Monday, December 14, 2015

YESU NI MUNGU AMBAYE ANAPONYA MAGONJWA YOTE

Yesu alisema kwamba ishara moja itakayofuatana na waaminio ni kwamba wataweka mikono juu ya wagonjwa nao watapona (ona Marko 16:18).
[Yesu] Akawaambia, Enendeni ulimwengu mwote mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya (Marko 16:15-18).
Mtumishi afanyaye watu kuwa wanafunzi, akiwa anaiga huduma kamilifu ya Kristo, hakika atatumia vipawa vyake kuendeleza huduma ya uponyaji wa Mungu katika eneo lake la ushawishi. Anajua kwamba uponyaji wa Mungu hukuza ufalme wa Mungu kwa njia mbili. Kwanza – miujiza ya uponyaji ni matangazo mazuri sana kwa Injili, kama mtoto yeyote anayesoma Injili au kitabu cha Matendo atakavyoelewa (ingawa watumishi wengi wenye madigirii makubwa wanaonekana hawaelewi). Pili – wanafunzi wenye afya njema hawazuiwi kufanya huduma kwa magonjwa binafsi.
Pia, mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi anahitaji kuwa makini kwa wale katika mwili wa Kristo wanaohitaji uponyaji, ila wana shida ya kupokea. Mara nyingi wanahitaji mafundisho ya taratibu na kutiwa moyo kwa upole, hasa kama wamefikia mahali pa kupingana na ujumbe wowote wa uponyaji. Mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi anakabiliwa na uchaguzi: anaweza kuepuka kufundisha kuhusu uponyaji wa Mungu moja kwa moja. Akifanya hivyo, hakuna atakayekwazika wala hakuna atakayeponywa. Au, anaweza, kwa upendo sana, kufundisha somo hilo na kudiriki kuwakwaza wengine huku akiwsaidia wengine kupokea uponyaji. Mimi binafsi nimeamua kufanya la pili, nikiamini kwamba ni kufuata mfano wa Yesu.
Uponyaji Pale Msalabani
Mahali pazuri pa kuanza kujifunza kuhusu uponyaji wa Mungu ni katika sura ya hamsini na tatu ya kitabu cha Isaya, ambayo huhesabika kuwa unabii kuhusu Masiya. Kwa njia ya Roho Mtakatifu, Isaya anaeleza vizuri sana juu ya kifo cha Yesu cha kujitoa dhabihu na kazi ambayo angetimiza msalabani.
Hakika ameyachukua masikitiko yetu, amejitwika huzuni zetu. Lakini tuimdhania ya kuwa amepigwa, amepigwa na Mungu na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, alichubuliwa kwa maovu yetu. Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe, na BWANA ameweka juu yake maovu yetu sisi sote (Isaya 53:4-6).
Kwa uvuvio wa Roho Mtakatifu, Isaya alitangaza kwamba Yesu alibeba huzuni na masikitiko yetu. Tafsiri nzuri ya lugha ya asili ya Kiebrania inaonyesha kwamba Yesu alichukua magonjwa na maumivu yetu.
Neno la Kiebrania huzuni katika Isaya 53:4 ni neno choli, ambalo pia linapatikana katika Kumbu. 7:15; 28:61; 1Wafalme 17:17; 2Wafalme 1:2; 8:8; na 2Nyakati 16:12; 21:15. Katika maandiko haya yote linatafsiriwa kama magonjwa au maradhi.
Neno masikitiko katika Kiebrania ni makob, ambalo pia linapatikana katika Ayubu 14:22 na 33:19. Pote hapo linatafsiriwa maumivu.

Kwa hali hiyo, Isaya 53:4 inatafsiriwa vizuri kama ifuatavyo: “Hakika magonjwa yetu Yeye Mwenyewe aliyabeba, na maumivu yetu aliyachukua.” Ukweli huu unatiwa muhuri na Mathayo kurejea maneno ya Isaya 53:4 katika Injli yake, hivi: “Yeye Mwenyewe alichukua udhaifu wetu na kuyabeba maradhi yetu” (Mathayo 8:17, TLR).
Kwa kuwa si rahisi kuepuka kweli hizi, kuna wanaojaribu kutufanya tuamini kwamba Isaya alikuwa anasema juu ya “magonjwa ya kiroho” na “maradhi ya kiroho” tuliyo nayo. Lakini maneno ya Isaya 53:4 yanayotumiwa na Mathayo yanaonyesha bila shaka yoyote kwamba Isaya alikuwa anazungumzia magonjwa halisi ya kimwili na maradhi. Hebu tuyatazame katika mantiki yake.
Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, ‘Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, na kuyachukua magonjwa yetu’ (Mathayo 8:16-17. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Mathayo alieleza waziwazikwamba uponyaji wa kimwili uliotendwa na Yesu ulikuwa kutimizwa kwa Isaya 53:4. Basi hakuna shaka kwamba Isaya 53:4 ni maandiko yanayosema kuhusu Kristo kuchukua udhaifu wetu na magonjwa.[2] Sawa na jinsi Maandiko yanavyosema kwamba Yesu alichukua maovu yetu (ona Isaya 53:11), yanasema pia kwamba alichukua maradhi yetu na udhaifu wetu. Hizo ni habari za kumfanya mgonjwa yeyote kufurahi. Kwa dhabihu Yake ya kupatanisha, Yesu alikwisha weka mpango kwa ajili ya sisi kupata wokovu na uponyaji.
Uthibitisho Zaidi Kwamba Ni Mapenzi Ya Mungu Kuponya
Chini ya agano la zamani, uponyaji wa mwili ulikuwemo katika agano la Israeli na Mungu. SIku chache tu baada ya Waisraeli Kutoka Misri, Mungu aliwaahidi hivi:
Kwamba utaisikiza kwa bidii sauti ya BWANA Mungu wako, na kuyafanya yaliyoelekea mbele zake, na kutega masikio usikie maagizo yake, na kuzishika amri zake, mimi sitatia juu yako maradhi yoyote niliyowatia Wamisri; kwa kuwa Mimi ndimi BWANA nikuponyaye (Kutoka 15:26).
Yeyote aliye mkweli atakubali kwamba uponyaji ulikuwemo katika agano la Mungu na Israeli, kutegemeana na utii wa watu. (Hata Paulo anaweka wazi kabisa katika 1Wakor. 11:27-31) kwamba afya ya kimwili katika agano jipya hutegemeana na utii wetu pia.)
Vile vile, Mungu aliwaahidi Waisraeli hivi:
Nanyi mtamtumikia BWANA Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza (Kutoka 23:25-26. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Utabarikiwa kulio mataifa yote; hakutakuwa na mtu mume wala mke aliye tasa kati yenu wala kati ya wanyama wenu wa mifugo. Na BWANA atakuondolea ugonjwa wote; wala hatatia juu yako maradhi yoyote mabaya uyajuayo ya Misri, lakini atayaweka juu ya wote wakuchukiao (Kumbu. 7:14-15. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Ikiwa uponyaji ulihusishwa katika agano la kale, mtu atashangaa kiwa hautahusishwa katika agano jipya, ikiwa agano jipya ni bora kuliko la zamani kama yanavyosema Maandiko.
Lakini sasa [Yesu] amepata huduma iliyo bora zaidi, kwa kadiri alivyo mjumbe wa agano lililo bora, lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora (Waebrania 8:6. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Uthibitisho Zaidi Tena
Biblia ina Maandiko mengi sana yenye kutoa uthibitisho usiopingika kwamba ni mapenzi ya Mungu kumponya kila mtu. Hebu nitaje mistari mitatu iliyo bora zaidi.
Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA. Naama, vyote vilivyo ndani yangu vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA, wala usizisahau fadhili zake zote. Akusamehe maovu yako yote, akuponya magonjwa yako yote (Zaburi 103:1-3. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Ni Mkristo gani atakayepingana na tamko la Daudi kwamba Mungu anapenda kusamehe maovu yetu yote? Ila, Daudi aliaminipia kwmaba Mungu anataka kuponya magonjwa yetu yote.
Mwanangu: sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni uhai kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote (Mithali 4:20-22. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa (Yakobo 5:14-15. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Ona kwamba ahadi hii ya mwisho ni kwa yeyote aliye mgonjwa. Tena, ona kwamba si wazee wala mafuta yanayoleta uponyaji, bali ni “maombi ya imani.”
Je, ni imani ya wazee au ya mgonjwa? Ni imani ya wote wawili. Imani ya mgonjwa inaonyeshwa kwa sehemu anapowaita wazee wa kanisa. Kutokuamini kwa mgonjwa kungeweza kubatilisha matokeo ya maombi ya wazee. Aina hii ya maombi inayosemwa na Yakobo ni mfano mzuri kuhusu “maombi ya makubaliano” ambayo Yesu alitaja katika Mathayo 18:19. Wote wanaohusika katika maombi aina hii lazima “wakubaliane.” Kama mmoja anaamini na mwingine haamini, hawakubaliani.
Pia tunajua kwamba katika vifungu kadhaa, Biblia inamtaja Shetani kama mhusika wa magonjwa (ona Ayubu 2:7; Luka 13:16; Matendo 10:38; 1Wakor. 5:5). Basi, ni sawa kabisa kwamba Mungu apingane na kazi ya Shetani katika miili ya watoto Wake. Baba yetu anatupenda sana kuliko baba yeyote wa duniani anavyoweza kuwapenda watoto wake (ona Mathayo 7:11), nami sijawahi kukutana na baba aliyetamani watoto wake kuwa wagonjwa.
Kila uponyaji wa Yesu wakati wa huduma Yake hapa duniani na kila uponyaji unaotajwa katika kitabu cha Matendo unapaswa kututia moyo kuamini kwamba Mungu anataka sisi tuwe na afya njema. Mara nyingi sana Yesu aliponya watu waliomtafuta ili waponywe, Naye alisema imani yao ilihusika na muujiza wao. Hii inathibitisha kwamba Yesu hakuchagua watu fulani aliotaka kuwaponya. Mtu yeyote mgonjwa angeweza kumjia kwa imani na kuponywa. Alitaka kuwaponya wote, lakini alitaka wawe na imani.
Max Shimba Ministries Org.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW