Friday, December 12, 2014

Mwanadamu ni Nini Hasa?



Wewe hujawahi kujiona hata siku moja! Biblia inasema kwamba sisi tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. Mungu alipopanga kumwumba mwanadamu alisema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu. (Mwa. 1:26).


Biblia pia inasema: BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi(Mwa. 2:7). Na tena: Mungu ni Roho. (John 4:24).

Maandiko haya mawili yanatuonyesha mambo kadhaa kuhusu mwanadamu:
  • Mwanadamu ana sura ya Mungu (yaani anafanana na Mungu).
  • Mwanadamu ni udongo.
  • Mungu ni Roho; si udongo.
  • Pale ninapojitazama, kile ninachoona ni udongo (mwili).
  • Kwa vile Mungu si udongo, basi yule mtu ambaye Mungu alisema ni mfano wake si hiki ninachokiona, yaani udongo.
Mimi halisi lazima nitakuwa roho pia kama alivyo Mungu; si mwili. Kimsingi, baada ya Mungu kuumba, hata maandiko yanasema: akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai. (Mwa. 2:7b).

Mimi halisi (ile roho ambayo ndiyo sura ya Mungu) ninaishi ndani ya huu udongo ninaouona.

Kwa vile mimi ni roho, kibiblia mwili wangu unaitwa nyumba ya maskani yetu iliyo ya dunia. (2 Kor. 5:1).

Nitakapotoka nje ya mwili huu ndipo nitakapokuwa katika ngazi ileile sawa na Mungu, malaika na hata mapepo, yaani nitakuwa ni roho kama wao walivyo roho. Hapo ndipo nitakuwa mimi halisi.

Nitakapokuwa nje ya mwili huu, bado nitakuwa ni mtu kamili kabisa, tofauti na watu wengine kama sasa. Hebu tuone anachosema mtume Paulo juu ya kuwa nje ya mwili: Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua. (2 Kor. 12:2).

Ukisoma aya zilizo kabla na baada ya aya hii, utagundua kuwa Paulo anajiongelea yeye mwenyewe. Sote tunafahamu kuwa mtu hawezi kwenda mbinguni na mwili huu wa udongo. Mungu anasema wazi kwamba: kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi. (Mwa. 3:19).

Ni roho, yaani yule mtu wa ndani; yule mtu halisi ambaye ndiye ana uwezo wa kuingia kwenye ulimwengu wa roho. Kwa hiyo, haikuwa ni Paulo-udongo aliyeenda mbinguni bali ni Paulo-roho. Ukiwa nje ya mwili, bado unakuwa na ufahamu wako wote. Paulo anatuambia: akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene. (2 Kor. 12:4). Aliweza kusikia na kuelewa mambo yaliyosemwa kule mbinguni; lakini wakati huo mwili na masikio yake ya udongo yalikuwa hapa duniani.

Sasa basi, ile roho, ambayo ndiyo mimi halisi ndiyo:
Inayoupa mwili wangu uhai. Ukiondoa mwili wangu kutoka kwangu, bado nitaendelea kuwa hai kabisa; lakini ukiondoa roho yangu kutoka kwenye mwili, mwili unakufa mara moja! Mungu anasema: … mwili pasipo roho umekufa, ... (Yak. 2:26).
  • Mimi-roho ni halisi zaidi kuliko mimi-udongo.
  • Roho itakuwa hai milele.
  • Roho ndiyo sehemu yangu ya muhimu ninayotakiwa kuitilia maanani zaidi. 
  • Roho ndiyo ambayo shetani anatumia juhudi zake zote kuiharibu na kuitenga na Mungu milele.

Kile anachofanya shetani
Kwa kuwa shetani na malaika zake walishahukumiwa milele na hawana tena tumaini la wokovu, wanajibidisha usiku na mchana kutekeleza jambo moja tu – kutumia kila njia kumharibu mwanadamu! Mungu anatueleza wazi: Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. (Yohana 10:10).

Ili kutekeleza lengo hili, shetani anafanya kile awezalo kutufanya tusielekeze macho yetu kwenye roho (mimi halisi); badala yake nielekeze macho yangu kwenye mimi-udongo. Matokeo yake, tunatumia muda mwingi sana tukijaribu kutimiza tamaa mbalimbali za mwili, ilhali mwili hauwezi kamwe kuridhishwa na kitu chochote – huku ndiko kutia maji kwenye gunia hasa! Kamwe haliwezi kujaa! Imeandikwa: Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho hushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. (Gal. 5:17). Matokeo ya haya ni kuwa: Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu. (Gal. 6:8).

Ili kutekeleza kusudi hilo, majeshi yaliyo kwenye ufalme wa giza yanahakikisha kuwa tunahangaishwa kila uchao na mambo kama vile ulevi, uzinzi, kusaka fedha, kusaka umaarufu, ulipizaji kisasi, muziki wa kidunia, dawa za kulevya, uchawi, ... nk, nk. 

Tunapofungwa na mambo haya, tunakuwa vipofu na viziwi kabisa! Hatuwezi tena kusikia, kuona au kukubali wazo kwamba yapo maisha mengine bora zaidi ya yale tunayoendesha. Huu ndio ukweli halisi! Tunakuwa tunadhani hapo ndipo tumefika.

Kisha pale maisha ya mtu yanapofika mwisho, mara tu anapokufa, palepale anatambua jinsi ambavyo alikuwa akiishi kwenye uongo na udanganyifu siku zote. Na hapo ndipo anapotambua kuwa siku zote hakuwa anajifahamu yeye ni nani hasa. Anagundua kuwa kumbe alikuwa anahangaikia mwili usio na maana, huku akiwa ametelekeza sehemu ya muhimu kabisa, yaani yeye halisi (roho). Na hapo anakuwa ameshachelewa kabisa!

Unakuwa kama ilivyokuwa kwa tajiri katika Biblia; akili zake zilikuwa timamu kabisa na tena anaonyesha ufahamu na hekima kubwa; isipokuwa ni mahali ambapo hekima na ufahamu huo haukumsaida tena. Alitakiwa kuutumia angali duniani, kama ilivyo kwa sisi leo. Huyu tajiri alimwambia Ibrahimu: nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu. (Lk. 16:24).

Tunaporuhusu mambo yafike hapa, Mungu anasema: Ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; watanitafuta kwa bidii, wasinione. Kwa kuwa walichukia maarifa, wala hawakuchagua kumcha BWANA. Hawakukubali mashauri yangu, wakayadharau maonyo yangu yote. Kwa hiyo watakula matunda ya njia yao, watashiba mashauri yao wenyewe. Maana kurudi nyuma kwao wajinga kutawaua, na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza. Bali kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya. (Prov. 1:28-33).

Wakati mtu anapokuwa duniani, anadhani kuwa haiwezekani kuishi bila kutumia dawa za kulevya, pombe, uzinzi, uongo, hasira, nk. Lakini akishatumbukia upotevuni, anatamani apate japo hata tone moja la maji – ingawaje sasa hata hilo halipati! Hebu tafakari juu ya hilo! Kumbuka, kiu hii haitakuwa ya siku moja au mbili. Itakuwa ndio maisha yako milele na milele!!

Je, ni vibaya kuwa na maisha mazuri?
Sisemi hata kidogo kwamba kuwa tajiri ni dhambi. Kimsingi, hata Biblia inasema: Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake. (2 Kor. 8:9).

Tena Mungu anasema: Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la. (Mal. 3:10). Mungu anapenda kabisa tuwe matajiri, tena matajiri wakubwa!

Suala la msingi ni kuwa, je, umemkaribisha Bwana Yesu moyoni mwako na kumpa nafasi ya kwanza katika kila jambo ikiwa ni pamoja na mambo yako ya kusaka maisha? Utajiri na heshima vinatakiwa vitoke kwake. Tukitanguliza dunia na mwili mbele, bado tutakuwa matajiri kulingana na juhudi tulizo nazo, lakini mara tutakapotoka kwenye maisha haya ndipo tutakapojiona jinsi ambavyo tu maskini wa kutupwa. 

Bwana Yesu anasema: Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi. Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona. (Ufu. 3:17-18).

Sasa je, unaishi kulingana na sheria ya Mungu au unaishi kulingana na sheria ya mwili na dunia? Umeelekeza macho yako kwenye wewe-roho unayedumu milele au kwenye wewe-udongo uliye wa kitambo tu? 

Jukumu letu
Bwana Yesu anasema: Linda sana moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima. (Mithali 4:23).

Tukifuata tu mambo ya dunia kwa sababu tu yamepewa umaarufu na vyombo vya habari; au kwa kuwa tu eti watu fulani maarufu wanaonekana kuyafuata; kama mambo hayo yako kinyume na Neno la Mungu, hayo si lolote si chochote bali ni hila na uongo kutoka kuzimu ambao umepangwa kwa ustadi mkubwa ili kukunasa na kukuua milele!

Ibilisi yuko kazini ndugu. Yeye hana mchezo na malengo yake. Lakini wewe unachezacheza tu na maisha wala hukai uwaze unakoelekea. Maandiko yanasema: Wenye kiburi wamenifichia mtego na kamba; wametandika wavu kando ya njia; wameniwekea matanzi. (Zab. 140:5). Pia imeandikwa: Miiba na mitego huwa katika njia ya mshupavu; yeye aitunzaye nafsi yake atakuwa mbali nayo. (Mith. 21:5).

Rafiki, haya mambo ni halisi kabisa. Hakuna mwindaji atakayetega mtego waziwazi. Ni lazima ataufunika ili yule aliyetegwa asiutambue. Yale mambo ambayo wewe unadhani ni kula raha, yamewekewa hiyo hali ya raha ili wewe usishituke - iwe ni pombe, disko, kukesha kusaka utajiri, nk. Huo ni mtego kabisa wa adui. Huwezi kupona nje ya Kristo. Huwezi kamwe!

Rudi tena utwae usukani wa maisha yako kutoka mikononi mwa dereva muuaji, kisha uanze kutawala hayo maisha aliyokupa Mungu ambayo ni ya thamani kuliko unavyoweza kufikiri. Bwana Yesu yuko tayari kabisa kukuongoza kwa usalama hadi ufike nyumbani, mbinguni.

Tafadhali, tafadhali, tafakari juu ya mambo haya. Japokuwa yanaonekana ni ya kipuuzi kwa wengi, lakini jambo moja ni dhahiri – kila mmoja atakufa siku moja! Nini kitafuata kwako baada ya hapo?

Wewe halisi (yule mtu wa ndani) haishi kwa kula wali na ugali. Anaishi kwa kula Neno la Mungu lililoandikwa kwenye Biblia. Bwana wetu Yesu anasema: Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu. (Mt. 4:4).

Mambo ya rohoni ni halisi kabisa lakini yako kwa namna ambayo ni vigumu sana kuyaelewa kwa akili za kibinadamu. Ndiyo maana imeandikwa: Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. (1 Kor. 2:14).

Ndugu, kama unangoja akili zako zielewe ndipo uamini, hautaamini kamwe. Kwa maana nyingine, hapo tayari adui ameshakushika na kukutoa nje ya mstari.

Ni lazima tufahamu kwamba, japokuwa Mungu ana nguvu zote, kamwe hatamlazimisha mtu yeyote kumwamini. Badala yake yeye anaomba ruhusa ya kuingia moyoni mwako. Hakika Mungu wetu ni wa ajabu! Anasema: Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami. (Ufunuo 3:16). Ni pale tu tunaponyenyekea na kusema, “Karibu moyoni mwangu Bwana Yesu” ndipo mambo yanaanza kueleweka.

Usitafute sababu zinazoonyesha kwamba haiwezekani. Ukifanya hivyo, utazipata maana ziko nyingi sana. Badala yake, mwamini Bwana Yesu; mkaribishe moyoni mwako leo; amini ahadi zake maana yeye ndiye njia, kweli na uzima!

By permission: Injil ya Kweli

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW