia ipate kusikia Injili. Aliwaambia hivi wanafunzi Wake:
Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu, lakini kaeni humu mjini hata mvikwe uwezo utokao juu (Luka 24:49 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Luka tena anaandika maneno mengine ya Yesu, kwamba:
Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi (Matendo 1:7-8. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Yesu aliwaambia wanafunzi Wake hata wasiondoke Yerusalemu mpaka “wavikwe uwezo kutoka juu.” Alijua wasingekuwa na uwezo kama si hivyo, na wangeshindwa kabisa kutekeleza kazi aliyokuwa amewapa. Tunaona kwamba mara baada ya kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, Mungu alianza kuwatumia wao kwa njia ya ajabu sana kueneza Injili.

Wakristo milioni nyingi duniani, baada ya kubatizwa na Roho Mtakatifu, wamefahamu na kutambua kiwango kipya cha nguvu, hasa wakati wa kuwashuhudia watu ambao hawajaokoka. Waligundua kwamba maneno yao yalikuwa na maana zaidi, na kwamba wakati mwingine walitaja maandiko ambayo hawakujua waliyafahamu. Baadhi yao walijikuta wenyewe wakiwa wameitwa na kupewa karama kwa ajili ya huduma fulani, kama vile uinjilisti. Wengine waligundua kwamba Mungu aliwatumia kama alivyopenda katika karama mbalimbali za Roho Mtakatifu. Ujuzi wao ni wa KiBiblia kabisa. Wale wanaopinga ujuzi wao hawana msingi wowote KiBiblia kwa ajili ya kuwapinga. Ukweli ni kwamba wanapingana na Mungu.

Isitushangaze sisi ambao tumeitwa kumwiga Kristo kwamba tumeitwa kuiga ujuzi Wake na ROho Mtakatifu. Yeye alitungwa mimba tumboni mwa Mariamu kwa Roho Mtakatifu (ona Mathayo 1:20). Yeye aliyezaliwa kwa Roho alikuja kubatizwa na Roho kabla ya kuanza huduma Yake (ona Mathayo 3:16). Kama Yesu alihitaji kubatizwa na Roho Mtakatifu ili kumwezesha katika huduma, sisi je?


Ushahidi Wa Kwanza Kwamba Mtu Amebatizwa Katika Roho Mtakatifu

Mwamini anapobatizwa katika Roho Mtakatifu, ushahidi wa kwanza wa ujuzi wake ni kwamba ananena kwa lugha mpya, au kama Maandiko yanavyosema wakati mwingine, “lugha nyingine.” Kuna maandiko mengi sana yanayothibitisha jambo hilo. Hebu tuyatazame.

Kwanza – Muda mfupi tu kabla ya kupaa Kwake, yesu alisema kwamba mojawapo ya ishara zitakazofuatana na waamini ni kwamba wangesema kwa lugha mpya.
Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio: kwa jina langu watatoa pepo, watasema kwa lugha mpya (Marko 16:15-17. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Kuna waandishi wa vitabu vya mafafanuzi vya Biblia wanaodai kwamba maandiko hayo hayapaswi kuwa katika Biblia zetu kwa sababu baadhi ya magombo fulani ya zamani ya Agano Jipya hayana fungu hilo. Lakini, mengi katika magombo ya kale yana fungu hilo, na hakuna tafsiri nyingi za Kiswahili za Biblia ambazo hazina fungu hilo. Tena, yale ambayo Yesu alisema katika maandiko haya yanalingana vizuri tuna ujuzi wa kanisa la kwanza kama tunavyopata habari zake katika kitabu cha Matendo ya Mitume.

Kuna mifano mitano katika kitabu cha Matendo, yenye kuonyesha waamini wakibatizwa kwa mara ya kwanza na Roho Mtakatifu. Hebu tuitazame yote, na tutakapokuwa tunafanya hivyo, tutajiuliza maswali mawili yafuatayo: (1) Je, Ubatizo kwa Roho Mtakatifu ulikuwa ni kitu baada ya wokovu? Na (2) Je, waliopokea walinena kwa lugha mpya? Hii itatusaidia kuelewa mapenzi ya Mungu kwa ajili ya waamini siku za leo.

Yerusalemu

Mfano wa kwanza unapatikana katika Matendo sura ya 2, wakati wale wanafunzi mia na ishirini walipobatizwa kwa Roho Mtakatifu siku ya Pentekoste.
Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka (Matendo 2:1-4. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Hakuna shaka yoyote kwamba wale waamini mia na ishirini walikuwa wamekwisha okoka na kuzaliwa mara ya pili kabla ya wakati huo. Basi, walipokea ubatizo wa Roho Mtakatifu baada ya wokovu. Hata hivyo isingewezekana kwao kubatizwa katika Roho Mtakatifu kabla ya wakati huo kwa sababu Roho Mtakatifu hakuwa ametolewa kwa kanisa kabla ya siku hiyo.
Ni dhahiri basi kwamba ishara iliyoambatana na tendo hilo ilikuwa kunena kwa lugha nyingine.

Samaria

Mfano wa pili wa waamini kubatizwa kwa Roho Mtakatifu unapatikana katika Matendo sura ya 8, wakati Filipo alipokwenda jijini Samaria na kuhubiri Injili huko.
Lakini [WaSamaria] walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake. … Na mitume waliokuwako Yerusalemu waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana, ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu, kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu (Matendo 8:12-16).
Ni wazi kwamba Wakristo WaSamaria walipokea ubatizo wa Roho Mtakatifu kama kitu cha zaidi baada ya wokovu wao. Biblia inasema wazi kabisa kwamba kabla Petro na Yohana hawajafika, WaSamaria tayari walikuwa “wamelipokea neno la Mungu,” wameiamini Injili na kubatizwa katika maji. Lakini, wakati Petro na Yohana walipokuja kuwaombea, Maandiko yanasema ni ili wampokee Roho Mtakatifu.” Iwekwe wazi zaidi kuliko hapo jamani?
Je, waamini wa Samaria walinena kwa lugha mpya walipobatizwa kwa Roho Mtakatifu? Biblia haisemi, lakini inasema kwamba kitu cha kushangaza kilitokea kwao. Wakati mtu aitwaye Simoni alipoona yaliyotokea baada ya Petro na Yohana kuweka mikono yao juu ya Wakristo wa Samaria, alijaribu kununua kutoka kwao uwezo huo huo wa kumtoa Roho Mtakatifu.
Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema, ‘Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu apokee Roho Mtakatifu’ (Matendo 8:17-19).

Je, Simoni aliona nini kilichomshika hivyo? 

Tayari alikwisha ona miujiza mingi tu mingine, kama vile watu wakitolewa mapepo na waliolemaa na viwete wakiponywa (ona Matendo 8:6-7). Yeye mwenyewe alikuwa amehusika katika uchawi hapo kwanza, akiwashangaza watu wote wa Samaria (ona Matendo 8:9-10). Kama ni hivyo, alichokiona wakati Petro na Yohana walipoomba lazima kingekuwa kitu cha ajabu sana. Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika kabisa, inaonekana ni sawa kufikiri kwamba aliona kitu cha kushangaza kile kile kilichokuwa kinatokea kila mara ambapo Wakristo walipokea Roho Mtakatifu katika kitabu cha Matendo ya Mitume – aliona na kuwasikia watu wa Samaria wakinena kwa lugha nyingine.

Sauli Huko Dameski

Mara ya tatu katika kitabu cha Matendo kunapotajwa mtu akimpokea Roho Mtakatifu ni kwa habari ya Sauli wa Tarso, ambaye baadaye alijulikana kama mtume Paulo. Aliokolewa akiwa njiani kwenda Dameski, na alikuwa amepofuka kwa muda. Siku tatu baada ya kuokoka kwake, mtu aitwaye Anania alitumwa kwake na Mungu.
Anania akaenda zake, akaingia mle nyumbani, akamwekea mikono akisema, ‘Ndugu Sauli! Bwana amenituma, Yesu, yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, ukajazwe Roho Mtakatifu.’ Mara vikaanguka machoni pake vitu kama magamba, akapata kuona, akasimama, akabatizwa (Matendo 9:17, 18).
Hapana shaka kwamba Sauli aliokoka kabla ya Anania kufika kumwombea. Alimwamini Bwana Yesu alipokuwa yungali njiani kwenda Dameski, na mara moja akatii maagizo ya Bwana wake mpya. Tena, wakati Anania alipokutana na Sauli mara ya kwanza alimwita “Ndugu Sauli.” Ona kwamba Anania alimwambia Sauli kwamba amekuja ili apate kuona na kujazwa na Roho Mtakatifu. Basi kwa Sauli, kujazwa na Roho Mtakatifu – au kubatizwa basi – kulitokea siku tatu tu baada ya kuokoka kwake.
Maandiko hayasemi tukio hilo la Sauli kubatizwa na Roho Mtakatifu, lakini bila shaka lilifanyika muda mfupi tu baada ya Anania kufika mahali Sauli alipokuwa. Hakuna shaka kwamba Sauli alinena kwa lugha kwa sababu, baadaye anasema katika 1Wakor. 14:18 hivi: “Namshukuru Mungu kwamba mimi nanena kwa lugha kuliko ninyi wote” (TLR).

Kaisaria

Mara ya nne ambapo waamini wanatajwa kwamba wamebatizwa kwa Roho Mtakatifu ni katika Matendo 10. Mtume Petro alikuwa ameagizwa na Mungu kwenda kuhubiri Injili huko Kaisaria, nyumbani kwa Kornelio. Mara tu baada ya Petro kudhihirisha kwamba wokovu hupokelewa kwa imani katika Yesu, wasikilizaji wake wote waliokuwa si Wayahudi (yaani, WaMataifa) waliitikia kwa imani, na Roho Mtakatifu akawashukia.
Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote waliolisikia lile neno. Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, ‘Ni nani awezaye kuzuia maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi?’ Akaamuru wabatizwe kwa Jina lake Yesu Kristo (Matendo 10:44-48a).
Hapa, inaonekana kwamba watu wote wa nyumbani mwa Kornelio, waliokuwa wasiokuwa Wayahudi wa kwanza kumwamini Yesu, walizaliwa mara ya pili na kubatizwa hapo hapo.

Tukijifunza maandiko yanayoambatana na hayo pamoja na mantiki kihistoria, kuna sababu iliyo dhahiri kabisa iliyomfanya Mungu asingojee Petro na waamini wenzake wawawekee mikono waamini wale wasiokuwa Wayahudi, ili wapokee Roho Mtakatifu. Petro na waamini wanzake wa Kiyahudi walikuwa na shida sana kuamini kwamba wasiokuwa Wayahudi wanaweza kuokoka – achilia mbali kumpokea Roho Mtakatifu! Yawezekana wasingewaombea familia ya Kornelio wapokee ubatizo wa Roho Mtakatifu. Basi Mungu akafanya kwa enzi Yake. Mungua likuwa anamfundisha Petro na wenzake kitu kuhusu neema Yake ya ajabu kwa wasiokuwa Wayahudi.

Kilichomshawishi Petro na wale waamini wengine Wayahudi kwamba familia ya Kornelio walipokea Roho Mtakatifu kweli ni nini? Luka anaandika hivi: “Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha” (Luka 10:46). Petro akatamka kwamba wasiokuwa Wayahudi wamempokea Roho Mtakatifu kama wale mia na ishirini walivyofanya siku ya Pentekoste (ona 10:47).

Efeso

Mara ya tano ambapo waamini wanatajwa kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni katika Matendo sura ya 19. Alipokuwa anasafiri na kupitia Efeso, mtume Paulo alikutana na wanafunzi fulani, akawauliza hivi: “Je, mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini?” (Matendo 19:2, TLR).

Paulo, mtu aliyeandika sehemu kubwa ya nyaraka za Agano Jipya aliamini dhahiri kabisa kwamba inawezekana kumpokea Yesu na usiwe umempokea Roho Mtakatifu.Vinginevyo, asingeuliza swali alilouliza.
Wale ndugu wakajibu kwamba hawakuwa hata wamesikia kuhusu Roho Mtakatifu. Ni kwamba walikuwa wamesikia kuhusu Masiye anayekuja tu kupitia Yohana Mbatizaji, ambaye alikuwa amewabatiza. Paulo mara moja akawabatiza tena kwa maji, na wakati huu wakawa wamebatizwa Kikristo. Hatimaye, Paulo akawawekea mikono ili wapokee Roho Mtakatifu.
Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao, wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri. Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili (Matendo 19:5-7).
Hapa tena ni kitu wazi kwamba ubatizo wa Roho Mtakatifu ulikuwa baada ya wokovu, bila kujali kama hao watu kumi na mbili walikuwa wameokoka kabla ya kukutana na Paulo. Tena, ishara iliyoambatana na wao kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ilikuwa kunena kwa lugha (na hapa, kutabiri pia).
Sawa – Hebu tuitazame tena ile mifano mitano. Katika mifano minne, ubatizo kwa Roho Mtakatifu ulikuwa kitu kilichotokea baada ya wokovu.

Katika mifano mitatu, Maandiko yanasema wazi kabisa kwamba wahusika walinena kwa lugha nyingine. Tena, Paulo alipokutana na Anania, yeye kubatizwa kwa Roho Mtakatifu hakuelezwi, lakini tunajua kwamba hatimaye alikuja kunena kwa lugha. Huo ni mfano wa nne.

Katika mfano uliosalia, kitu kisicho cha kawaida kilitokea wakati waamini huko Samaria walipompokea Roho Mtakatifu kwa sababu, Simoni alijaribu kununua nguvu za kumtoa Roho Mtakatifu.

Basi, ushahidi uko wazi kabisa. Katika kanisa la kwanza, waamini waliozaliwa mara ya pili walipata kitu kingine na Roho Mtakatifu, na walipofanya hivyo, walinena kwa lugha nyingine. Hii isitushangaze kwa sababu Yesu alisema wale wanaomwamini watanena kwa lugha nyingine.

Tunao ushahidi thabiti kabisa kwamba kila mtu aliyezaliwa mara ya pili anatakiwa pia kupokea kazi nyingine ya Roho Mtakatifu – kubatizwa katika Roho Mtakatifu. Tena, kila mwamini anapaswa kutazamia kunena kwa lugha nyingine wakati anapobatizwa kwa Roho Mtakatifu.

Jinsi Ya Kupokea Ubatizo Wa Roho Mtakatifu

Roho Mtakatifu hupokelewa kwa imani (Wagal. 3:5), sawa tu na zawadi nyingine zote za Mungu. Ili kuwa na imani ya kupokea, mwamini anatakiwa kwanza ashawishike kwamba ni mapenzi ya Mungu kwake kubatizwa kwa Roho Mtakatifu. Kama ana mashaka au wasiwasi, hatapokea (ona Yakobo 1:6-7).
Hakuna mwamini yeyote mwenye sababu nzuri ya kuamini kwamba si mapenzi ya Mungu kwake kupokea Roho Mtakatifu, kwa sababu Yesu alieleza waziwazi mapenzi ya Mungu kuhusu swala hilo.
Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? (Luka 11:13).
Ahadi hiyo kutoka kwa Yesu inapaswa kumwaminisha kila mtoto wa Mungu kwamba ni mapenzi ya Mungu yeye apokee Roho Mtakatifu.

Mstari huo huo pia unathibitisha ukweli kwamba kubatizwa kwa Roho Mtakatifu hutokea baada ya wokovu, kwa sababu hapa Yesu aliwaahidi watoto wa Mungu (watu pekee ambao Mungu ndiye “Baba yao wa mbinguni”) kwamba angewapa Roho Mtakatifu, wakiomba. Bila shaka ni kwamba, kama ujuzi pekee na Roho Mtakatifu ambao mtu angepata ni kuzaliwa mara ya pili wakati wa wokovu tu, basi ahadi ya Yesu isingekuwa na maana. Kinyume na kikundi cha wanatheolojia wachache wa kisasa ambacho kinaelekea kutoweka, Yesu aliamini kwamba ni sawa kabisa kwa watu waliokwisha zaliwa mara ya pili kumwomba Mungu awape Roho Mtakatifu.

Kwa maneno ya Yesu, kuna masharti mawili tu ambayo lazima mtu atimize ikiwa anataka kupokea Roho Mtakatifu. Kwanza – Mungu lazima awe Baba, na ndivyo ilivyo kama umezaliwa mara ya pili. Pili – umwombe Roho Mtakatifu.

Pamoja na kwamba kumpokea Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ni kitu kinachoungwa mkono na Maandiko (ona Matendo 8:17; 19:6), si lazima. Mkristo yeyote anaweza kumpokea Roho Mtakatifu akiwa peke yake katika faragha yake ya maombi. Anachohitaji kufanya ni kuomba tu, kupokea kwa imani, na kuanza kunena kwa lugha kama Roho atakavyomwezesha kutamka.


Hofu Za Wengi

Kuna watu wenye kuogopa kwamba wakiomba Roho Mtakatifu, wanaweza kujiweka wazi kuingiwa na pepo. Hakuna msingi wowote wa hofu kama hiyo. Yesu aliahidi hivi:
Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanamwe akimwomba mkate atampa jiwe, au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akiomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba yenu wa mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? (Luka 11:11-13).
Tukiomba Roho Mtakatifu, Mungu atatupa Roho Mtakatifu. Tusiwe na hofu kwamba tutapokea kitu kingine chochote!

Kuna wengine wenye kuogopa kwamba, wakinena kwa lugha, ni kitu chao watakachokuwa wametunga badala ya lugha ya kimuujiza itolewayo na Roho Mtakatifu. Sawa – ila, kama utajaribu kutunga lugha ya hakika kabla ya kubatizwa na Roho Mtakatifu utagundua kwamba ni kitu kigumu sana, kisichowezekana. Ila, ni lazima uelewe kwamba kama utanena kwa lugha nyingine, itakubidi utumie midomo yako, ulimi, na ngano za sauti. Roho Mtakatifu hakusemei – anakupa lugha. Yeye ni msaidizi wetu, si anayetenda. Inakupasa weweuseme. Ni kama Biblia inavyofundisha, kwamba:
Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka (Matendo 2:4 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanzakunena kwa lugha (Matendo 19:6 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Baada ya mwamini kuomba zawadi ya Roho Mtakatifu, anatakiwa kuamini na kutazamia kunena kwa lugha nyingine. Kwa kuwa Roho Mtakatifu anapokelewa kwa imani, mwenye kupokea asitazamie hisia za namna fulani au msisimko kimwili. Anatakiwa kufungua kinywa chake tu na kuanza kutamka zile sauti mpya na silabi zitakazosababisha ile lugha mpya ambayo Roho Mtakatifu anampa. Mwamini asipoanza kusema kwa imani,hakuna maneno yatakayotokea kinywani mwake. Ni lazima yeye aseme, ndipo Roho Mtakatifu atakapomjalia kutamka.


Mahali Lugha Inapotoka

Kulingana na Paulo – aaminiye anapoomba kwa lugha – si akili yake iombayo bali ni roho yake.
Maana nikiomba kwa lugha,roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda. Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia, nitaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia (1Wakor. 14:14-15).
Paulo alisema kwamba alipoomba kwa lugha, akili yake haikuwa na matunda. Maana yake ni kwamba akili yake ilikuwa haihusiki, wala hakuelewa alichokuwa anaomba kwa lugha. Basi, anachosema ni kwamba, badala ya kuomba kwa lugha wakati wote na huku haelewi anachosema, alikuwa pia anaomba kwa akili, kwa lugha yake mwenyewe. Alitumia muda mwingi kuimba kwa lugha na kuimba kwa akili yake pia. Ipo nafasi kwa maombi ya aina zote hizo mbili pamoja na kuimba kwa aina zote hizo mbili, nasi tuwe na busara kufuata mfano wa Paulo.

Ona pia kwamba, kwa Paulo, kunena kwa lugha kulikuwa chini ya mamlaka ya mapenzi yake, sawa na jinsi kuzungumza lugha yake kulivyokuwa. Alisema hivi: “Nitaomba kwa roho na nitaomba kwa akili pia” (TLR). Mara nyingi wakosoaji hudai kwamba kama kunena kwa lugha siku hizi ni zawadi kweli kutoka kwa Mungu, hakuna mtu ambaye angeweza kuitawala, maana kufanya hivyo ni sawa na kumtawala Mungu. Wazo kama hilo halina msingi wowote. Kunena kwa lugha zamani na siku hizi kuko chini ya mamlaka ya mtu binafsi, na ndivyo Mungu alivyopanga. Wakosoaji hao ni vizuri waendelee na kusema kwamba watu wenye mikono ambayo imeumbwa na Mungu kweli hawana mamlaka na utawala juu ya mikono yao, na watu wenye kufanya maamuzi ya kutumia mikono yao wanamtawala Mungu.

Ukisha batizwa kwa Roho Mtakatifu, ni rahisi sana kuthibitisha kwamba kunena kwa lugha kwako kunatoka rohoni na si akilini mwako. Kwanza – Hebu jaribu kuzungumza na mtu huku unasoma kitabu hiki. Utaona kwamba huwezi kufanya yote mawili kwa wakati mmoja. Lakini, utagundua kwamba unaweza kuendelea kunena kwa lugha unapoendelea kusoma hiki kitabu. Sababu ni hii: hutumii akili yako kunena kwa lugha – tendo la kunena hutoka rohoni mwako. Basi, unapotumia roho yako kuomba, waweza pia kutumia akili yako kusoma na kuelewa.


Sasa – Kwa Kuwa Umebatizwa Kwa Roho Mtakatifu

Usisahau sababu kuu ya Mungu kukupa ubatizo wa Roho Mtakatifu – ni ili kukutia nguvu kwa ajili ya kuwa shaiidi Wake, kwa madhihirisho ya tunda na karama (au zawadi) za Roho Mtakatifu (ona 1Wakor. 12:4-11; Wagal. 5:22-23). Unapoishi maisha yanayofanana na Kristo na kujonyesha upendo Wake, furaha na amani Yake kwa dunia pamoja na kudhihirisha karama zisizo za kawaida za Roho, Mungu atakutumia kuwavuta wengine Kwake. Uwezo wa kunena kwa lugha ni sehemu moja tu ya “mito ya maji yaliyo hai” inayotakiwa kububujika kutoka ndani mwako.

Pia kumbuka kwamba Mungu alitupa Roho Mtakatifu atuwezeshe kuwafikishia Injili watu wote duniani (ona Matendo 1:8). Tunaponena kwa lugha zingine, tunapaswa pia kutambua kwamba lugha tunayosema inaweza kuwa lugha ya kabila fulani au nchi fulani ya kigeni. Kila mara tunapoomba kwa lugha, tukumbuke kwamba Mungu anataka watu wa kila lugha wasikie habari za Yesu. Tunapaswa kumwomba Bwana kuhusu jinsi anavyotaka sisi tuhusike kutimiza Agizo Kuu la Yesu Kristo.

Kunena kwa lugha ni kitu tunachopaswa kufanya mara nyingi iwezekanavyo. Paulo – mtu wa hali ya juu sana kiroho – aliandika hivi: “Ninamshukuru Mungu kwamba mimi nanena kw alugha zaidi yenu wote” (1Wakor. 14:18, TLR). Aliandika maneno hayo kwa kanisa lililokuwa linanena sana kwa lugha (japo kwa nyakati zisizofaa). Basi, Paulo bila shaka alinena kwa lugha mara nyingi sana mpaka akawazidi. Kuomba kwa lugha hutusaidia kumtambua Roho Mtakatifu anayeishi ndani yetu, na itatusaidia “kuomba bila kukoma” kama Paulo alivyofundisha katika 1Wathes. 5:17.

Vile vile Paulo alifundisha kwamba kunena kwa lugha zingine humjenga mwamini (ona 1Wakor. 14:4). Maana yake ni kwamba inatujenga kiroho. Kwa kuomba kwa lugha, tunatia nguvu utu wetu wa ndani kwa njia tusizoelewa kabisa. Kunena kwa lugha kunatakiwa kuleta utajiri mpya kila siku katika maisha ya kiroho ya kila aaminiye, wala si tukio la wakati mmoja tu tunapojazwa na Roho Mtakatifu mara ya kwanza.

Ukiisha batizwa kwa Roho Mtakatifu, ninakutia moyo utumie muda mwingi kila siku kumwomba Mungu kwa lugha yako mpya. Itakusaidia sana katika maisha yako ya kiroho na kukua kwako kiroho.


Majibu Kwa Maswali Kadhaa Ya Kawaida

Je, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba wote ambao hawajawahi kunena kwa lugha hawajabatizwa na Roho Mtakatifu? Mimi nadhani sivyo.

Sikuzote nimewatia watu moyo watazamie kunena kwa lugha wakati nilipowaombea kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, nami nadhani asilimia 95 ya hao walifanya hivyo baada ya kuwaombea kwa nukta chache. Ni maelfu ya watu kwa kipindi cha miaka mingi sana.

Lakini siwezi kusema kwamba Mkristo aliyeomba kubatizwa kwa Roho na ambaye hajanena kwa lugha hajabatizwa na Roho Mtakatifu. Hii ni kwa sababu ubatizo wa Roho hupokelewa kwa imani, na kunena kwa lugha ni kitu cha hiari. Ila, nipatapo nafasi ya kuzungumza na mwamini ambaye ameomba kubatizwa na Roho Mtakatifu lakini hajawahi kunena kwa lugha, ninachoanza nacho ni kumwonyesha mtu huyo maandiko yote katika kitabu cha Matendo kuhusu swala lenyewe. Isha, ninamwonyesha huyo mwamini jinsi ambavyo Paulo aliandika, kwamba yeye husimamia wakati wa kunena na wakati wa kutonena kwa lugha. Kama Paulo, mimi mwenyewe naweza kunena kwa lugha wakati wowote ninaotaka, na hivyo naweza kuamua, nikitaka, kutonena tena kwa lugha. Kama ni hivyo, inawezekana nikawa nimebatizwa kwa Roho Mtakatifu na kutonena kwa lugha kwa kutoshirikiana na tamko analoleta Roho Mtakatifu.

Basi – ninapokuwa na nafasi ya kuzungumza na Mkristo ambaye ameomba kwa imani apokee ubatizo wa Roho Mtakatifu lakini hajawahi kunena kwa lugha, simwambii jinsi ambavyo kunena kwa lugha si kitu Roho anachofanya bila sisi. Ninajaribu kumweleza kwamba Roho Mtakatifu ndiye ajaliaye kutamka, lakini sisi lazima tuseme – au tunene – sawa tu na jinsi ambavyo inakuwa mtu anaposema lugha ya kawaida. Kisha ninamtia moyo mtu huyo kushirikiana na Roho Mtakatifu na kuanza kunena kwa lugha. Mara nyingi baada ya hayo, watu hao hunena baadaye.


Je, Paulo Hakuandika Kwamba Si Wote Wanenao Kwa Lugha?

Swali la Paulo – “Kwani ni wote wanenao kwa lugha?” (1Wakor. 12:30) – ambalo jibu lake dhahiri ni “Hapana” lazima litazamwe kwa kuangalia Agano Jipya kwa jumla. Swali lake linapatikana katika mantiki ya mafundisho aliyotoa juu ya karama za kiroho, ambazo zinadhihirishwa kadiri Roho apendavyo tu (1Wakor. 12:11). Paulo alikuwa anaandika kuhusu karama ile ya “aina za lugha” (1Wakor. 12:10), ambayo, kulingana na Paulo, lazima kila mara iambatane na karama ya kiroho ya tafsiri za lugha. Hii karama isingeweza kuwa ile ambayo Wakorintho waliitumia mara kwa mara kanisani mwao, kwa sababu wao walikuwa wananena kwa lugha hadharani pasipo kuwepo na mtu wa kutafsiri. Tunatakiwa kujiuliza hivi: Kwa nini Roho Mtakatifu atoe karama ya lugha kwa mtu katika ibada ya hadhara, bila ya kumpa mtu mwingine karama ya kutafsiri?Jibu ni kwamba hawezi kufanya hivyo, maana akifanya, hawi anaendeleza mapenzi ya Mungu.

Bila shaka Wakorinto walikuwa wanaomba kwa lugha kwa sauti wakati wa ibada zao kanisani bila ya kuwepo na tafsiri aina yoyote. Basi, tunajifunza kwamba kunena kwa lugha kuna matumizi mawili tofauti. Moja ni kuomba katika lugha, ambako Paulo anasema kufanywe kibinafsi. Matumizi hayo hayaambatani na tafsiri, kama Paulo alivyoandika, kwamba, “Roho yangu huomba, lakini akili yangu haina matunda” (1Wakor. 14:14). Ni kwamba Paulo hakujua kila wakati alikuwa anasema nini aliponena kwa lugha. Hakuelewa, wala haikuwepo tafsiri.

Ila pia kuna matumizi ya kunena kwa lugha ambayo ni kwa ajili ya kusanyiko, na hayo huambatana na karama ya tafsiri ya lugha. Hiyo hutokea wakati Roho Mtakatifu anapomjia mtu fulani kama apendavyo, akimpa karama hiyo. Mtu huyo atanena waziwazi, kisha inakuwepo tafsiri. Ila, Mungu hamtumii kila mtu hivyo. Ndiyo sababu Paulo aliandika kwamba si wote wanenao kwa lugha. Si wote wanaotumiwana Mungu katika kile kipawa kitolewacho mara moja cha lugha, kama ambavyo Mungu hamtumii kila mtu katika karama ya tafsiri za lugha. Hiyo tu ndiyo njia rahisi ya kufafanua swali la Paulo – “Kwani ni wote wanenao kwa lugha?” – na yanayofundishwa na Maandiko kwa ujumla.
Mimi naweza kunena kwa lugha wakati wowote nitakao, kama na Paulo pia. Basi, hatuwezi kusema kwamba kila tunaponena kwa lugha, ni “kama Roho apendavyo tu.” Hapana – ni kama sisi tupendavyo. Kwa hiyo, tunachofanya kila tunapotamani si karama ya kunena kwa lugha itokeayo “kama Roho apendavyo tu.” Tena, Paulo – kama mimi – alinena kwa lugha kibinafsi pasipo kuelewa alichokuwa anasema. Basi, hiyo si karama ya lugha ambayo aliandika habari zake katika 1Wakorintho, aliyosema kwamba lazima kila mara iambatane na karama ya tafsiri ya lugha.

Ni mara chache sana nimenena kwa lugha katika kusanyiko. Ni wakati nilipojisikia kwamba Roho Mtakatifu amenishukia ili nifanye hivyo, japo ningeweza (kama Wakorintho walivyokuwa wanafanya) kuomba kwa lugha kwa sauti wakati wowote niliotaka nikiwa kanisani bila ya kuwepo tafsiri. Ninapohisi Roho Mtakatifu akinijilia kwa nguvu na karama hiyo, kila mara imekuwepo tafsiri ambayo ilileta kujengwa kwa mwili wa Kristo wakati huo.

Tunapohitimisha sehemu hii, ni vizuri kutafsiri Biblia kwa umoja. Wale wanaosema kwamba si waamini wote wanaopaswa kunena kwa lugha kwa sababu ya swali la Paulo katika 1Wakorinto 12:30, wanapuuza maandiko mengine mengi sana yasiyokubaliana na tafsiri yao. Kwa sababu ya kosa lao, wanakosa baraka kubwa sana kutoka kwa Mungu.

Ref: King James Version,
Sherperd Server
Christ Nations
Davidi Servant Ministry

By Permission 2015

Max Shimba Ministries

Monday, August 17, 2015

KAMA YESU ALIKUWA NI MUNGU, JE ALIKUWA ANAMWOMBA NANI?

Swali la Yesu ni Mungu na nani alikuwa anamwomba, huwa linaleta utatanishi mkubwa sana na kama usipo kuwa makini, unaweza kuanza kuuliza maswali katika imani yako ya Ukristo. Katika mijadala mbali mbali ya kidini, wanadhuoni wa Kiislam na hata Mashahidi wa Yehova huwa wanauliza:- Yesu alipo kuwa katika Bustani ya Gethemane, alikuwa anamwomba nani? Tena zaidi ya hapo, wanauliza, tokea lini Mungu akaomba msaada? Hakika maswali haya yanahitaji majibu thabit tena yenye aya za Biblia.

Ili umwuelewe Yesu kama Mungu duniani akiomba kwa Baba yake mbinguni , tunahitaji kutambua kwamba Mungu Baba na Yesu “Mwana” walikuwa na uhusiano wa milele kabla ya Yesu kuuchukua mwili wa mwanadamu. Zaidi ya hapo, itakupasa uelewe kuwa, Yesu alipo kuwa duniani alikuwa na asilia mbili, yaani Yesu alikuwa Mungu na wakati huo huo alikuwa Binadamu (Rejea katika Kijarida cha “Asilia mbili za Yesu Kristo”). Tafadhali soma Yohana 5:19-27, hasa mstari wa 23 ambapo Yesu anafundisha kwamba Baba alimtuma Mwana (pia tazama Yohana 15:10.

Katika Isaya 9:6 inatuambia kwamba Mwana alipeanwa na mtoto alizaliwa. Yesu alikuwa daima sehemu ya utatu, pamoja na Roho Mtakatifu. Utatu ulikuwa kila mara, kama, Mungu Baba , Mungu Mwana, na Mungu Roho, si miungu mitatu, lakini Mungu ni mmoja anajidhihirisha kama watu watatu. Yesu alifundisha kwamba Yeye na Baba yake ni kitu kimoja (Yohana 10:30), kumaanisha kwamba Yeye na Baba yake ni wa kiini kimoja na asili moja. Baba, Mwana na Roho ni watu watatu walio na ushirikiano sawa wakiwepo kama Mungu. Hawa watatu walikuwa, na wataendelea kuwa na uhusiano wa milele. Hawa watatu walikuwepo kabla ya mwanzo kuwepo na wataendelea kuwepo milele na milele yote.

Wakati Yesu, mwenye asili mbili kwa wakati mmoja, yaani Mungu na Binadamu, (Isaya 9:6) aliuchukua ule mwili wa mwanadamu usio na dhambi Yeye pia alichukua namna ya mtumwa, kupeana utukufu wake wa mbinguni (Wafilipi 2:5-11). Yesu Kama “Mwanadamu”, alikua na kujifunza utiifu (Waebrania 5:8) kwa Baba yake hasa wakati wa kujaribiwa na Shetani, alishitakiwa uongo na wanadamu, kukataliwa na watu wake, na hatimaye alisulubiwa. Kuomba kwa Baba yake mbinguni kulikuwa kwa kumwomba nguvu (Yohana 11:41-42) na hekima (Marko 1:35, 6:46), HAYO YOTE ALIFANYA KAMA MWANADAMU. 

Kuomba kwake kulionyesha utegemezi wake kwa Baba yake katika ubinadamu wake ili atekeleze mpango wa ukombozi wa Baba yake, kama ilivyoshuhudiwa katika Yohana 17. Kuomba kwake kulionyesha kwamba Yeye hatimaye alijisalimisha kwa mapenzi ya Baba yake, ambayo ilikuwa ni pomoja na kwenda msalabani kulipa adhabu (kifo) kwa kuvunja kwetu sheria Mungu (Mathayo 26:31-46). Bila shaka, Alifufuka katika mwili kutoka kaburini, akishinda msamaha na uzima wa milele kwa wale ambao watatubu dhambi zao na kumwamini kama Mwokozi.

Hivyo basi, hakuna tatizo kwa Mungu Mwana kuomba au kuzungumza na Mungu Baba. Kama ilivyotajwa, walikuwa na uhusiano wa milele kabla ya Kristo awe mwadamu. Uhusiano huu ni taswira katika Injili ili tuweze kuona ni jinsi gani Mwana wa Mungu katika ubinadamu wake ulitekeleza mapenzi ya Baba yake, na katika kufanya hivyo, kulinunua ukombozi kwa ajili ya watoto wake (Yohana 6:38). Kwa kuendelea kujiwasilisha kwa Baba yake mbinguni Kristo daima aliwezeshwa na kutiwa nguvu na akabaki kuwa na lengo katika maisha yake ya maombi. Mfano wa Kristo wa maombi ni wetu kuufuata.

Yesu Kristo hakuwa chini ya Mungu duniani wakati anaomba kwa Baba yake mbinguni, kumbuka kuwa, Yesu alikuwa na asilia Mbili, -Mungu na Binadamu. Alikuwa anaonyesha jinsi hata katika ubinadamu wa dhambi ni muhimu na maisha ya maombi ili kufanya mapenzi ya Baba yake. Kuomba kwa Yesu kwa Babaye kulionyesha mfano wa uhusiano ulioko katika Utatu wake na mfano kwetu sisi, kwamba ni lazima tumtegemee Mungu kwa nguvu na hekima tunahitaji kwa njia ya maombi. Tangu Kristo, kama Mungu -mwanadamu, alihitaji kuwa na maisha mahiri ya maombi, hivyo ndivyo inavyowapasa wafuasi wa Kristo hii leo.

Hivyo basi, Yesu kuomba kwa Baba yake, alifanya hivyo kama Binadamu (Yohana 17), ingawa wakati huohuo, yeye alikuwa ni Mungu (Rejea katika Kijarida cha “Asilia Mbili za Yesu Kristo”). Huu ni uthibitisho tosha kuwa, tokea Dunia hii iumbwe, hakujawai tokea mtu kama Yesu Kristo. Yesu Anaombwa/prayed (Matendo ya Mitume 7:59), wakati huo huo tunasoma kuwa Yesu Anamwomba Mungu Baba (Yohona 17)

Hakika Yesu Ni Mungu.

Kwa Maswali zaidi wasiliana nasi katika maxshimbaministries@gmail.com

Imeletwa kwenu na Max Shimba

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW