Monday, April 4, 2016

JE, SABATO NI SI SIKU KATIKA JUMA?


1. Je, Israeli walipokuwa jangwani kwani hawakuwa wakitunza sabato kama siku?
2. Kama basi waliitunza sabato, iweje tena Mungu aseme, ‘Hawataingia rahani mwangu’? 

Ndugu msomaji,

Upo ushahidi wa kutosha katika Biblia unaoonyesha kwamba sabato si siku katika juma. Bwana anapoongelea kuhusu safari ya wana wa Israeli anasema:

Kwa hiyo nalichukizwa na kizazi hiki, nikasema, Siku zote ni watu waliopotoka mioyo hawa ... hawataingia rahani mwangu. (Waebrania 3:10-11).

Pia imeandikwa: Maana ameinena siku ya saba mahali fulani hivi, Mungu alistarehe siku ya saba, akaziacha kazi zake zote; na hapa napo, Hawataingia rahani mwangu. (Waebrania 4:4-5).

Katika maandiko haya Mungu anasema kwamba, kutokana na kukasirishwa na uasi wa wana wa Israeli kule jangwani, alimua kwamba hawataingia kwenye raha aliyokuwa amewaandalia. Neno rahani hapa, au kwa Kiingereza rest, ndilo hilohilo sabato. Ndiyo maana hapo juu katika Waebrania. 4:4-5, anahusisha siku ya saba na kuingia rahani.

Lakini hebu tujiulize maswali yafuatayo ili tuweze kupiga hatua zaidi.

1. Je, Israeli walipokuwa jangwani kwani hawakuwa wakitunza sabato kama siku?
Jibu ni ndiyo, waliitunza. Biblia inasema: Basi ikawa siku ya sita wakaokota kile chakula sehemu mara dufu, kila mtu pishi mbili; na wazee wote wa mkutano wakaenda na kumwambia Musa. Akawaambia, Ndilo neno alilonena BWANA,Kesho ni starehe takatifu, Sabato takatifu kwa BWANA ... (Kutoka 16:22-23).

2. Kama basi waliitunza sabato, iweje tena Mungu aseme, ‘Hawataingia rahani mwangu’?
Kama ingekuwa ni kumwuliza Mungu, mtu ungesema, “Bwana, unasemaje hawataingia rahani mwako wakati kila siku ya saba wanapumzika?” Hii ni ishara ya wazi kwamba sabato hasa si kupumzika au kutofanya kazi kimwili katika siku ya saba. Sabato ni jambo jingine tofauti na siku ya saba. Iko sabato halisi ambayo siku ya saba na kupumzika kwake vilikuwa ni kivuli chake tu.

Jambo jingine la kujiuliza ni kwamba, japo ni kweli kwamba wale ambao Mungu alisema hawataingia rahani mwake walifia wote jangwani, lakini walikuwapo wengine wengi walioingia, yaani watoto wao. Sasa je, hao walioingia waliipata hiyo raha (sabato)?

Mtu anaweza kujibu, Ndiyo, maana sote tunajua kuwa hata wakati alipokuja Bwana Yesu, alikuwa akifundisha mara nyingi kwenye masinagogi 'siku ya sabato'. Kwa hiyo, mtu anaweza kusema, ‘Ndiyo, waliingia kwenye raha au kwenye sabato.’

Lakini Mungu ambaye ndiye mwenye usemi wa mwisho juu ya mambo yake mwenyewe anasema:

Basi kwa kuwa neno hili limebaki kwamba wako watu watakaoingia humo, na wale waliohubiriwa habari ile zamani walikosa kuingia kwa sababu ya kuasi kwao, aweka tena siku fulani, akisema katika Daudi baada ya muda mwingi namna hii, Leo; kama ilivyonenwa tangu zamani, Leo, kama mtaisikia sauti yake, msifanye migumu mioyo yenu. Maana kama Yoshua angaliwapa raha (yaani sabato), asingaliinena siku nyingine baadaye. Basi imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu. (Waebrania. 4:4-9).

Yaani, hawa watu licha ya kwamba kila mwisho wa wiki walikuwa wakipumzika, bado Mungu anasema ‘walikosa kuingia.’ Lakini cha kushangaza zaidi ni kwamba, kumbe hata siku yenyewe ilibadilishwa! Je, umeona hayo maneno ‘aweka tena siku fulani’? Pia hapo mwishoni nako anasema, ‘siku nyingine baadaye’!!

Hebu jiulize, inakuwaje siku nyingine wakati tumesema kwamba hadi Yesu anakuja watu hao walikuwa wakipumzika kila mwisho wa wiki?

Jibu ni wazi kwamba ‘siku nyingine’ hapa haimaanishi siku katika juma – maana hiyo haikuwahi kuachwa! Kwa hiyo, ni wazi kwamba, hii ni ‘siku ya sabato’ tofauti na ile iliyojulikana na kufuatwa tangu siku za Musa!

HOJA YA SABATO KUTOKA KINYWANI MWA MUNGU

Iko hoja kwamba sabato ni amri ya muhimu sana kwa sababu ilitoka moja kwa moja kinywani mwa Mungu tofauti na amri zingine ambazo zililetwa kupitia manabii au mitume.

Hoja hii haina uzito kwa sababu kuu mbili:

1. Biblia kwa ujumla wake ni Neno la Mungu ambalo limetoka kinywani mwake lote. Na maandiko yako wazi kwamba: Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa, apate kutenda kila tendo jema. (2 Timotheo. 3:16-17).

Na kimsingi maandiko haya, ukisoma kwenye Biblia ya Kiingereza, hayasemi “Kila andiko lenye pumzi ya Mungu”. Badala yake yanasema: All Scripture is God-breathed (NIV); au All scripture is given by inspiration of God (KJV). Hii ina maana kwamba: Maandiko yote yametokana na pumzi ya Mungu.

Kwa hiyo, hakuna mantiki kusema kwamba andiko hili lina maana zaidi kuliko lile kwa kuwa hili alitamka Mungu mwenyewe. Yote yana nguvu ileile; yote yametoka kwa Mungu yuleyule.

2. Sababu ya pili ni kuwa, Bwana Yesu alisema: Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea yeye aliyenituma. (Matendo ya Mitume. 10:40).

Maana yake ni kuwa Musa au nabii yeyote hakusema kwa niaba yake au kwa nafsi yake mwenyewe. Maneno waliyoyasema na kuyaandika hayakuwa yao.

Ukimpokea Musa au Paulo na maneno yake, unakuwa umempokea Kristo, na hatimaye Mungu Baba mwenyewe.

Kwa hiyo, si sahihi kudhani kuwa maneno ya Musa au ya Paulo ni yake yeye, na kwamba yana uzito wa chini kuliko yale yaliyotoka kinywani mwa Mungu moja kwa moja kuhusiana na sabato.

Mungu awabariki sana.

By permission: Yesu ni Njia, Injili Timilifu, James John, NKJV, NIV, KJV, Christ Nations and Max Shimba Ministries Org.

Ni mimi Max Shimba, mtumwa wa Yesu Kristo,

For Max Shimba Ministries Org,

MAX SHIMBA MINISTRIES ORG ©2016. ALL RIGHTS RESERVED

Everyone is permitted to copy and distribute verbatim copies of this license document, but changing it is not allowed.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW