Tuesday, January 10, 2017

JE, BWANA YESU ANAPATAJE KUWA MUNGU?

Image may contain: text
Ni vyema sasa tukapiga hatua nyingine ya ufahamu kwa kuangalia swali hili makini ambalo kwa kiasi kikubwa pia huchanganya hisia za watu wengi katika ulimwengu wa imani, ambapo kile kinachoonekana kuwachanganya watu wengi hapa ni uelewa juu ya ukweli kuhusu chimbuko la Uungu wa Bwana Yesu na hivyo watu wengi kuhoji kuwa Yesu anapataje sasa kuwa Mungu?
Ni wazi kuwa swali hili hasa hulenga kutafuta kujua asili au chimbuko la mamlaka ya Kiuungu ya Yesu anayotajwa kuwa nayo hasa kutokana na kile kinachoonekana kuwa Bwana Yesu alikuwa na mwonekano unaoonyesha kuwa huenda naye alikuwa na asili au chimbuko la dunia hii.
Hivyo ili kupata majibu ya msingi ya hili ni vyema kwanza tuanze na hoja juu ya asili ya Yesu na ndipo tunaweza kufunguka zaidi kiufahamu na kuelewa mengi zaidi juu ukweli kuhusu Uungu wa Yesu.
Ufahamu juu ya asili ya Yesu:
Kile kilichoongeza upinzani mkubwa wa Mafarisayo na baadhi ya Wayahudi juu ya Uungu wa Yesu ni uelewa usiyo sahihi juu ya asili ya Yesu.
Ufahamu wa wengi kati ya Wayahudi uligotea katika dhana ya mwonekano wa ubinadamu wa Yesu na historia yake ya uzazi wa kidunia toka katika tumbo la Mariam, ambapo kama matokeo ya hili Wayahudi walisikika wakati fulani wakitamka:-
Yahana 6:42
Wakasema, Je! Huyu siye Yesu, mwana wa Yusufu, ambaye twamjua babaye na mamaye? Sasa asemaje huyu, Nimeshuka kutoka mbinguni?
Unaweza sasa kupata pichani juu ya mzizi wa hoja hii, na ni kama tunavyoona katika nukuu hiyo ya kitabu cha Yohana kuwa hoja kuu ya Wayahudi ilikuwa ni kile walichoona kuwa haikuwa sahihi kwa Yesu kusema ameshuka toka mbinguni maana kile wao wanachojua ni kuwa alizaliwa na bi’Mariam na baba yake ni Yusufu kwahivyo asili yake ni duniani tu.
Hivyo kwa hali hiyo iliwapa ugumu kukubali pale Yesu alipojitaja kuwa na asili ya mbinguni na kimsingi ndicho kilichokuwa chanzo kikubwa cha upinzani wao dhidi ya matamko ya Yesu.
Habu ona tena hoja ya Wayahudi pale Yesu alipoeleza uwepo wake wa milele’
Yohana 8: 56-58
Ibrahimu, baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi. 57 Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe hujapata bado miaka hamsini, nawe umemwona Ibrahimu? 58 Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko.

Katika andiko hilo tena Wayahudi walipingana na Yesu kutokana na tamko lake lililoonyesha uhusiano wake na ukaribu na mzee Ibrahimu, kitendo ambacho kilifanya Wayahudi hao kumhoji kwa madai kuwa yeye ni kijana mdogo hasiyepata hata miaka hamsini anawezaje kuwa amemwona Ibrahimu?, na ndipo Yesu anajibu na kuwaambia bayana kuwa uwepo wake ni wa kabla ya Ibrahimu’ 58 Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko.
Hivyo kwa mtazamo wangu binafsi ninaona kuwa tatizo la Wayahudi au wale wanaopinga Uungu wa Yesu kwasababu ya ubinadamu alokuwa nao au sababu ya kuzaliwa na Mariam tatizo lao kuu si hilo bali zaidi ni kutolewa kabisa msingi mzima wa asili ya Yesu kabla ya kuzaliwa kwake na Mariam.
Je’ Asili ya Yesu ni wapi?
Katika kujibu swali hili Bwana Yesu mwenyewe mara kadhaa aliwaelimisha Wayahudi juu ya ukweli kuhusu asili yake ili kuwasaidia kuondokana na dhana au mtazamo wa kumchukulia kama mtu mwenye asili ya kidunia na badala yake alitaka waone kuwa yeye alikuwako kabla ya kuja duniani kama mwanadamu kwa kusudi la ukombozi wa watu. Soma kwa makini maandiko haya:-
Yohana 8:23
Akawaambia, Ninyi ni wa chini, mimi ni wa juu; ninyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu huu
Yahana 6:62
Itakuwaje basi, mmwonapo Mwana wa Adamu akipaa huko alikokuwako kwanza?
Katika maandiko hayo yote mawili, Bwana Yesu kwa uwazi kabisa anaweka bayana juu ya asili yake ya mbinguni kabla ya kufanyika mwanadamu na kuzaliwa na bi’ Mariam, katika andiko lile la kwanza Bwana Yesu anaweka utaofauti wa wazi baina yake na wanadamu wa kawaida kwa kusema ‘Ninyi ni wa chini, mimi ni wa juu; ninyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu huu.
Na katika tamko jingine Yesu anawauliza Wayahudi kuwa Itakuwaje basi, mmwonapo Mwana wa Adamu akipaa huko alikokuwako kwanza?, kwahivyo Yesu anaonyesha kuwa kabla ya ujio wake duniani kuna mahali (mbinguni) alikokuwako kwanza.
Asili ya Yesu na msingi wa mamlaka yake ya Uungu:
Uelewa juu ya asili ya Yesu linakuwa ni jambo rahisi tu sasa kadri ya msingi mzuri tuloujenga tangu mwanzo wa uchanbuzi wa mada hii na hususani kupitia matamko mbalimbali hata yale ya Yesu mwenyewe yanayotoa picha ya wazi kuwa Yesu hakuwa kamwe na asili ya dunia hii ya ubinadamu licha ya kwamba alizaliwa na Mariam kwakuwa pale alipozaliwa na Mariam haukua ndiyo mwanzo wa kuwepo kwakwe, bali kupitia kuzaliwa na Mariam alikuwa tu akitengenezewa njia ya kufunika mamlaka yake ya kuu ili aweze kumfikia mwanadamu kama tutakavyoona katika kipengele kinachofuata.
Hatahivyo kanuni za msingi zinazofanya Yesu kuwa mwanadamu wa asili ya kawaida hazikufikiwa katika mchakato wa kuzaliwa kwake, hebu tusome kidogo andiko hili’
Mathayo 1:18
Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu.
Hivyo kuzaliwa kwa Yesu kunatofautiana kabisa na kanuni ya kawaida ya uzazi wa wanadamu wengine ambapo kadri ya andiko hilo Biblia inaweka bayana kuwa Mariam alipata mimba ya kumzaa Yesu kabla hajakaribiana na mwanamume na yakuwa mimba hiyo ni kwa uwezo wa roho mtakatifu.
Kwa hali hiyo katika uzazi wa Yesu hapakuwepo kamwe na mfumo wa kawaida wa kibaolojia unaohusisha hatua mbalimbali za Kisayansi za uzazi kama ambavyo hata maandiko ya Qur an yanavyoainisha katika sura mojawapo ya kitabu cha msaafu wa Qur an kama tunavyosoma hapo chini:-
Qur an 22:5
Enyi watu! Kama mumo katika shaka juu ya ufufuo; (mnaona haimkiniki kufufuliwa), basi (tazameni namna Tulivyokuumbeni); kwa hakika Tulikuumbeni kwa udongo. (Mzee wenu Nabii Adamu),kisha (Tukawa Tunakuumbeni ninyi) kwa manii, (mbegu ya uhai)
Msahafu wa Qur an hapo unaweka bayana hatua hizo za uumbaji na inazitaja kama kanuni zilizo na zinazotumika kuibua mwanadamu na kuendeleza kizazi cha wanadamu huyo, ambapo njia hizo mbili yaani ile awali ya kuumbwa kwa udongo (Nabii Adam na Hawa) na ile ya mbegu ya uzazi (Viumbe wengine).
Hivyo Yesu alizaliwa kipindi ambacho mfumo wa kupatikana kwa mwanadamu au kiumbe cha kawaida unapaswa kuhusisha jinsia mbili za wanadamu ambao hujamiiana na hatimaye mama hutunga mimba na kuzaa binadamu mwingine wa kawaida baada ya miezi tisa ya kubeta ujauzito kama sayansi inavyoeleza kwa upana zaidi:-
‘Sexual reproduction is a process that creates a new organism by combining the genetic material of two organisms; and this is followed by exchange of genetic information (a process called genetic recombination). After the new recombinant chromosome is formed it is passed on to progeny.’
Uzazi wa kujamiiana ni hatua inayoumba kiumbe kipya kwa njia ya kukutanisha viini vya uzazi vya pande mbili za viumbe hai; na hili linafuata baada ya mbadilishano wa taarifa baina ya viini vya uzazi (mchakato huu hutambulika kama muunganiko wa kiuzazi). Baada ya muunganiko mpya nyuzi zenye jeni za urithi wa tabia za maumbile katika kiini cha seli hutengenezwa na kupita katika homoni za kike ambazo huwezesha hali ya uzazi katika uterasi na kukuza kiini tete.(na hatua mbalimbali huendelea hadi kuzaliwa kiumbe).’
Hivyo kwajumla kiumbe kingine hutokea kwa kanuni hiyo tu ya mmunganiko wa seli za uzazi toka pande zote mbili za jinsia yaani toka kwa baba na kwa mama tendo ambalo kamwe halikufanyika katika hatua za kuzaliwa kwa Bwana Yesu na hivyo kuibua tafakari kubwa juu ya asili yake na mamlaka yake hasa.
Na hivyo katika sehemu hii tutakwenda moja kwa moja katika maandiko ya msingi ili kupata ufumbuzi kamili juu ya mamlaka hasa ya asili ya Bwana Yesu na kwa hali hiyo basi nivyema kwanza kujenga msingi wa hili kupitia maelezo ya ya mtume Yohana:-
Yohana 1:1
Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu 2’ Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu.
Ni wazi msomaji wangu kuwa’ sasa unaweza kuanza kupata nuru baada ya kusoma andiko hilo la Injili ya Yohana ambapo kwa uwazi kabisa mtume Yohana kwa msaada wa Roho Mtakatifu anabainisha msingi wa asili ya Yesu na kumtaja dhahiri Bwana Yesu kuwa ndiye ‘Neno’ aliyekuwako mbinguni ,na kimsingi ndiye mhusika wa kazi nzima ya uumbaji.
Na kama utakumbuka vizuri ndugu msomaji wangu hapo nyuma nilishazungumzia kwa upana kabisa juu ya utendaji wa Mungu katika nafsi tatu za milele Mungu mmoja, ambapo Neno (Mwana)’ni miongoni mwa nafsi hizo:-
Hivyo kwa hali hiyo mtume Yohana anaweka bayana na kumtambulisha Neno huyo kwamba alikuwa ni Bwana Yesu mwenyewe kabla hajafanyika mwanadamu. Rejea maelezo ya aya ya 14’ ya Injili ya Yohana sura ya 1’.
14’Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.
Aya hiyo ya 14’ inataja wazi kuwa Neno huyo ni Yesu ambaye hatimaye alifanyika mwili na kukaa kwetu ndipo kwa kuonekana katika utukufu ikaonekana kuwa ni mwana pekee atokaye kwa Baba. (Tutaliona hilo mbele).
Na kwa msingi huo basi Biblia inaweka bayana kuwa Bwana Yesu yeye alikuwako kabla ya Ulimwengu huu kuwako na kama ni msomaji mzuri wa Biblia utagundua kwamba hata Yesu mwenyewe katika matamko yake mbalimbali ameweka bayana swala hili la kuwepo kwake mbinguni katika umoja wa Mungu naye akiwa ni nafsi ile ya Neno. Hebu tusome wote aya hii:
Yohana 17:5
Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.
Hapo Bwana Yesu mwenyewe anatamka wazi kuwa alikuwako kabla ya ulimwengu kuwako na zaidi ya yote anaonyesha kuwa alikuwa katika umoja wa utendaji na umiliki na nafsi ya Baba na hivyo utagundua kwamba maelezo hayo yanawiyana sawia na yale aliyowahi kuyatoa mbele ya Wayahudi na kupelekea Wayahudi hao kuadhimu kumpiga kwa mawe kwakuwa waligundua kuwa kwa kutamka hivyo alikuwa akijitambulisha kuwa yeye kiasili ana mamlaka ya Kiuungu kiasili. Reje aya hiyo hapo chini:-
Yohana 10:30-33
Mimi na Baba tu umoja. 31 Basi Wayahudi wakaokota mawe tena ili wampige. 32 Yesu akawajibu, Kazi njema nyingi nimewaonyesha, zitokazo kwa Baba; kwa ajili ya kazi ipi katika hizo mnanipiga kwa mawe? 33 Wayahudi wakamjibu, Kwa ajili ya kazi njema hatukupigi kwa mawe; bali kwa kukufuru, na kwa sababu wewe uliye mwanadamu wajifanya mwenyewe u Mungu.
Pamoja na hayo kipengele muhimu sana katika aya ile ya Yohana 1:1, ni kile kinachotaja bayana juu ya mamlaka aliyokuwa nayo Bwana Yesu akiwa mbinguni kwa kusema:- (rejea sehemu ya mwisho ya aya ya kwanza’)
Yohana 1:1……naye Neno alikuwa Mungu.
Hapa mtume Yohana anataja wazi kabisa juu ya nafasi hasa ya kimamlaka aliyokuwa nayo Bwana Yesu akiwa mbinguni kwamba alikuwa katika mamlaka kamili ya Uungu.
Kimsingi hiyo ndiyo mamlaka halisi ya Bwana Yesu kama inavyowekwa bayana katika mafungu lukuki ndani ya Biblia kama tulivyoanza kuona katika maandiko hayo ya awali na yale tutakayoendelea kuyapitia katika vipengele mbalimbali vya uchambuzi wa mada hii.
Vinginevyo katika andiko hilo la Yohana 1;1-3 huwa ninasikia hoja fulani ikijengwa ambayo ninatamani kuiweka wazi pamoja na kuipatia majibu mafupi ili kuondoa chachu inayojaribu kuwekwa na baadhi ya walimu wenye lengo la kuhafifisha maana ya msingi ya andiko hilo ili kupingana na ukweli huu.
Hoja inayaojengwa hapo ni ile yenye lengo la kupingana maelezo ya andiko hilo juu ya kuwepo kwa Neno aliyekuwako kwa Mungu naye kuwa Mungu, na katika kupingana na maelezo hayo ya wazi ya andiko wamekuwa wakiweka mfano kwa kudai kuwa kuyakubali maelezo hayo ya andiko la Yohana ni sawa na kusema:- (Yohana 1:1-3)
“Hapo mwanzo kulikuwa na kistuli, nacho kistuli kilikuwa kwa fundi, nacho kistuli kilikuwa fundi’“
Hivyo kwa mfano huo unaowekwa na baadhi ya walimu katika ulimwengu wa imani zetu ndipo wafuasi na baadhi ya waamini wa dini hizo hujikuta wakitiwa moyo na kupinga kwa nguvu zote juu ya ukweli huu wa mamlaka ya Yesu ya Uungu.
Jibu la msingi la hoja hii’
Endapo utachunguza kwa makini juu ya hoja hii utagundua kuwa ni hoja ndogo sana hasa ukiwa na utulivu wa kiakili na kuanza kwanza kwa kuuchunguza mfano wenyewe unaotumiwa ambapo utagundua kuwa mfano huo umechanganya dhana mbili zisizopaswa kuchanganywa, dhana hizo zilizochanganywa ni ile ya kunasibisha Neno na Mungu na kielelezo cha Kistuli na Fundi pasina kujali kuwa kistuli ni mti na fundi ni mtu na hivyo haviwezi kuakisi dhana ya umoja tofauti na uhusiano na umoja wa kiasili uliyopo baina ya Neno na Mungu.
Hivyo ni vyema ikaeleka kuwa uhusiano uliyopo baina ya Neno na Mungu kamwe hauwezi kulinganishwa na fundi na kistuli na badala yake ungeweza kulinganishwa na uhusiano wa Kistuli na Mti’ , na kwa hali hiyo mfano ambao ungeweza kutumika ni ule wa kusema:- (Yohana 1;1-3).
“Hapo mwanzo kulikuwako na Kistuli, nacho Kistuli kilikuwa kwa Mti, nacho Kistuli kilikuwa Mti.”
Mfano huo ndiyo unaoweza kuwiyana na andiko hilo la Yohana kwakuwa kimsingi unahusisha dhana mbili zinazowiyana (Kistuli na Mti) na hivyo kuakisi msingi halisi na mantiki ya maelezo ya andiko lile la Injili ya Yohana.
Hivyo kwajumla mfano unaotumiwa na walimu hao si sahihi na kwa lugha nyingine ni kumaanisha kuwa Neno na Mungu ni mamlaka zisizoweza kutenganishwa kiasili, kama ambavyo huwezi kutenganisha kati ya kistuli na mti maana kimsingi asili ya kistuli ni mti kama ambavyo asili ya Yesu ni Uungu.
Shalom.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW