Saturday, February 3, 2018

FEDHA NA KUPENDA FEDHA

No automatic alt text available.


Nimewahi kumsikia mhubiri mmoja akisema; “Fedha ni shina la maovu, kwa hiyo wakristo wajihadhari nazo.” Na wakristo wengi wamekuwa wakisikika wakisema hivyo, kwa hiyo wanaogopa kuwa na fedha za kutosha.
Lakini ninaposikia watu wakisema hivi, huwa najiuliza wanaupata wapi usemi huu? Biblia haisemi; “Fedha ni shina la maovu.”
Badala yake Biblia inasema hivi;“ Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha;ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi”(1Timotheo 6:10)
Kupenda fedha ni kuwa na tamaa ya fedha; ni kuzitamani fedha. Na kupenda fedha huku ndiko shina moja la mabaya ya kila namna.
Kuwa na fedha nyingi au kidogo siyo dhambi, kwa kuwa fedha ni mali ya Mungu (Hagai 2:8) Lakini kupenda fedha nyingi au kidogo ni shina moja la maovu.
Tamaa ya fedha ndiyo inayoleta wizi, ujambazi, mauaji, dhuluma, kutokutosheka, uchoyo, wivu, uasherati; nakadhalika. Lakini unaweza kuwa na fedha bila ya kufungwa na roho ya kupenda fedha.
Je! Unafahamu ni kwa nini shetani hapendi wakristo safi wawe na fedha? Maana ni kazi ya shetani kuwapiga vita wakristo wanaotaka kujipatia fedha kwa njia ya halali. Akishindwa kuwazuia kupata fedha; atahakikisha zile fedha walizonazo wanazimaliza haraka hata kwa matumizi ambayo hawakupanga.
Je! Unafahamu ni kwa nini?
Kwa sababu anafahamu mkristo safi akiwa na fedha za kutosha, atazitumia hizo kumpiga nazo vita kwa kuihubiri injili! Na shetani anafahamu kuwa Yesu alisema mwisho hautakuja mpaka injili ihubiriwe katika mataifa yote. Kwa hiyo anajua akiweza kuwakosesha wakristo fedha za kutosha ili injili ihubiriwe, yeye anapata muda wa kupumua na kupumzika.
Wengi wameshindwa kujenga makanisa kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Watumishi wa kanisa wanalipwa mishahara kidogo, kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Mikutano ya injili na semina za neno la Mungu hazifanyiki mara kwa mara kwa kukosa fedha. Wainjilisti wanatafuta fedha za kununulia vipaza sauti wanakosa. Na matokeo yake ni kazi ya Mungu kupoa.
Je! Unadhani ni nani ambaye anaweza kutoa fedha yake ili ikahubiri injili kama siyo wakristo wenyewe? Na wakristo watatoaje fedha kama hawana fedha? Na watakuwaje na fedha, kama wanadhani kuwa na fedha nyingi ni dhambi?
Na shetani ameutumia mwanya huu kuzitumia fedha ambazo wanazo watu wasiopenda haki kueneza dhambi na uovu. Je, ni haki kwa nchi nyingine kutumia ma-billioni ya fedha kutengeza silaha ambazo baadaye wanaziharibu tena, huku mamillioni ya watu wanakufa kwa njaa na maafa mengine?
Kwa hiyo usikubali unaposikia mtu akisema kuwa na fedha ni vibaya; lakini uwe mtu wa kutokupenda fedha. Kwa kuwa ukizitamani fedha utajikuta unaanza kuzitafuta hata kwa njia ambazo ni kinyume cha maadili yetu ya Kikristo; na pia kinyume cha utu wa mwanadamu.
Shalom

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW