Thursday, May 1, 2014

ROHO MTAKATIFU NA KAZI ZAKE KWETU


SOMO LA 1

ROHO MTAKATIFU,MTOA UTAKATIFU
Katika somo la kwanza katika mfululizo wa masomo haya yanayohusu Roho Mtakatifu,Tulijifunza kwamba Roho Mtakatifu,ni mtakatifu,hivyo anakuwepo na kudumu mahali palipo na utakatifu tu.Tukiwana maisha ya uchafu,yaani dhambi;humfanya Roho Mtakatifu akose makao kwetu,na hivyo hawezi kuwepo kwetu.Kama alikuwepo mwanzo kwetu,huondoka (1Samweli 16:14;
Zaburi 51:4,10-11).Sasa swali linakuja,tunawezaje kuwa watakatifu katika maisha yetu ili Roho Mtakatifu afanye makao
kwetu?Jibu ni kwamba,Roho Mtakatifu ,ndiye huyohuyo anayetoa utakatifu tunaouhitaji.Sasa tunamwangalia Roho
Mtakatifu kama Mtoa Utakatifu,kwa kutafakari kazi yake hiyo katika vipengere vitano:-
1. ROHO MTAKATIFU,ROHO ATUPAYE KUZALIWA MARA YA PILI
2. ROHO MTAKATIFU ROHO AWAFUFUAYE WATU WALIOKUFA KIROHO
3. ROHO MTAKATIFU, ROHO AWATIAYE UZIMA WATU WALIOZIMIA KIROHO
4. ROHO MTAKATIFU ROHO ATUPAYE UTAKASO
5. ROHO MTAKATIFU, ROHO ATUPAYE TUNDA LA ROHO

1. ROHO MTAKATIFU,ROHO ATUPAYE KUZALIWA MARA YA PILI
Hatupaswi kamwe kudanganyika kwamba utakatifu siyo duniani ni mbinguni,Maandiko yanaeleza waziwazi kwamba watakatifu walioko duniani ndiyo anaopendezwa nao Mungu(Zaburi 16:3). Hatupaswi pia kudanganyika kwamba tunaweza kufanya dhambi hapa duniani,halafu tukasalimika baada ya kufa,kutokana na misa ya wafu n.k(1Wakorintho 6:9-10;Waefeso 5:5-7;Wagalatia 6:7 ;Waebrania 9:27;IYohana 5:16;Kumbukumbu 10:17) la maana hapa ni kufahamu ni jinsi gani tunavyoweza kuwa na ushindi dhidi ya dhambi hapa duniani,na kuokoka kutupwa motoni,maana bila shaka tunatakiwa kuokoka tukiwa hapahapa duniani (Luka 19:8-10);Tito 3:3-4)Tunawezaje kuwa na ushindi dhidi ya dhambi?Ni kwa kuzaliwa mara ya pili,kwa Roho Mtakatifu(Yohana 3:3-10;Tito 3:3-5)Yesu Kristo,alijaribiwa sawasawa na sisi lakini hakutenda dhambi(Waebrania 4:14-15)Ni nini siri ya ushindi wake huo?Ni kwa sababu alizaliwa kwa Roho Mtakatifu,yaani alizaliwa tofauti na kawaida ya kimwili ya mume na mke.Sisi nasi tunapotubu dhambi
zetu kwa kumaanisha kuziacha,tunapata rehema hii kwa imani tu(Mithali 28:13)Tunazaliwa mara ya pili katika ulimwengu wa roho,na hivyo kuwa na uwezo wa kushinda dhambi kwa muujiza mkubwa.Katika hali ya kawaida ya jinsi tulivyozaliwa kimwili,kamwe hatuwezi kushinda dhambi.Ni mpaka tufanyike viumbe vipya kwa Roho Mtakatifu.Mwambie Roho Mtakatifu kwamba unataka kuzaliwa mara ya pili,naye atafanya.

2. ROHO MTAKATIFU ROHO AWAFUFUAYE WATU WALIOKUFA KIROHO
Kurudi nyuma na kuacha wokovu kunaitwa pia kufa kiroho(Ufunuo 3:1;Waefeso 2:1).Kwa kila aliyerudi nyuma na kuacha wokovu,hii ni saa ya kuamka usingizini na kuanza upya(Warumi 13:11-12).Lakini,je,inawezekana kuanza upya tena katika hali hii?Ndiyo,kwa msaada wa Roho Mtakatifu.Hii ni kazi yake nyingine .Roho Mtakatifu ndiye aliyemfufua Yesu,alipokufa(Warumi 13:11). Kwa jinsi hiyo hiyo,Roho Mtakatifu anaweza kutufufua kiroho
na kutupa uhai tena wa kiroho(Waefeso 2:1,4-6).Mwambie Roho Mtakatifu kwamba unataka kufufuliwa kiroho, naye atafanya.

3. ROHO MTAKATIFU, ROHO AWATIAYE UZIMA WATU
Kabla ya kufa kiroho,hutangulia kuzimia kiroho.Shetani hutupeleka hatua kwa hatua,kama upepo katika tairi unavyotolewa kidogo kidogo kutokana na pancha ndogo.Tukizimia kiroho,upendo wa kwanza unatoweka. Ingawa bado hatujafikia hali ya kufanya dhambi za uzinzi,uasherati,ulevi n.k kama mataifa,hata hivyo,mambo ya rohoni yanakuwa hayana mvuto kwetu kama mwanzo.Kuomba,kushuhudia,kuhudhuria ibada n.k,yanakuwa
mzigo kwetu.Tunaanza kuvutwa zaidi na mambo ya dunia.Katika hali hii tunahitaji nguvu mpya,uzima mpya (Isaya 40:28-31). Anayefanya kazi hii pia ni Roho Mtakatifu,Roho wa uzima (Warumi 8:2). Pepo wa udhaifu wanatolewa kwa Roho wa Mungu (Mathayo12:28), na vivyo hivyo udhaifu wetu kiroho unatolewa na Roho wa Mungu.Je umezimia kiroho,Mwambie Roho Mtakatifu akuzindue,naye atafanya.

4. ROHO MTAKATIFU ROHO ATUPAYE UTAKASO
Baada ya kuokolewa,tunahitaji pia kutakaswa.Bila utakaso,tutajikuta bado hatuna ushindi dhidi ya dhambi za ndani katika mawazo,na moyoni,ingawa tayari tuna ushindi dhidi ya dhambi za kutenda. Dhambi za ndani ,ni kama hasira, wivu ,chuki, masengenyo, kugombania ukubwa,kiburi,majivuno,kutokusamehe,kinyongo,
kupenda udunia n.k.Hivi vinaweza vikaonekana kwa watu waliookoka ambao hawajatakaswa: Mawazo yasiyo ya ki Mungu (Mathayo 16:21-23),kugombania ukubwa (Luka 22:24-26;Mathayo 20:20-22,25-28; Marko 9:30-37),hasira (Mathayo 20:24) wivu, fitina, ugomvi (Marko 9:38-39;Luka 9:49-50; 1Wakorintho 3:3-5), faraka na matengano(1Wakorintho1:10-13),umimi(Mathayo 28:6-13), kutokusamehe (Mathayo 18:21-35), chuki,kushindwa kuvumilia maudhi,kushtakiana wapendwa mahakamani (Luka 9:51-56; 1Wakorintho 6:1-8); Warumi 7:15 n.k .Mambo haya huondolewa kwa utakaso.



Ndiyo maana Yesu aliwaombea Utakaso wanafunzi wake waliokuwa tayari wameokoka(Yohana 17:14-19) Roho Mtakatifu ndiye atupaye Utakaso(1Wakorintho 6:11;1Petro1:2)Je,hujatakaswa,mwambie
Roho Mtakatifu akutakase,yeye ni waminifu,atafanya(1Thesalonike5:23-24)

5. ROHO MTAKATIFU, ROHO ATUPAYE TUNDA LA ROHO
Katika Wagalatia 5:22-23,tunajifunza juu ya tunda la Roho.Katika lugha ya asili,yote katika mistari hii yanamaanisha kwamba Tunda la Roho ni moja tu,Upendo.Hata hivyo,upendo huo unadhihirishwa kwetu katika tabia na matendo kama furaha,amani,uvumilivu,utu wema,fadhili,imani,upole,na kiasi.Ni pale tu tunapokuwa na maisha yaliyojaa upendo,ndipo tunapokuwa tunatimiza mapenzi ya Mungu katika maisha yetu.

Pasipo upendo,tunakuwa shaba iliayo na upatu uvumao,tunakuwa si kitu.Lolote jingine tunalolifanya linakuwa halina faida (1Wakorintho 13:3). Hatuwi wanafunzi wa Yesu (Yohana 15:8)Sasa basi ,ni muhimu kufahamu kwamba upendo ni tunda la Roho, tunalolipokea kutoka kwa Roho Mtakatifu.Tukilipokea tunda hili,na kukua kila siku katika upendo (1Wathesalonike 3:12), Kama matunda yanavyokua,ndipo tunapokuwa wanafunzi wa Yesu kwelikweli.Tukiwa na tunda la Roho la upendo,tunakuwa na Furaha ya wokovu ambayo haiwezi kuondoka kwetu kwa sababu ya majaribu yoyote au kukosekana kwa lolote la kimwili(Yakobo1:2). Tutakuwa na amani ipitayo fahamu zote (Wafilipi 4:7) inayotuwezesha kuwa na amani na watu ambao tusingeweza kuwa na amani nao.Tutakuwa na lengo la kutafuta amani na watu wote wakati wote(Waebrania 12:14)Tutakuwa na uvumilivu wa kipekee katika mateso,makwazo kutoka kwa watu n.k Tutakuwa na utu wema kwa watu wengine hata wale ambao hawajaokoka
(Marko 10:17). Tutakuwa na fadhili yaani hali ya kutaka wakati wote watu wanaotuzunguka wawe na furaha.
Tutakuwa watu tuliojaa imani,tusiotetereka kirahisi.Tutakuwana upole yaani unyenyekevu (Mathayo 11:29; Wafilipi2:5-8)Na pili tutakuwa na kiasi (self-control)yaani uwezo wa kukataa kufanya lile ambalo Yesu hataki, kwa gharama yoyote.Je,unataka kuwa na tunda la Roho katika maisha yako?Mwambie Roho Mtakatifu,naye atafanya.

SOMO LA 3:ROHO MTAKATIFU, ROHO ATUSAIDIAYE KUOMBA

Kila Mkristo,au mtu aliyeokoka,hana budi kuwa na lengo la kufikia kimo na cheo cha utimilifu wa Kristo katika tabia na Utumishi wa
Mungu(Waefeso 4:11-15)Kufikia kiwango cha Yesu Kristo katika tabia ni jambo linalowezekana,Kama siyo,tusingetakiwa
kuwa wakamilifu na watakatifu kama Baba wa mbinguni alivyo Mtakatifu(Mathayo 5:48;1`Petro 1:15-16)Neno la Mungu pia,
linatufundisha uwezekano wa kuwa na viwango vya utumishi vya yesu alipokuwa duniani,na hata kuzidi(Yohana 14:12). Hata
hivyo haya yote hayawezekani kama sisi siyo waombaji kama Yesu alikuwa mwombaji namba moja.Alifanya maombi alfajiri na mapema (Marko 1:35).Alijitenga na shughuli mchana na kufanya maombi (Luka 5:15-16)Aliomba jioni (Mathayo 14:23)Wakati mwingine alifanya maombi usiku kucha(Luka 6:12)Je,sisi tunaweza kuwa waombaji kiasi hiki?Kwa nguvu na jitihada zetu hatuwezi.
Tunaweza tu,tukisaidiwa na Roho Mtakatifu.Ndiyo maana tunajifunza somo hili muhimu leo katika mfululizo wa masomo haya
ya Roho Mtakatifu ,na kichwa cha somo la sasa ni ”

ROHO MTAKATIFU, ATUSAIDIAYE KUOMBA”, NA TUTAJIFUNZA SOMO HILI KATIKA VIPENGERE VINNE:-

6. UMUHIMU WA MAOMBI KATIKA MAISHA YA KIROHO
7. KUSHUKA KWA MUNGU BAADA YA MAOMBI YA KUUGUA NA KULIA
8. MAFUNDISHO TUNAYOYAPATA KUTOKANA NA MAOMBI YA YESU
9. ROHO MTAKATIFU,MSAIDIZI ATUSAIDIAYE KUOMBA
2. UMUHIMU WA MAOMBI KATIKA MAISHA YA KIROHO
Shetani ndiye adui yetu mkuu.Kazi yake ni kuiba chochote kizuri cha kiroho tulicho nacho,na tena kuchinja au kuua na kuharibu yote
mema kwetu kiroho na kimwili.Tukiwa peke yetu,kamwe hatuwezi kupambana na shetani na kumshinda.Hatuna budi kuwa na
Mungu katika maisha yetu ili tumshinde ibilisi.Daudi alimshinda Goliathi kwa Jina la Bwana.Hakumshinda kwa nguvu zake.Kwa maana nyingine hatuwezi kuzaa matunda yoyote mema ya kiroho kama hatuko ndani ya Yesu.Usalama wetu na ushindi wetu wa kiroho,unategemeana sana na sisis kukaa ndani yake Yesu,yaani sisi kuwa na uhusiano au ushirika na Kristo.Pasipo yeye,sisi hatuwezi kufanya neno lolote .(Yohana 15:4-5). Kukaa ndani ya Yesu, kunafananishwa na tawi lililounganishwa na shina. Kuunganishwa huko ndiyo uhai wa tawi.

Tawi likijitenga na shina,linanyauka na kufa. Sasa basi, tunaunganisha na Mungu na Mungu tunapokuwa tunawasiliana naye katika maombi.Tukiwa hatuna maisha ya maombi,kimsingi ni kwamba tunakuwa ni tawi lililojenga na shina,na hivyo tunanyauka na hatimaye

kufa kiroho. Hatuwezi kuwa na kitu tusipoomba(Yakobo 4:2)
Tutaingia majaribuni tusipoomba (Mathayo 26:41).Tutapepetwa kama ngano na ibilisi na mazuri yote ya kiroho yataondoshwa,na
imani yetu itatoweka(Luka 22:31-32).Shetani atatumeza na kuturudisha katika ufalme wake(1Petro 5:8).Hatuwezi kuwaleta watu kwa Yesu,tusipokuwa waombaji, maana Shetani hatawaachia(Zaburi 2:8).Hatuwezi kuona watu wakifunguliwa katika vifungo vya shetani vya kimwili (Luka 13:16) na vile vinavyotokana na mambo ya rohoni (Matendo 12:5-17).Kwa ufupi tutachukuliwa na mafuriko ya Shetani(Zaburi 32:6).

3. KUSHUKA KWA MUNGU BAADA YA MAOMBI YA KUUGUA NA KULIA
Maandiko yanatufahamisha kwamba makao ya Mungu mbinguni,ni Mahali palipoinuka,na Mlimani kwenye kiti cha enzi cha Mungu (Isaya 57:15;Kutoka 24:12-13;Ufunuo 7:9-10). Ingawa Mungu wetu yuko mlimani,maandiko yanasema tukimwomba, yeye husikia huko mbinguni na kutujibu maombi yetu kwa kuyatenda tunayoyataka (1Wafalme 8:32;Zaburi 76:8;102:19).Hata hivyo,hatuna budi kufahamu pia kwamba katika mazingira Fulani Mungu hushuka kutoka mlimani na kuja duniani katika hali isiyo ya kawaida.Mungu anaposhuka kwa jinsi hii,hutenda mambo ya kutisha,na ya kushangaza, yasiyo ya kawaida na hivyo kuwavuta wengi mno kwake(Waamuzi 4:12-16,5:13;Isaya 31:4; Hesabu 11:23-25,31-32).Uamsho hutokea Mungu anaposhuka,na watu wagumu wa mioyo huvutwa kwa Yesu,walio vuguvugu huwa moto,mambo mengine makubwa ya kuitikisa jamii kama mamia ya wenye ukimwi kupona kwa mpigo,hutokea,Mungu akishuka.

Hata hivyo kushuka kwa Mungu hutokea baada ya maombi ya kuugua na kulia kwa uchungu mkubwa(Kutoka 2:23-24;3:7-8;
Matendo 7:32-34).Wakati wote Yesu Kristo alimfanya Mungu kushuka katika huduma yake kwa kuwa aliomba kwa kulia sana
na machozi(Waebrania 5:7),na wengine walimuombolezea kwa kilio na uchungu mkubwa(Luka 23:27)Kulia kwa kuugua katika
maombi hushusha majibu ya maombi namna ya kipekee(2Nyakati 34:27;Zaburi 34:17;39:12;51:1-2,17;72:12;12;88:1-2; Isaya 58:9; Yeremia 31:9; Luka 18:7). Sasa basi ni rahisi kuomba maombi kwa kulia na kuugua?jibu ni la,bila msaada wa Roho Mtakatifu, itakuwa kama tunaigiza tu.

4. MAFUNDISHO TUNAYOYAPATA KUTOKANA NA MAOMBI YA YESU
Tunajifunza mambo mengi zaidi kuhusiana na maombi kwa kuyaangalia maisha ya maombi ya Yesu, na mafundisho yake kuhusu maombi:-

§ Yesu Kristo alikuwa na wakati wa kuomba pamoja na wanafunzi wake(Luka 9:18),Lakini pia alikuwa na muda mrefu wa maombi ya peke yake (Luka 5:16;Marko 6:45-46).Ni muhimu kujiunga na kikosi cha maombi cha Kanisa na kushiriki maombi ya pamoja na wengine,lakini ni lazima kila mmoja kuwa na muda wa kuomba mwenyewe.

§ Yesu hakukubali kuchukuliwa na huduma za kushauri watu,kuwaombea watu n.k na kuziruhusu zimkoseshe kuomba.
Alijua bila maombi,huduma hizo zitakuwa hazina nguvu.Aliziacha huduma,akafanya maombi(Luka 5:15-16).Kabla ya kuzungumza na watu,alizungumza na Mungu KWANZA.Alifanya maombi ya alfajiri na mapema sana na baadaye alipokutana na watu ilikuwa rahisi mno kwake kuponya ukoma na kutoa pepo.(Marko 1:35-42).

§ Kabla ya Yesu kutembea juu ya maji,na kukomesha upepo, alikuwa na kipindi kirefu cha maombi(Marko 6:46-51).Vipindi virefu vya maombi vinaweza kutupa uwezo wa kuona yasiyowezekana yakiwezekana!

§ Utukufu wa Yesu ulitokana na maombi!(Luka 9:28-29)Hatuna utukufu wa Mungu kwa kuwa siyo waombaji!Mwombaji, utukufu wake humwogopesha shetani

§ Alipokuwa na huzuni aliomba hakunung’unika tu na kulalamika, na ghafla alipata ujasiri wa kukabili lolote lile (Mathayo 26:36-39;47-49). Hatuna ujasiri na tumejaa woga kwa kuwa hatuombi
§ Maombi yake yalikuwa ni vita hasa.Alipokuwa akiomba,alitoka jasho(hari)kama matone ya damu(Luka 22:44). Maombi ni mapambano dhidi ya shetani anayezuia majibu yetu(Danieli 10:12-13).Ni lazima iwe ni vita.Mwili ni lazima tuushughulishe kama wapiganaji hasa,tukiwa katika roho Maombi yenye matokeo makubwa,ni yale ya kutoka jasho! Ni lazima tumkabili shetani katika vita ya maombi kabla hata hajatushambulia.Katika vita ya siku sita kati ya waisraeli na wamisri, miaka kadha iliyopita;Waisraeli walishinda Wamisri ingawa walikuwa na ndege nyingi zaidi za kivita kuliko wao,kwa kuwa walizipiga KABLA hazijaondoka katika vituo vyao.Tusingoje matatizo ndio tuombe!

§ Imani yetu na ya ndugu zetu,inaweza kutokutindika,ikiwa tu tutakuwa waombaji;kinyume cha hapo ni rahisi kumezwa na
shetani(Luka 22:31-32;1Petro 5:8-9)

§ Maombi ndiyo yanafanya tuutunze utakatifu wetu,na kuwa mbali na dunia.Bila maombi ni rahisi kuvutwa na masumbufu
ya dunia(Luka 21:34-36)

§ Yesu aliliombea Kanisa(Yohana 17:14-15).Ni muhimu kuliombea kanisa na siyo kujiombea wenyewe tu wakati wote.

Je tunaweza kuyatendea kazi yote haya kwa nguvu zetu?jibu ni la.Kwa nguvu zetu hatuwezi,bila msaada wa Roho Mtakatifu.

5. ROHO MTAKATIFU MSAIDIZI ATUSAIDIAYE KUOMBA
Shetani anafahamu sana umuhimu wa maombi,na hivyo atatuzuia sana kufanya maombi kuliko yote mengine, ili tubaki kama matawi ambayo hayajaunganishwa na shina.Anajua pasipo Mungu,sisi hatuwezi neon lolote. Kwa kujifunza tu juu ya maombi,bado hatuwezi kuwa na maisha ya maombi.Tunaweza kuomba sisi hatuwezi neon lolote.Kwa kujifunza tu juu ya maombi,bado hatuwezi kuwa na maisha ya maombi.Tunaweza kuomba siku mbili,tatu,halafu basi.Pamoja na wanafunzi wa Yesu kuhimizwa kuomba na Yesu mwenyewe,bado walishindwa kuwa waombaji(Matahyo 26:37-43).Ndipo hatimaye akawaambia atakuja Msaidizi ambaye kazi yake mojawapo,ni kutusaidia kuomba(Yohana 16:7;Warumi 8:26-28).Yeye Roho,kwa kuwa hutuombea kwa kuugua,na tena ni Roho ya neema na kuomba,huweza kutupa msaada wa kutuwezesha kuomba kwa kuugua na kulia(Zekaria 12:10)Baada ya Roho Mtakatifu kuja na kuwasaidia wanafunzi wa
Yesu,maisha yao ya maombi yalibadilika(Matendo 10:9).Siri ni hii,usitumie nguvu zako kuomba.Kabla ya kuingia katika maombi,
mwombe Msaidizi akusaidie kuomba.

SOMO 4:

UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU

Ili tuweze kuwa mashahidi wa Mungu,tunahitajika kubatizwa kwa Roho Mtakatifu baada ya kuokoka na kutakaswa.Ili tumtendee Mungu kazi kikamilifu,ni lazima tupokee nguvu ya Roho Mtakatifu (Matendo 1:8;Luka 24:49).Kwa sababu hili,somo hili,ni la muhimu sana
kwa mtu yeyote anayetaka kuwa mtendakazi mzuri wa Mungu. Tutaligawa somo hili katika vipengere vinne:-

10. MAANA YA UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU
11. UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU,UWEZA WA KUTUWEZESHA KUWA MASHAHIDI WA MUNGU
12. ALAMA 9 ZA ROHO MTAKATIFU NA JINSI ZINAVYOTUPAUFAHAMU KUHUSU

UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU
13. JINSI YA KUBATIZWA KWA ROHO MTAKATIFU
14. ISHARA YA KWANZA YA KUBATIZWA KWA ROHO MTAKATIFU NA NIDHAMU INAYOAMBATANA
15. UMUHIMU WA KUUCHOCHEA MOTO WA ROHO MTAKATIFU
6. MAANA YA UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU

Baada ya mtu kuokolewa,inambidi kubatizwa kwa maji kwa jina la baba,Mwana na Roho Mtakatifu(Mathayo 28:19).Hata hivyo,huo siyo ubatizo wa mwisho.Baada ya mtu kutakaswa,anahitajika kubatizwa kwa Roho Mtakatifu(Mathayo 3:11) Ubatizo wa maji, unamfanya mtu azamishwe ndani ya maji na kuzungukwa na maji pande zote.Vivyo hivyo,Ubatizo wa Roho Mtakatifu unamfanya mtu aliyeokoka,kuzamishwa ndani ya Roho Mtakatifu na kuzungukwa na Roho Mtakatifu pande zake zote.Roho Mtakatifu,anakuwa msaidizi wake(Yohana 15:26). Ubatizo wa maji,tunabatizwa na wanadamu waliopewa Agizo la Mungu lakini Ubatizo wa Roho Mtakatifu, tunabatizwa na Yesu mwenyewe(Mathayo 3:11).

6. UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU,UWEZA WA KUTUWEZESHA KUWA MASHAHIDI WA MUNGU

Neno “mashahidi”katika (Matendo 1:8),linatokana na neno la lugha ya Kiyunani “Martus” ambalo linatafsiriwa katika Kiingereza,” Martyr” ambalo maana yake ni “Mtu anayekuwa tayari kuteswa sana au hata kuuawa kwa sababu ya imani yake,pamoja na hayo,

hawezi kuiacha imani yake”.Bila ubatizo wa Roho Mtakatifu,hatuwezi kuwa mashahidi kama walivyokuwa Stefano na Antipa (Matendo 22:20;Ufunuo 2:13).Kabla ya kubatizwa kwa Roho Mtakatifu,Petro alisema asingemkana Yesu hata ikibidi kuuawa,
lakini kinyume chake alimkana mara tatu,na yeye pamoja na wanafunzi wenzake walipoyaona mateso yanakuja,walimwacha na
kumkimbia Yesu (Mathayo 26:31-35,56) Lakini baada ya ubatizo walikuwa na ujasiri mkubwa. Matendo 4:13

7. ALAMA 9 ZA ROHO MTAKATIFU NA JINSI ZINAVYOTUPA UFAHAMU KUHUSU UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU

§ Maji (Yohana 7:37-39)Hakuna maisha bila ya maji.Mwanadamu ni asilimia 60%maji.Kuharisha na kutapika sana humfanya mtu kupoteza maji mengi na huweza kusababisha mtu kupoteza uhai.Vilevile sisi tunaosema tumeokoka, hatuwezi kabisakuwa na maisha ya kiroho yaliyo hai yenye nguvu,bila Ubatizo wa Roho Mtakatifu.Ni lazima tunyweshwe Roho (1Wakorintho 12:13) Jambo jingine,maji ni muhimu katika usafi wa miili yetu hutuondolea kunuka n.k Roho Mtakatifu hutumulikia dhambi au uchafu wowote.
§ Moto (Mathayo 3:11).Kuwepo kwa moto ni alama ya uwepo wa Mungu (Kutoka 3:1-5;Matendo 2:2-3).Moto vilevile,unangarisha madini kama dhahabu na fedha(Malaki 3:2-3).Ubatizo wa Roho Mtakatifu hufanya uwepo wa Mungu uwe dhahiri kwa mtu na pia humng’arisha mtu na kuwa mtumishi wa Mungu anayeng

Â’aa .Siyo hayo tu,moto huleta mwanga.Ubatizo wa Roho Mtakatifu hutupa mwanga mkubwa wa maandiko yaani Biblia na kutupa mwanga wa uzuri wa mbinguni na ubaya wa Jehenam.Ukiwa na mwanga huo hakutakuwa na gharama kubwa yoyote ya kukufanya
ushindwe kufanya mapenzi ya Mungu.Moto pia huleta nguvu ya kuendesha,magari,treni,Ndege n.k vifaa vyote hivyo huendeshwa kutokana na moto unaotokea baada ya cheche za umeme kuunguza mafuta.Kazi ya Mungu inaendeshwa kwa nguvu ya moto,ubatizo wa Roho Mtakatifu na kwa moto.Mtu aliyebatizwa kwa Roho Mtakatifu, moto unawake ndani yake na hawezi kuacha kushuhudia au kuhubiri na kufundisha(Yeremia 20:9;Isaya 62:1;Matendo4:20).Mtu
aliyebatizwa kwa Roho Mtakatifu,maneno yake huwa moto unaoteketeza kila ugumu wa mioyo ya watu kwa kuwa Roho Mtakatifu hushuhudia pamoja naye na hivyo matokeo yake ya utumishi wake huwa makubwa.Ni nguvu kwa ajili ya Utumishi (Yeremia 5:14; Yohana 15:26-27;16:6-8;Mika 3:8).

§ Upepo (Yohana 3:8)Upepo wakati wote unatembea,na uko mahali pote.Roho Mtakatifu hakufanya kazi wakati wa mitume tu,hata sasa anatembea na yuko kwetu tayari,ni wajibu wetu kumpokea tu.Upepo huvuma upendako.Ni vigumu kuubadilisha

mkondo wa upepo tunavyotaka sisi,jahazi hufuata mkondo wa upepo.Ni muhimu kutakaswa kwanza kabla ya Ubatizo huu.Utakaso humfanya mtu kuwa mtii mno katika yote na Roho Mtakatifu ni mshirika wa wale wamtiio(Matendo 5:32)Upepo pia hutuletea hewa safi inayotuburudisha wakati wa joto,moshi n.k Mazingira yoyote magumu tukiyakabili katika utumishi wa Mungu,Roho Mtakatifu huwa hewa safi kwetu inayorekebisha mazingira.

§ Mafuta (Luka 4:16-21)Roho Mtakatifu hututia mafuta au kutuweka katika utumishi wa Mungu (1Samweli 16:13;Kutoka 30:30;1Wafalme 19:16;Yohana 2:27)Rais kabla hajaapishwahuitwa Rais mteule na hana mamlaka sana wakati huo kisheria.Kuapishwa kwa leo ndiyo kutiwa mafuta kwa zamani.Bila ubatizo huu,mamlaka yetu huwa hafifu.Mafuta yanalainisha na kuzuia msuguano.Ubatizo wa Roho Mtakatifu hutupa hekima ya kuvuta roho za watu(Mithali 11:30) mafuta huufanya mwili uwe laini.Ubatizo wa Roho Mtakatifu hulainisha ukavu wa maombi yetu (Warumi 8:26)

§ Mvua (Zaburi 72:6;Hosea 6:3)Nchi haiwezi kutoa matunda bila mvua.Mtu aliyeokoka hawezi kuwa na matunda mengi bila mvua yaani ubatizo wa Roho Mtakatifu(Yohana 15:16)

§ Mvinyo(Waefeso 5:18;Matendo 2:12-13) mvinyo kwa walevi unasahaulisha shida.Ubatizo wa Roho Mtakatifu, humwezesha mtu kudharau majaribu na kuondoa wasiwasi na kubabaishwa na mambo madogomadogo tu.Mvinyo kwa walevi, pia unawapa ujasiri wa kufanya lolote lile,aibu,woga vinatoweka.Ubatizo wa Roho Mtakatifu humfanya mtu kuwa jasiri kama simba na mtu aliye kuwa mwoga kama Petro,kuwa jasiri(Mithali 28:1;Mathayo 26:31-35,56;Matendo 4:13).

§ Hua (njiwa)- (Yohana 1:32) Ubatizo wa Roho Mtakatifu haufanyiki kwa mtu wa ulimwengu huu yaani ambaye
hajaokoka.Njiwa hakutua kwenye ulimwengu,alirudi safinani kwa waliookoka(Mwanzo 8:8-9)Roho Mtakatifu ni mweupe, kama hua.Ni Mtakatifu,huja kwa watakatifu waliotakaswa.

§ Muhuri (Waefeso 1:13)Muhuri ni alama ya mamlaka.Bila muhuri barua hupungua mamlaka yake.Ubatizo wa Roho Mtakatifu humfanya mtu kuwa na mamlaka ya Yesu kwake na shetani husema “ Yesu namjua na Paulo namfahamu(Matendo 19:15) Ubatizo wa Roho Mtakatifu ni mamlaka au uwezo kutoka juu wa kuzifanya kazi za Yesu.

§ Arabuni (2Wakorintho 1:21-22)Neno arabuni maana yake- Uhakikisho au uthibitisho wa Uimara.Ubatizo wa Roho Mtakatifu, hutufanya kuwa na uthibitisho wa uimara wa Neno la Mungu, hutuongezea imani ya kufanya maajabu.Shetani hawezi kumpeperusha huku na kule mtu aliyebatizwa kwa Roho Mtakatifu.

8. JINSI YA KUBATIZWA KWA ROHO MTAKATIFU
q Kuokoka au kuzaliwa mara ya pili.Mafuta haya hayatiwi kwa mtu mgeni ambaye jina lake haliko katika kitabu cha Uzima mbinguni (Kutoka 30:31-33)
q Kutakaswa(Yohana 17:17;1Wathesalonike 5:23)Wanafunzi 120 orofani,walitakaswa kabla ya Ubatizo wa
Roho Mtakatifu.
q Kuwa na Imani kama Roho Mtakatifu yuko kwetu tayari na kwamba ni ahadi ya Mungu kwetu(Matendo 2:38-39);Luka 11:10-13)
q Kuwa na kiu ya kumtumikia Mungu(Isaya 44:3)
q Kuomba kwa kufumbua sana kinywa na kutokuruhusu kutumia akili,wala kuwaza kwambatutasema lugha ya
mapepo.(Luka 11:10-13;Zaburi 81:10).

9. ISHARA YA KWANZA YA KUBATIZWA KWA ROHO MTAKATIFU NA NIDHAMU INAYOAMBATANA
Mtu akibatizwa kwa Roho Mtakatifu,kutakuwa na mambo ya kusikia kwake na ya kuyaona kwake(Mathayo 3:16-17).

Ishara ya kwanza ni kusikia kutoka kwake kabla ya kuona mengine.Atasema au ananena kwa lugha mpya asiyoifahamu
ambayo siyo ya dunia hii(Matendo 2:4;10:44-46;19:6).Ni muhimu mno kwa mtu aliyeokoka kuomba kwa kunena kwa lugha hii(1Wakorintho 14:2,4-5,15).Hata hivyo hatupaswi kunena kwa lugha mbele ya mataifa wasioelewa kitu.Watadhani sisi ni wendawazimu(1Wakorintho14:18-25)Kunena kwa lugha mbele ya mataifa wasiojua kitu nikuwapa mbwa kilicho kitakatifu na kutupa lulu zetu mbele ya nguruwe matokeo yake watatudhihaki kwa kuwa hawajui maana (Mathayo 7:6).

10. UMUHIMU WA KUUCHOCHEA MOTO WA ROHO MTAKATIFU
Moto bila kuchochewa huzimika(Mithali 26:20).Hatuna budi kuwa waombaji na kuomba kwa Roho,yaani kunena kwa lugha katika maombi mara kwa mara katika maombi yetu binafsi(1Wakorintho 14:14-15;Yuda 1:20)Vile vile hatuna budi kudumu katika usafi kwa Neno(Zaburi 51:4,11;119:11;Yohana 15:3).Hatuna budi pia kujihusisha katika kushuhudia na kuwaleta watu kwa Yesu (Mika 3:8).

Nyimbo:
Kutakaswa:
1. I will say “YES” Lord x2, “YES” Lord x2 ,I will say YES Lord
Nitasema “NDIO” X2 , “NDIO” Bwana x2,Nitasema “NDIO”

Ubatizo wa Roho Mtakatifu:
2. Moto moto moto moto umewaka x 2, siku ile ya Pentekoste moto umewaka x2.
Moto moto moto moto umewaka x 2, siku ya leo ACL moto umewaka x2
Moto moto moto moto umewaka x 2, siku ya leo Rohoni mwangu moto umewaka x2

Tafuta utakatifu kwani pasipo huo Utakatifu hakuna mtu atakayemwona Mungu.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW