Thursday, April 7, 2016

JE, YESU ALITUMWA KWA ISRAELI PEKE YAKE (MATHAYO 15:26)?



Ndugu msomaji,
Waislamu “wanahubiri” kuwa Yesu hakuja kwa ajili ya ulimwengu wote bali alikuja kwa ajili ya Wayahudi peke yao. Kisha wanasema kuwa Muhammad ndiye mtume sahihi kwa sababu huyo alikuja kwa ajili ya ulimwengu wote. Andiko wanalotumia kupinga utume wa Yesu kwa ulimwengu ni lile alilolisema Yesu wakati akiongea na mwanamke Mkananayo (yaani asiye Myahudi), ambaye alikuwa anaomba Yesu amponye mwanawe.
Imeandikwa:
Akajibu akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. (Mathayo 15:26).
Mungu ni Mungu wa utaratibu na ratiba kamili. Ndiyo maana hakuumba kila mtu kwa mara moja. Alianza na mtu mmoja tu, kisha wengine wote tukatokea kwa huyo mtu. Vivyo hivyo, alianza kwa kujifunua kwa taifa moja tu duniani kote. Kisha kutokea hapo ndipo wokovu unasambaa kwenye mataifa yote. Ni ukweli ulio wazi kwamba, ukiacha Israeli, jamii zote zilizobakia duniani, kwa asili zilikuwa zikiabudu miungu (yaani mashetani). Ni Israeli peke yao ndio ambao kwa asili walianza na Mungu wa kweli.
Ndiyo maana Bwana Yesu alipoongea na mwanamke Msamaria pale kisimani alimwambia hivi:
Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. (Yohana 2:22).
Wokovu unatoka kwa Wayahudi kwa sababu hakuna taifa jingine lolote duniani ambalo lilimjua Mungu wa kweli – yote yalikuwa na dini za kipagani – iwe ni wazungu, Waafrika, Wahindi, Waarabu, n.k. Huo ndio ukweli.
Kusema kwamba Yesu hakuja kwa ajili ya mataifa yote hakuna tofauti na kusema kuwa, kwa vile Mungu alimuumba Adamu na Hawa peke yake, basi Yeye si wa familia yangu maana hakuniumba na mimi kama alivyomuumba Adamu.
Yesu aliongea na wanafunzi wake siku moja na akawaambia kuwa:
Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanzia tangu Yerusalemu. (Luka 24:46-47).
Je, unaona kwamba Injili inatakiwa kuanzia Yerusalemu? Na je, unaona pia kwamba anasema kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake? Je, mataifa yote ni Israeli peke yake?
Mwanamke Mkananayo alikuja wakati usio wake. Huo ulikuwa ni wakati wa kuhubiri Injili kwa Israeli kwanza ndipo iende ulimwenguni kote.
Ufuatao ni ushahidi zaidi wa maneno ya Bwana Yesu mwenyewe kuthibitisha kwamba alitumwa kwa mataifa yote ulimwenguni na kwamba Yeye ndiye Masihi wa Mungu, yaani aliyepakwa mafuta kwa Roho Mtakatifu kwa ajili ya kuukomboa ulimwengu wote.
Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi. (Matendo 1:8).
Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu (Mathayo 28:19).
Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. (Yohana 3:17).
Na mtu akiyasikia maneno yangu, asiyashike, mimi simhukumu; maana sikuja ili niuhukumu ulimwengu, ila niuokoe ulimwengu. (Yohana 12:47).
Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. (Yohana 10:15-16).
Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja. (Mat 24:14).
Nihitimishe kwa kurejea tena mambo machache niliyoyasema. Mungu amekuwa na kawaida ya kuanza jambo na mtu mmoja.
Aliumba mwanadamu mmoja, kisha tukatokea humo wote.
Alijifunua kwa taifa moja, kisha tukamjua wote.
Alianza na Mwana mmoja (Yesu), kisha tunazaliwa wote kwa imani katika huyo.
Vivyo hivyo, alileta wokovu kwa taifa moja la Israeli, kisha unasambaa kote – ndiyo maana anasema na mwanamke Msamaria pale kisimani – “Wokovu watoka kwa Wayahudi.” (Yohana 4:22).
Hali hii ya kuanza na mtu au sehemu moja, ni ushahidi kuwa wale wote wanaojifariji kwa maneno eti “dini mbalimbali ni njia tofauti ambazo zote zinaishia kwa Mungu”, wanajidanganya na kupoteza muda wao na uzima wao wa milele! “Wokovu watoka kwa Wayahudi” – yaani KWA YESU PEKEE!
Sasa, kwa kuwa muda wa kusambaa kwa wokovu huo ulikuwa haujatimia (maana Mungu anakwenda kwa ratiba ya majira na nyakati), ndiyo maana akamwambia yule mwanamke Mkananayo (yaani asiye Myahudi) kuwa hakutumwa ila kwa Israeli.
Lakini utimilifu wa majira ulipofika, yaani alipokufa na kufufuka, tunaona akiwaagiza sasa mitume wake waende ulimwenguni kote.
Na Biblia inasema wazi: Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono; kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani. Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo. Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga. Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani. Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba. (Waefeso 2:11-16).
Tafakari
Hoji mambo
Jiulize
Chukua hatua
By permission NIV, NKJV, Waislam kwa Yesu, James John, Tanzania Bible Society.
Mungu awabariki sana.
Ni mimi Max Shimba, mtumwa wa Yesu Kristo,
For Max Shimba Ministries Org,
MAX SHIMBA MINISTRIES ORG ©2016. ALL RIGHTS RESERVED
Everyone is permitted to copy and distribute verbatim copies of this license document, but changing it is not allowed.
April 6, 2016

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW