Saturday, May 27, 2017

ELISHA ALIONA MAGARI YA VITA YA MOTO

Image may contain: text
ELISHA ALIONA MAGARI YA VITA YA MOTO
NABII ELISHA:
Elisha (kwa Kiebrania אֱלִישַׁע, Elisha, yaani "Mungu wangu ni wokovu", kwa Kigiriki Ἐλισσαῖος, Elissaios au Ἐλισαιέ, Elisaie, kwa Kiarabu الْيَسَع Elyasaʿ) alikuwa nabii anayetajwa katika Biblia.
Elisha alikuwa mwana wa Shaphat kutoka Abel-meholah aliyepata kuwa mfuasi wa nabii Elia (Kitabu cha kwanza cha Wafalme 19:16–19).
Sasa tusome simulizi zake kidogo:
Mfalme wa Siria alikuwa akimwinda Elisha, nabii wa Mungu, na kumfuatilia hadi Dothani, jiji lenye ukuta lililo mlimani. Wakati wa usiku, mtawala huyo wa Siria alipeleka farasi, magari ya vita, na wanajeshi huko Dothani. Asubuhi, majeshi yake yalikuwa yamezunguka jiji hilo.—2 Falme 6:13, 14.
Mtumishi wa Elisha alipoamka na kutoka nje, akawaona watu waliokuja kumkamata nabii huyo. Basi mtumishi huyo akalia akisema: “Ole, bwana wangu! Tutafanya nini?” Elisha akamjibu hivi: “Usiogope, kwa maana wale walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” Kisha nabii huyo akasali hivi: “Ee Mungu, tafadhali fungua macho yake, ili aone.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Mara moja Mungu akafungua macho ya yule mtumishi, hivi kwamba akaona; na, tazama! lile eneo lenye milima lilikuwa limejaa farasi na magari ya vita ya moto kumzunguka Elisha pande zote.” (2 Falme 6:15-17) Tunaweza kujifunza nini kutokana na tukio hilo na mengine yaliyompata Elisha maishani mwake?
Elisha alikuwa mtulivu walipozingirwa na Wasiria kwa sababu alimtegemea Mungu naye akaona ulinzi Wake. Ingawa leo hatutarajii miujiza, tunatambua kwamba Mungu huwalinda watu wake wakiwa kikundi. Kwa njia fulani, sisi pia tunazungukwa na farasi na magari ya vita yenye moto. ‘Tukiyaona’ kwa macho yetu ya imani na tukimtegemea Mungu siku zote, ‘tutakaa kwa usalama’ na kupata baraka za Mungu. (Zaburi 4:8) Acheni tufikirie jinsi tunavyoweza kufaidika kutokana na matukio mengine katika maisha ya Elisha.
ELISHA AANZA KUMTUMIKIA ELIYA
Pindi moja Elisha alipokuwa akilima shamba, nabii Eliya alimkaribia na kulitupa vazi lake rasmi juu yake. Elisha alijua maana ya tendo hilo. Akafanya karamu, akawaaga baba na mama yake, na kuondoka nyumbani ili kumhudumia Eliya. (1 Falme 19:16, 19-21) Kwa kuwa Elisha alijitolea kwa utayari kumtumikia Mungu kikamili iwezekanavyo, Mungu aliweza kumtumia kwa njia nyingi na baadaye akatumikia akiwa nabii baada ya Eliya.
Elisha alimtumikia Eliya kwa miaka sita hivi. Wakati huo, Elisha ndiye “aliyemimina maji juu ya mikono ya Eliya.” (2 Falme 3:11) Katika siku hizo, ilikuwa desturi ya watu kula kwa kutumia mikono yao badala ya uma, visu, au vyombo vingine vya kulia chakula. Baada ya mlo, mtumishi angemimina maji juu ya mikono ya bwana wake ili kuisafisha. Hivyo, kazi fulani za Elisha zilikuwa za hali ya chini. Hata hivyo, aliliona kuwa pendeleo kuwa mtumishi wa Eliya.
Leo, Wakristo wengi wanatumikia katika aina mbalimbali za utumishi wa wakati wote. Kwa kufanya hivyo, wanachochewa na imani na tamaa ya kutumia nguvu zao kikamili iwezekanavyo katika kumtumikia Mungu. Wengine wanalazimika kuondoka nyumbani ili kutimiza migawo fulani kama utumishi wa Betheli, miradi ya ujenzi, na kadhalika, jambo ambalo huenda wengine wakaliona kuwa la hali ya chini. Mkristo yeyote hapaswi kuona utumishi wa aina hiyo kuwa duni au wa hali ya chini kwa kuwa Mungu anauthamini sana.—Ebrania 6:10.
ELISHA ALIBAKI KATIKA MGAWO WAKE
Kabla Mungu ‘hajamchukua Eliya katika dhoruba ya upepo kwenda juu kuelekea mbinguni,’ alimtuma nabii huyo kutoka Gilgali ili aende Betheli. Eliya alipendekeza kwamba mwandamani wake asiende naye, lakini Elisha akamjibu hivi: “Mimi sitakuacha.” Walipoendelea na safari, Eliya alimsihi mara mbili zaidi Elisha abaki lakini akakataa. (2 Falme 2:1-6) Kama Ruthu alivyoshikamana na Naomi, ndivyo Elisha alivyoshikamana na Eliya. (Ruthu 1:8, 16, 17) Kwa nini? Kwa sababu Elisha alithamini pendeleo alilopewa na Mungu la kumhudumia Eliya.
Elisha anatuwekea mfano bora sana. Tukipewa mapendeleo fulani ya utumishi katika tengenezo la Mungu, tutayathamini sana ikiwa tutakumbuka kwamba tunamtumikia Mungu. Hakuna heshima kubwa zaidi kuliko hiyo.—Zaburi 65:4; 84:10.
“OMBA LILE NINALOPASWA KUKUTENDEA”
Wanaume hao wawili walipokuwa wakisafiri, Eliya akamwambia Elisha hivi: “Omba lile ninalopaswa kukutendea kabla sijachukuliwa kutoka kwako.” Elisha akatoa ombi lililohusu mambo ya kiroho kama alilotoa Sulemani miaka mingi mapema. Aliomba kwamba ‘sehemu mbili za roho ya Eliya zije kwake.’ (1 Falme 3:5, 9; 2 Falme 2:9) Katika Israeli, mwana mzaliwa wa kwanza alipaswa kupewa sehemu mbili za urithi. (Kumbukumbu 21:15-17) Kwa kweli, Elisha aliomba kutambuliwa kuwa mrithi wa kiroho wa Eliya. Zaidi ya hilo, ni wazi kwamba Elisha alitaka kuwa na roho ya ujasiri kama ya Eliya, aliyekuwa na “wivu kwelikweli kwa ajili ya Mungu.”—1 Falme 19:13, 14.
Eliya aliitikiaje ombi la mtumishi wake?
Nabii huyo akasema hivi: “Umeomba jambo gumu. Ukiniona wakati nitakapochukuliwa kutoka kwako, itakuwa hivyo kwako; lakini kama sivyo, haitakuwa hivyo.” (2 Falme 2:10) Inaonekana kwamba jibu la Eliya lilikuwa na maana mbili. Kwanza, ni Mungu tu angeweza kuamua ikiwa Elisha angepokea kile alichoomba. Pili, ili Elisha apokee alichoomba, alipaswa kudumisha azimio lake la kushikamana na Eliya hata jambo gani litokee.
ALICHOONA ELISHA
Mungu alikuwa na maoni gani kuhusu ombi la Elisha la kupewa sehemu mbili za roho ya Eliya?
Simulizi hilo linasema hivi: “Ikawa kwamba walipokuwa wanatembea, wakizungumza huku wakitembea, tazama! gari la vita lenye moto na farasi wenye moto, nao wakawatenganisha hao wawili; na Eliya akaanza kupanda katika ile dhoruba ya upepo kuelekea mbinguni. Wakati huo wote Elisha alikuwa akiona jambo hilo.”* Hilo lilikuwa jibu la Mungu kwa ombi la Elisha. Elisha alimwona Eliya akichukuliwa kutoka kwake, akapokea sehemu mbili za roho ya Eliya na kuwa mrithi wa kiroho wa nabii Eliya.—2 Falme 2:11-14.
Elisha akachukua vazi rasmi lililokuwa limeanguka kutoka kwa Eliya na kulivaa. Vazi hilo sasa lilimtambulisha Elisha kuwa nabii wa Mungu. Uthibitisho zaidi wa kwamba amewekwa rasmi ulionekana wazi baadaye alipofanya muujiza wa kugawanya maji ya Mto Yordani.
Bila shaka, Elisha hangesahau kamwe kile alichoona Eliya alipokuwa akipaa katika dhoruba ya upepo. Kwa kweli, si jambo la kawaida kwa mtu kuona gari la vita lenye moto na farasi wenye moto! Mambo hayo yalithibitisha kwamba Mungu alikubali ombi la Elisha. Mungu anapojibu sala zetu, hatupati maono ya gari la vita lenye moto na farasi wenye moto. Lakini tunaweza kutambua kuwa Mungu anatumia nguvu zake nyingi kuhakikisha kwamba mapenzi yake yanatendeka. Na tunapoona Mungu akibariki sehemu ya kidunia ya tengenezo lake, ni kana kwamba ‘tunaona’ gari lake la kimbingu likiwa katika mwendo.—Ezekiel 10:9-13.
Elisha aliona mambo mengi yaliyomsadikisha kwamba Mungu ana nguvu nyingi sana. Kwa kweli, roho takatifu ya Mungu ilimwezesha nabii huyo kufanya miujiza 16, mara mbili zaidi ya miujiza aliyofanya Eliya.* Elisha aliona farasi wenye moto na gari la vita lenye moto kwa mara ya pili, walipokabili hali ngumu huko Dothani kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii.
ELISHA ALIMTEGEMEA MUNGU
Elisha alibaki akiwa mtulivu ijapokuwa alizungukwa na maadui huko Dothani. Kwa nini?
Kwa sababu alikuwa amesitawisha imani yenye nguvu katika Mungu. Sisi pia tunahitaji imani ya aina hiyo. Kwa hiyo, acheni tusali ili kupata roho takatifu ya Mungu ili tuweze kuonyesha imani na sifa nyingine za tunda la roho.—Luka 11:13; Galatia 5:22, 23.
Jambo lililotokea huko Dothani lilimpa pia Elisha sababu nzuri ya kumtegemea Mungu na majeshi yake yasiyoonekana. Nabii huyo alitambua kwamba Mungu aliwatuma malaika zake ili kulizunguka jiji na wale waliolizingira. Mungu alimwokoa kimuujiza Elisha na mtumishi wake alipowapiga maadui hao kwa upofu. (2 Falme 6:17-23) Katika kipindi hicho hatari, kama tu alivyofanya katika hali nyingine, Elisha alionyesha imani naye alimtegemea kabisa Mungu.
Kama Elisha, acheni tumtegemee Mungu. (Met. 3:5, 6) Tukifanya hivyo, “Mungu mwenyewe atatuonyesha kibali na kutubariki.” (Zaburi 67:1) Ni kweli kwamba hatuzungukwi kihalisi na farasi na magari ya moto. Hata hivyo, wakati wa “dhiki kuu” inayokuja, Mungu atatulinda tukiwa undugu wa ulimwenguni pote. (Mathayo 24:21; Ufunuo 7:9, 14) Kabla ya wakati huo, acheni tukumbuke sikuzote kwamba “Mungu ni kimbilio letu.”—Zaburi 62:8.
Shalom,
Max Shimba Mtumwa wa Yesu Kristo

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW