Tuesday, December 3, 2013

NYOTA YA MTU NA MAISHA ALIYONAYO

Na Mchungaji Josephat Gwajima 16.9.2012


Utangulizi:
Biblia imeeleza kuhusu nyota ya Yesu ilivyoonekana  kutoka mashariki,(Mathayo2:1); Hii inadhihirisha wazi kuwa kila mtu ana nyota yake. Hivyo katika mfulilizo wa somo hili tutaona maana ya nyota, kazi ya nyota, nyota yaweza kufunikwa kichawi, madhara ya kuishi bila nyota, dalili za kuchukuliwa nyota, nyota yaweza kurudishwa na namna ya kutambua nyota yako. Hapa hatuzungumzii kuhusu kusoma nyota au utabiri wa nyota bali tunaangalia nyota kama ilivyo katika Biblia.

MAANA YA NYOTA:
Nyota katika Biblia inawakilisha kipawa, hatma ya mtu, lengo lililomfanya Mungu akulete  hapa duniani na kusudi lako la maisha. Hivyo tunaposema nyota yako ipo au imechukuliwa maana yake hayo mambo yamechukuliwa au yapo. Kimsingi hakuna mtu asiye na maana tangu kuzaliwa kwake, kwasababu kila mtu aliye duniani amekuja kwa kusudi lake.
Kuna tofauti kati ya elimu na nyota; elimu sio nyota lakini elimu yaweza kunoa nyota. Na si kwamba kujifunza kunaleta nyota bali nyota ipo kwa wote lakini elimu inainoa nyota; na ndio maana ni rahisi kumwona mtu hana elimu lakini anamafanikio mahali fulani. Ukisoma Mhubiri 9:11 Biblia inasema wakati na bahati huwapata wote na sio swala la elimu au ujuzi tu.

KAZI YA NYOTA:
  •        Nyota humfanya mtu kuwa mahiri katika utendaji kazi wake. (Effectiveness)
  •        Nyota huleta ubunifu katika maisha ya kila siku (Creativity)
  •        Nyota inamfanya mtu anatenda kwa ufanisi (Efficiency)
  •        Nyota huleta mvuto kwa watu kutoka mbali ili kuleta vitu kwa ajili yako. (Attraction)
  •      Nyota humfanya mtu awe na maisha yenye mwelekeo na kibali mbele za watu. (Acceptance  and Favor)
  •        Nyota humfanya mtu kusikilizwa katika jamii.
Kuna vitu ambavyo mtu anaweza kuvipata kwasababu nyota yake imeonekana. Nyota yaweza kuvuta zawadi yaani vile vitu ambavyo hujavitaabikia, na ndio maana Yesu alipokuwa mdogo aliletewa zawadi na mamajusi wa mashariki. (Mathayo 2:11) kwahiyo nyota ikichukuliwa maana sahihi ni kwamba hayo mambo hapo juu yote hayapo.
Mathayo 2:1-2; Wakati Yesu anazaliwa kulikuwa na watu wanaitwa mamajusi, ambao walikuwa na uwezo wa kusoma nyota. Hivyo katika ulimwengu wa roho waweza kuona watawala wajao, maisha yajayo au yale yatarajiwayo.  Na ndio maana Mamajusi wa mashariki ya mbali waliweza kuifuata nyota ya Yesu.
Nyota inapoonekana inaweza kufuatwa, yaani watu waona zile kazi zake na kumfuata mtu. Kimsingi tunaposema mtu hana nyota maana yake umahiri, ufanisi na kibali vimechukuliwa. Lakini nyota ikionekana  maana yake haya mambo yote yamerudishwa na hapo utamwona mtu anafanikiwa hata kama elimu yake sio kubwa.

NYOTA ILIYOCHUKULIWA/ ILIYOFUNIKWA KICHAWI:
Nyota ikifunikwa au kuchukuliwa kichawi maana yake mvuto, umahiri, ufanisi na uwezo unakuwa umechukuliwa au umefunikwa. Na ndio maana kuna watu wanahangaika kuanzisha kampuni, kujenga nyumba, kulima, au kufanya biashara kama nyota imefunikwa au kuchukuliwa kichawi huwezi kupokea mafanikio ya sahihi kwenye maisha. Watu wengi wanahangaika kuonekana au kukubalika lakini kumbe tatizo lipo kwenye nyota yaani imefunikwa au imechukuliwa kichawi.
Wachawi wanaweza kuona nyota ya mtu na kuifunika ili isionekane; na kwa namna hii watu wengi wanaonekana hawana mafanikio katika maisha kumbe nyota zao zimefunikwa. Hivyo ni muhimu kupambana Kwa Jina la Yesu ili nyota yako ionekane.

MADHARA YA KUISHI BILA NYOTA YAKO:
  •   Kwa kuwa nyota ndiyo inamwezesha mtu kuwa na kila kitu, ndio kusudi la mtu, upendeleo wa mtu; hivyo madhara ya kutokuwa na nyota ni kutokuwa navyo vyote vile.
  •   Siku zote unakuwa unatenda chini ya kiwango (Under performance). Na kwa namna hiyo hakuna mtu anakubali kile unachotenda; yaani elimu na maarifa yote yakuwa chini ya kiwango.
  •   Utapata na kuibiwa; unapata kazi baadaye unaibiwa au unapata mchumba baadaye anaibiwa. Kimsingi huwezi kudumu na haya mambo.
  •   Unapata lakini anatumia mtu mwingine.

DALILI ZA NYOTA ILIYOFUNIKWA:.
  •   Maisha kukosa mwelekeo; mtu akikosa nyota hata kama akiwa na elimu kama nyota haipo lazima mtu huyo atakosa mwelekeo.
  •   Kukwama kibiashara na kuishi maisha kwenye madeni.
  •   Unafanya kazi lakini hupati maendeleo. Yaani mtu anapata mshahara mzuri lakini anakosa mafanikio halisi kwasababu ya nyota iliyofunikwa au kuibiwa.
  •   Wewe ni kiongozi lakini jamii haikutambui.
  •   Ukichangia hoja za mijadala mbalimbali hakuna anayekusikiliza.
  •   Umesoma lakini hupati kazi, na ukipata kazi haiendani na elimu yako
  •   Maisha ya upweke na hakuna anayekujali katika familia.
  •   Unatenda kazi kwa bidii lakini hupandi cheo.
  •   Kama ni binti  sifa zote lakini hakuna anayekuchumbia maana huonekani.
  •   Kuandamwa na mabalaa na mikosi.
  •   Kupotelewa na watu wa muhimu
NYOTA YAWEZA KURUDISHWA:
Hatua ya kwanza kama hujaokoka unatakiwa kuokoka; kuokoka ni kumpokea Yesu awe Bwana na Mwokozi wa maisha yako ili upate uwezo wa kushindana, hivyo ukigundua nyota imechukiliwa unatakiwa umpokee Yesu ndani ya moyo wako. Ni kitu cha kushangaza kuhitaji msaada wa Yesu halafu yeye humtaki kimsingi kuokoka ni hatua ya kwanza ya kurudisha nyota.
Hatua ya pili ni kushindana kwa maombi; kama mtu anayetaka kurudisha nyota yake ni lazima achukue hatua  ya kushindana katika maombi. Hivyo baada ya kuokoka hatua inayofuata ni kushindana ili nyota irudi. Nyota yaweza kurudishwa kwa kuomba katika Jina la Yesu Kristo.

UTAJUAJE NYOTA YAKO NI IPI:
Usithubutu kwenda kwa mganga wa kienyeji au kusoma kwenye magazeti ili kujua nyota yako.  Ni muhimu kujua kilichoibiwa ni kipi katika maisha yako. Isaya 47:13 “Umechoka kwa wingi wa mashauri yako; basi, na wasimame hao wajuao falaki, wazitazamao nyota, watabirio kila mwezi mambo ya mwezi huo, wakakuokoe na mambo yatakayokupata.” FALAKI ni elimu juu ya mambo ya nyota; biblia inataja kuwa kuna watu wanaojishughulisha na usomaji wa nyota. Lakini kuna mambo kadhaa yanayoweza kukuonyesha nyota yako ni ipi:-
Moyo wako, akili zako na mawazo yako yanakuwa katika hilo jambo AMBALO NI NYOTA YAKO. Mfano kama nyota yako ni biashara basi utakuta moyo wako upo kwenye biashara, basi lazima nyota yako ni k biashara. Kama nyota ni kuimba au siasa lazima moyo utakupeleka kwenye kuimba na siasa. Hivyo tambua kuwa kwenye nyota yako ndipo kuna Baraka zako.
Jambo ambalo ni nyota yako utalitenda bila kupambana; Yaani hutatumia nguvu kwenye kulitekeleza jambo hilo.

MAOMBI YA KURUDISHA NYOTA:

Kurudisha nyota Iliyoibiwa:
Baba katika Jina la Yesu, nimetambua kuwa nyota yangu yaweza kufunikwa na kuibiwa; na leo ninaamua kuirudisha kwa Jina la Yesu kila nyota yangu iliyoibiwa, nyota ya kukubaliwa, ufanisi, umahiri, biashara, kazi au nyota ya hatma njema naamuru irudi kwa Jina la Yesu Kristo. Ninaamuru nyota yangu ikombolewe kwa damu ya Yesu, ninaamuru iachiliwe katika Jina la Yesu.



Kufunua nyota iliyofunikwa:
Katika Jina kuu la Yesu ninasafisha nyota yangu iliyofunikwa; nyota ya mafanikio ninaisafisha kwa Jina la Yesu. Katika torati kila kitu husafishwa kwa Damu nami natumia Damu ya Yesu kusafisha nyota yangu katika Jina la Yesu. Ninatakasa nyota yangu iliyochafuliwa katika Jina la Yesu. Ninang’arisha nyota yangu katika Jina la Yesu.

Kuangamiza wasimamizi wa nyota:
Ninasimama kinyume na kila mashetani, wachawi na waganga wa kienyeji wanaoshikilia nyota yangu katika Jina la Yesu. Waliofunika nyota ninawaangamiza katika ulimwengu wa roho, ninateketeza wote walioiba nyota yangu kwa Jina la Yesu. Katika Jina la Yesu niharibu kazi na utawala wa mashetani wanaoiba nyota yangu katika Jina La Yesu.

Kukiri ushindi:                           
Ninatangaza kurudishwa kwa nyota yangu katika Jina la Yesu; ninatangaza maisha yangu kung’arishwa katika Jina la Yesu. Mafanikio yangu yamerudi katika Jina la Yesu. Nimeshinda  kwa damu ya Yesu.

UFUFUO NA UZIMA (THE GLORY OF CHRIST (T) CHURCH)
TANGANYIKA PACKERS,
KAWE, DARES SALAAM.

2 comments:

Unknown said...

Nimesoma maelezo yako kuhusu Neno NYOTA na jinsi ambayo umejitahudi kulijengea muktadha wa kibiblia.Lakini,naona huo muktadha haujajieleza ama kuekeweka vizuri.Kusema "nyota" ya Yesu,sidhani kwamba ile nyota in uhusiano wowote na hicho unachokieleza.Biblia haionyeshi connection Kati ya nyota hiyo na kipawa chake.Pili,hakuna mahali pengine katika Biblia ambapo Kuna maandiko au msitari ambao umrbeba maana kama hiyo.Kwa ufahamu wangu mdogo wake Biblia,hakuna maelezo ya kibiblia ambayo yanahusisha "nyota" na kipaji au kipawa cha mtu.Lazima Biblia ijieleze yanyewe.Lakini ninachoona mimi,neno "nyota" kwa maana uliyojaribu kuitoa ni katika muktadha wa kinajimu(astrilogy) yaani kwa watabiri wa nyota au wasoma nyota.Hiyo nilugha yao,sio lugha au mtazamo wa Biblia.Na maandiko yanatukataza kuwatumia wanajimu au wasoma nyota, na aina zote za uchawi.MTAZAMO WANGU HUO!

Unknown said...

Je, hukusom aya kwenye Mathayo 2:1? Je, huo ni unajimu?

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW