Saturday, May 13, 2017

UNABII NI NINI?


Image may contain: text
JE, UNAJUA MAANA YA UNABII NA JINSI UNAVYOPATIKANA?
Unabii ni ujumbe ulioongozwa na Roho ya Mungu, ufunuo kutoka kwa Mungu. Biblia inasema kwamba manabii “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na Roho Mtakatifu.” (2 Petro 1:20, 21) Kwa hiyo, nabii ni mtu anayepokea ujumbe kutoka kwa Mungu na kuwapitishia wengine ujumbe huo.— Matendo 3:18.
JE, MANABII WALIPATE UJUMBE KUTOKA KWA MUNGU?
Mungu alitumia njia kadhaa kuwapitishia manabii wake mawazo yake:
KWA KUTUMIA MAANDISHI:
Mungu alitumia njia hii angalau pindi moja alipompa Musa zile Amri Kumi zikiwa zimeandikwa.—Kutoka 31:18.
KUPITIA MALAIKA WAKE:
Kwa mfano, Mungu alitumia malaika kumletea Musa ujumbe ambao alipaswa kumpelekea Farao wa Misri. (Kutoka 3:2-4, 10) Wakati ambapo maneno hususa yalikuwa muhimu, Mungu aliwaongoza malaika wamwambie mtu maneno hususa ya kuandika, kama alivyofanya alipomwambia Musa hivi:
“Jiandikie maneno haya, kwa sababu ninafanya agano pamoja nawe na Israeli kupatana na maneno haya.”—Kutoka 34:27. *
KUPITIA MAONO:
Nyakati nyingine nabii alipokea maono alipokuwa macho na akiwa anafahamu kabisa kinachoendelea. (Isaya 1:1; Habakuki 1:1) Maono mengine yalikuwa halisi kabisa hivi kwamba wahusika waliyashiriki. (Luka 9:28-36; Ufunuo 1:10-17) Pindi nyingine, maono yalipitishwa mhusika akiwa katika njozi. (Matendo 10:10, 11; 22:17-21) Pia Mungu aliwasilisha ujumbe wake katika ndoto wakati ambapo nabii alikuwa amelala.—Danieli 7:1; Matendo 16:9, 10.
KUPITIA AKILI-KUIONGOZA AKILI:
Mungu aliongoza mawazo ya manabii wake ili kupitisha ujumbe wake. Hiyo ndiyo maana inayotolewa na maneno haya ya Biblia: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” Maneno hayo yanayosema “limeongozwa na roho ya Mungu” yanaweza pia kutafsiriwa “lenye pumzi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16; Union Version) Mungu alitumia roho yake takatifu, au kani ya utendaji, kuingiza mawazo yake katika akili za watumishi wake. Ujumbe ulikuwa wa Mungu, lakini manabii ndio waliochagua namna ya kuyapanga maneno.—2 Samweli 23:1, 2.
Je, nyakati zote unabii unahusisha kutabiri wakati ujao?
Hapana, unabii wa Biblia hautabiri tu kuhusu mambo ya wakati ujao. Hata hivyo, ujumbe mwingi kutoka kwa Mungu unahusiana na wakati ujao, hata ikiwa si moja kwa moja. Kwa mfano, manabii wa Mungu waliwaonya Waisraeli wa kale kuhusu njia zao mbaya. Maonyo hayo yalifafanua baraka za wakati ujao ikiwa watu wangetii, na pia yalitaja madhara ambayo wangepata kwa kutotii. (Yeremia 25:4-6) Matokeo yalitegemea njia ambayo Waisraeli waliamua kufuata.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.
Mifano ya unabii wa Biblia usiohusisha utabiri
Pindi moja Waisraeli walipomwomba Mungu msaada, alituma nabii kueleza kwamba kwa kuwa walikataa kutii amri za Mungu, basi Mungu alikataa kuwasaidia.—Waamuzi 6:6-10.
Wakati ambapo Yesu alizungumza na mwanamke Msamaria, alifunua mambo kuhusu maisha yake ya zamani ambayo hangeweza kuyajua bila kufunuliwa na Mungu. Mwanamke huyo alitambua kwamba Yesu alikuwa nabii hata ingawa hakuwa ametabiri kuhusu wakati ujao.—Yohana 4:17-19.
Wakati wa kesi ya Yesu, maadui wake walimfunika uso, wakampiga, kisha wakamwambia: “Toa unabii. Ni nani aliyekupiga?” Hawakuwa wakimwambia Yesu atabiri wakati ujao bali kwa msaada wa Mungu aseme ni nani aliyempiga.—Luka 22:63, 64.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW