Saturday, March 17, 2018

Kwa Nini Wanasayansi Fulani Humwamini Mungu?

Image result for SCIENTIST BELIVE IN GOD
SAYANSI inaendelea kufunua mambo mapya kuhusu ulimwengu na uhai ulio katika sayari yetu. Hata hivyo, wanasayansi na watu wa kawaida bado wanakabili maswali haya muhimu: Ulimwengu ulitokeaje? Ni nini kilichokuwako kabla ya wakati huo? Kwa nini ulimwengu unaonekana kuwa umebuniwa hasa kwa kusudi la kutegemeza uhai? Uhai ulitokeaje duniani?
Bado sayansi kwa kweli haiwezi kujibu maswali hayo. Watu fulani hawafikiri kwamba itapata kuyajibu maswali hayo. Hivyo, wengi wamelazimika kufikiria upya maoni na imani zao. Hebu tuchunguze mambo matatu yanayowafanya wanasayansi fulani wafikirie kuwapo kwa Muumba.
Je, Ulimwengu Wenye Vipimo Sahihi Ulitokea Wenyewe Tu?
Jambo moja muhimu linahusu vipimo sahihi vya ulimwengu wetu. Kwa nini ulimwengu una sheria za asili zisizobadilika na vipimo visivyobadilika vilivyowekwa kwa usahihi kabisa ili kutegemeza sayari yetu na uhai uliomo?
Tunamaanisha nini tunaposema kwamba ulimwengu wetu una vipimo sahihi? Kwa mfano, fikiria jinsi zile kani nne za msingi zilivyopimwa kwa usahihi: sumaku-umeme, nguvu ya uvutano, kani yenye nguvu ya nyuklia, na kani dhaifu ya nyuklia. Kani hizo huathiri vitu vyote ulimwenguni. Zimepimwa na kusawazishwa kwa usahihi kabisa hivi kwamba mabadiliko madogo tu yanaweza kufanya kusiwe na uhai wowote ulimwenguni.
Watu wengi wanaotumia akili wanaamini kwamba vipimo sahihi vilivyopo ulimwenguni havikutokea tu. John Polkinghorne, aliyekuwa mtaalamu wa fizikia kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, alisema: “Unapotambua kwamba sheria za kiasili zimewekwa kwa usahihi kabisa ili kufanyiza ulimwengu unaoonekana, jambo hilo linakufanya uanze kuamini kwamba ulimwengu haukutokea wenyewe tu, bali ulitokezwa kwa kusudi fulani.”
Mwanafizikia Mwaustralia Paul Davies alikuwa na maoni kama hayo. Anaandika hivi: “Ni wazi kwamba wanasayansi wengi . . . wanadhihaki wazo la kwamba huenda kuna Mungu au hata chanzo fulani kisicho na utu. Mimi sikubaliani nao. . . . Siwezi kuamini kwamba kuwa kwetu ulimwenguni kulitokea tu bila mpango, . . . kupitia tukio kubwa la kiholela lililofanyiza ulimwengu.”
Utata wa Uhai
Tatizo la pili linalowasumbua wanasayansi wa leo linahusu utata wa ulimwengu unaotuzunguka. Mtu anayetumia akili anajua kwamba jambo linapokuwa tata zaidi, ndivyo inavyokuwa vigumu hata zaidi kuamini kwamba limejitokeza lenyewe tu. Hebu fikiria mfano mmoja.
DNA, ambayo ni sehemu muhimu ya uhai, hufanyizwa kutokana na utendaji mwingi wa kemikali ambao hutukia kwa usahihi kabisa. Miongo mitatu iliyopita, Dakt. Frank Salisbury wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Utah, Marekani, alipiga hesabu kuona uwezekano wa molekuli ya DNA kutokea yenyewe tu. Hesabu zake zilionyesha kwamba uwezekano huo ni mdogo sana hivi kwamba haiwezekani kisayansi.*
Utata wa uhai unaonekana hasa katika viumbe vilivyo na viungo tata ambavyo vingekuwa bure ikiwa hakungekuwa na viungo vingine tata. Kwa mfano, fikiria uzazi.
Kulingana na nadharia za mageuzi, viumbe viliendelea kuzaa vilipokuwa vikizidi kuwa tata. Hata hivyo, kufikia wakati fulani, viumbe vya kike vya jamii kadhaa vililazimika kutokeza chembe za uzazi zilizohitaji kuunganishwa na chembe za uzazi za kiume. Ili wazao wao wapate idadi kamili ya kromosomu, chembe za uzazi za kila mzazi hugawanyika kwa njia ya ajabu, hivi kwamba chembe zinazotoka kwa kila mzazi hubaki na nusu ya idadi ya kromosomu. Utaratibu huo huwafanya wazao wasiwe na kromosomu nyingi mno.
Bila shaka, jamii nyingine pia za viumbe zingehitaji kupitia utaratibu huohuo. Basi, ilikuwaje hata “mama wa kwanza” katika kila jamii ya viumbe akapata uwezo wa kuzaa na “baba wa kwanza” aliyekomaa? Wote wawili wangewezaje kugawanya idadi ya kromosomu katika chembe zao za uzazi wakati uleule ili kutokeza kiumbe chenye afya kilicho na baadhi ya sifa za kila mzazi? Na ikiwa chembe hizo za uzazi zilisitawi hatua kwa hatua, viumbe vya kiume na vya kike vya kila jamii vingewezaje kuendelea kuwapo wakati ambapo chembe hizo muhimu bado hazikuwa zimesitawi kikamili?
Hata katika jamii moja ya viumbe, uwezekano wa jambo hilo kutokea lenyewe tu ni mdogo sana hivi kwamba hauwezi kukadiriwa. Uwezekano wa kwamba jambo hilo lilitokea katika jamii moja baada ya nyingine, haupatani na akili hata kidogo. Je, nadharia ya mageuzi inaweza kutatua utata huo? Mambo yaliyotokea yenyewe tu, pasipo mpango wowote, na kiholela, yangewezaje kutokeza mifumo hiyo tata inayohusiana? Viumbe vina sifa nyingi zinazoonyesha mpango na utaratibu, hivi kwamba ni lazima kuwe na Mpangaji mwenye akili.
Wasomi wengi wamefikia mkataa huo. Kwa mfano, mwanahisabati William A. Dembski aliandika kwamba “vitu vilivyobuniwa kwa akili” vilivyo katika “ulimwengu unaoonekana . . . vinaweza tu kuwa vilitokana na mtu mwenye akili.” Mtaalamu wa biokemia ya molekuli Michael Behe anakata maneno kwa kusema hivi: “Unaweza kuwa Mkatoliki kwa dhati na bado uamini nadharia ya Darwin. Hata hivyo, biokemia imefanya iwe vigumu zaidi kuwa mwanasayansi mwenye kutumia akili na wakati uleule kuamini nadharia hiyo.”
Rekodi Isiyo Kamili ya Mabaki ya Viumbe vya Kale
Jambo la tatu ambalo limewatatanisha baadhi ya wanasayansi ni rekodi ya mabaki ya viumbe vya kale. Ikiwa mageuzi yaliendelea kwa miaka mingi sana, tungetazamia kupata mabaki mengi ya viumbe vilivyokuwa vikigeuka. Hata hivyo, hakuna mabaki yoyote ya viumbe hivyo ambayo yamefukuliwa tangu wakati wa Darwin.
Kwa hiyo, wanasayansi kadhaa wamekata kauli kwamba uthibitisho wa mageuzi ni duni sana na haupatani hivi kwamba hauwezi kuthibitisha kwamba uhai ulitokana na mageuzi. Luther D. Sutherland, mhandisi wa vyombo vya angani, aliandika hivi katika kitabu chake Darwin’s Enigma: “Uthibitisho wa kisayansi unaonyesha kwamba wakati wowote ule ambapo viumbe vya aina tofauti vilitokea kwa mara ya kwanza Duniani, iwe ni viumbe vyenye chembe moja au mwanadamu, viumbe hivyo vilikuwa kamili, navyo viungo na sehemu zake zote zilikuwa kamili, zikifanya kazi kikamili. Basi, kutokana na jambo hilo la hakika, hatuna budi kukubali kwamba kabla ya uhai kutokea Duniani kwa mara ya kwanza, kulikuwa na mtu fulani mwenye akili.”
Kwa upande mwingine, rekodi ya mabaki ya viumbe vya kale inapatana sana na utaratibu wa kutokea kwa aina za viumbe vinavyotajwa katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Donald E. Chittick, mwanakemia aliyepata shahada katika Chuo Kikuu cha Jimbo la Oregon, anasema hivi: “Kuchunguza rekodi ya mabaki ya viumbe vya kale kwa makini humfanya mtu afikie mkataa wa kwamba wanyama walizaa kulingana na aina zao, kama vile kitabu cha Mwanzo kinavyosema. Hawakugeuka na kuwa aina nyingine. Uthibitisho uliopo sasa, kama ilivyokuwa wakati wa Darwin, unapatana na rekodi ya kitabu cha Mwanzo ya kwamba viumbe viliumbwa moja kwa moja. Mimea na wanyama wanaendelea kuzaa kulingana na aina zao. Kwa kweli, kuna tofauti kubwa sana kati ya uchunguzi wa mabaki ya viumbe vya kale na nadharia ya Darwin, hivi kwamba wanasayansi fulani wameanza kuamini kwamba mabaki ya viumbe vilivyokuwa vikigeuka hayatapata kuonekana.”
Kuukubali Uthibitisho
Hayo ni machache tu kati ya mambo yanayowatatanisha wale wanaopuuza uthibitisho wa kuwapo kwa Muumba. Wanasayansi fulani wanatambua kwamba kumkataa Mungu hakutokani na uthibitisho unaopatana na akili bali kunatokana na kushikilia makisio na dhana.
Hivyo, baada ya kufanya utafiti na uchunguzi wa kisayansi wenye mafanikio kwa muda mrefu, mtaalamu wa anga Allan Sandage alisema: “Uchunguzi wangu wa kisayansi ndio ulionichochea kufikia mkataa wa kwamba ulimwengu ni tata sana hivi kwamba hauwezi kuelezeka kisayansi. Ninaweza kuelewa chanzo cha vitu vilivyopo kupitia tu chanzo fulani kisicho cha kibinadamu.”
Je, vilitokea vyenyewe tu?
Gazeti National Geographic lilipochapisha jalada linalovutia lenye picha inayoonyesha uhusiano wenye upendo kati ya mama na mtoto, msomaji mmoja aliwaandikia hivi wachapishaji wa gazeti hilo: “Picha hiyo ya mama na mtoto kwenye jalada ni kazi bora ya sanaa. Siwezi kuelewa jinsi mtu anavyoweza kumtazama mtoto huyo mwenye kupendeza ambaye miezi tisa iliyopita alikuwa yai dogo sana linalotoshana na kichwa cha pini ndogo na kusema kwamba alitokea mwenyewe tu.”
Wengi wangekubaliana naye. Dakt. Gerald Schroeder, mwandishi aliyekuwa profesa wa fizikia ya nyuklia, anaulinganisha uwezekano wa ulimwengu na uhai kutokea wenyewe tu na uwezekano wa kushinda mchezo wa kamari mara tatu mfululizo anaposema hivi: “Kabla ya kupokea malipo ya ushindi wako wa tatu, utakuwa ukielekea jela ukishtakiwa kwamba umetumia udanganyifu. Uwezekano wa kushinda mara tatu mfululizo au mara tatu maishani, ni mdogo sana hivi kwamba haiwezekani.”
Alikadiria kwamba ingechukua miaka bilioni nne kwa molekuli moja ya DNA kutokea yenyewe kiasili katika mojawapo ya sayari 100,000,000,000,000,000,000 (1020) zenye “mazingira yanayoweza kutegemeza uhai.” Kuna uwezekano gani kwamba molekuli moja ya DNA ilitokea yenyewe? Alikadiria kwamba uwezekano huo ni sehemu moja kati ya 10415 (moja ikifuatwa na sufuri 415)!

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW