Friday, February 19, 2016

JE, WAKRISTO WANASTAHILI KUITUNZA SIKU YA SABATO? (SEHEMU YA PILI)


Ndugu msomaji,

Kwa kuwa Kristo alitimiza Sheria, je, Wakristo wana wajibu au daraka la kushika Sabato ya kila juma?

Akiongozwa na Roho wa Mungu, mtume Paulo anajibu hivi: “Kwa hiyo mtu yeyote asiwahukumu ninyi katika kula na kunywa au kuhusu sherehe au kuhusu kushika mwezi mpya au sabato; kwa maana mambo hayo ni kivuli cha mambo yanayokuja, bali uhalisi ni wa Kristo.”—Wakolosai 2:16, 17.


Maneno hayo yaliyoongozwa na Roho wa Mungu yanaonyesha kwamba matakwa ambayo Mungu aliwapa watumishi wake yalibadilika sana. Kwa nini yalibadilika? Kwa sababu Wakristo wako chini ya sheria mpya, “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Agano la zamani la Sheria ambalo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa lilifikia mwisho wake wakati kifo cha Yesu kilipotimiza agano hilo. (Waroma 10:4; Waefeso 2:15)


Je, amri ya kushika Sabato ilifikia mwisho pia?
Ndiyo. Baada ya kusema kwamba “tumefunguliwa kutoka katika Sheria,” Paulo alitaja amri moja kati ya zile Amri Kumi. (Waroma 7:6, 7) Kwa hiyo, zile Amri Kumi, kutia ndani sheria ya Sabato, ni sehemu ya ile Sheria ambayo ilifikia mwisho. Kwa hiyo, waabudu wa Mungu, hawako chini ya takwa la kushika Sabato ya kila juma.


Mfano unaofuata unaweza kutusaidia kuelewa badiliko kutoka katika ibada ya Waisraeli kuingia katika ibada ya Kikristo: Nchi inaweza kubadili katiba yake. Baada ya katiba mpya kukubaliwa kisheria, watu hawatakiwi tena kufuata katiba ya zamani. Hata ingawa huenda sheria fulani katika katiba hiyo mpya zikafanana na sheria fulani za katiba ya zamani, sheria nyingine zinaweza kuwa tofauti. Kwa hiyo, mtu angehitaji kujifunza katiba mpya kwa uangalifu ili aone sheria ambazo zinatumika sasa. Kwa kuongezea, raia mshikamanifu angependa kujua katiba hiyo mpya ilianza kutumika wakati gani.


Vivyo hivyo, Mungu aliwapa Waisraeli sheria zaidi ya 600, pamoja na zile amri 10 za msingi. Sheria hizo zilitia ndani sheria kuhusu maadili, dhabihu, mambo ya kiafya, na kushika Sabato. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa “taifa” jipya. (Mathayo 21:43) Kuanzia mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, taifa hilo limekuwa na “katiba” mpya ambayo inategemea sheria mbili za msingi, yaani, kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:36-40) Ingawa “sheria ya Kristo” inatia ndani maagizo mengi ambayo yanalingana na sheria ambazo Waisraeli walipewa, hata hivyo, Sheria fulani ni tofauti kabisa na sheria nyingine hazihitajiwi tena. Sheria ya kushika Sabato ya kila juma ni moja kati ya sheria ambazo hazitumiki tena.


Je, Mungu Amebadili Viwango Vyake?

Je, badiliko hilo la kuacha Sheria ya Musa na kufuata sheria ya Kristo linamaanisha kwamba Mungu amebadili viwango vyake?
Hapana. Yehova amebadili sheria ambazo watu wake wanapaswa kutii kama vile tu mzazi anavyobadili sheria anazowawekea watoto wake ikitegemea umri na hali zao. Mtume Paulo anaeleza hivi jambo hilo: “Kabla ya ile imani kufika, tulikuwa tukilindwa chini ya sheria, tukiwekwa pamoja kifungoni, tukiitazamia imani iliyokusudiwa kufunuliwa. Kwa sababu hiyo Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani. Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji.”—Wagalatia 3:23-25.


Hoja hizo za Paulo zinaihusu vipi Sabato?
Fikiria mfano huu: Mwanafunzi anaweza kuagizwa ajifunze somo fulani shuleni, kama vile useremala, siku fulani ya juma. Hata hivyo, anapoanza kufanya kazi, huenda akahitaji kutumia ustadi aliojifunza, kila siku ya juma badala ya kuutumia siku moja tu. Vivyo hivyo, Waisraeli walipokuwa chini ya Sheria walitakiwa watenge siku moja kila juma ya kupumzika na kuabudu. Hata hivyo, Wakristo wanatakiwa wamwabudu Mungu kila siku badala ya siku moja tu kwa juma.


Basi je, ni kosa kutenga siku moja kila juma ili kupumzika na kuabudu?
Hapana. Neno la Mungu linamruhusu kila mtu ajiamulie jambo hilo, linasema hivi: “Mtu mmoja anaamua kwamba siku moja ni takatifu kuliko nyingine. Mtu mwingine anaamua kwamba siku zote ni sawa. Ni lazima kila mtu afanye uamuzi wake mwenyewe.” (Waroma 14:5, tafsiri ya God’s Word) Ingawa huenda watu fulani wakaamua kuona siku moja kuwa takatifu kuliko siku nyingine, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Mungu hatarajii Wakristo washike Sabato ya kila juma.


“Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani. Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji.”—WAGALATIA 3:24, 25

Ndugu msomaji, leo tumejikumbusha tena kuwa hatupo chini ya Sheria bali tuna haki ya kuzitunza siku zote za Juma na kumwabudu Mungu kila siku, na sio siku moja to ya Jumamosi.

Mungu awabariki sana,

Max Shimba



For Max Shimba Ministries

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW