Sunday, April 23, 2017

KAMA YESU NI MUNGU, KWANINI AZALIWE NA KUVAA MWILI WA KIBIDANAMU?

Image may contain: 2 people, text and indoor
Ndugu msomaji,
Baada ya hoja na maswali mengi tuliyokwisha yapitia juu ya uhalali wa Uungu wa Yesu ndipo swali hili hufuatia ambapo hoja ya msingi hapa ni juu ya kile kinachoonekana kama kitu kisichowezekana kwa Yesu kuwa na asili ya Uungu na huku akiwa na umbile la kibinadamu umbile ambalo alilipata kwa njia ya kuzaliwa na Mariam, na kimsingi hapa ndipo mahali maswali mengi zaidi hujitokeza.
Kwanini kama ni Mungu avae ubinadamu?
Tendo la dhambi ya Adamu na Hawa lilimuingiza mwanadamu katika deni kubwa lisiloweza kulipwa na mwanadamu mwenyewe hebu tusome:-
Mwanzo 3:17
Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.
Kwa kadri ya Andiko hilo tunasoma kuwa Mungu alipomuweka Adamu na Hawa katika bustani ya edeni aliwapa masharti yahusuyo ulaji ambapo wanadamu hao walikatazwa kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, lakini mbali na kukatazwa huko pia walionyeshwa hasara ambayo wangeipata kama matokeo ya kukaidi agizo hilo la kula matunda hayo ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya.
Kwa uwazi kabisa Mungu aliwaambia juu ya hatari hiyo ambayo wangejiingiza kwayo kuwa ilikuwa ni kifo’ (siku utakapokula utakufa hakika) kwahivyo kimsingi tendo la wazazi hao kujiingiza katika tendo hilo la dhambi ilikuwa ni sawa na kujiingiza katika deni la dhambi ambalo malipo yake ni mauti (kifo).
Na kwa hali hiyo basi mwanadamu huyu alihitaji msaada wa kunasuliwa toka katika deni hilo la dhambi, hivyo ilipasa upande wa pili unaoweza kukabili deni hilo kujitokeza ili kumsaidia mwanadamu kwakuwa kimsingi hakuna mwanadamu mwenye uwezo wa kukabili deni la kifo maana liko nje ya uwezo wa mwanadamu kama Daudi anavyoeleza:-
Zaburi 49:7-8
Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, Wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake,8 (Maana fidia ya nafsi zao ina gharama, Wala hana budi kuiacha hata milele;)
Hilo ni tamko la wazi la Biblia likibainisha kuwa kamwe mwanadamu hawezi kujiokoa au kumwokoa jirani yake kwakuwa nafsi ya mwanadamu inagharama ambayo haiwezi kulipwa na mwanadamu mwenyewe.
Hivyo kwa hali hiyo swali la msingi hapa linaloibuka ni kuwa sasa ni mamlaka gani yenye uwezo huo wa kulipa deni hilo la mauti na hivyo kumnusuru mwanadamu?. Ili kupata urahisi katika kujibu swali hili jambo la msingi hapa ni kuangalia sifa za msingi za mamlaka inayoweza kufanya kazi hiyo ambapo kimsingi sifa hizo ni lazima zihusiane na:-
- Uwezo wa kuasisi uhai (kuumba).
- Mamlaka dhidi ya kifo (mauti).
Kadiri ya sifa hizi ninaamini haitakuwa jambo la kufikiri kwa muda mrefu kuwa jukumu hili la ukombozi linaangukia kwa nani hasa kutokana na ukweli kuwa sifa hizo zote zinaonekana kwa Bwana Yesu na jambo jema ni kuwa vitabu vyote vya dini vinathibitisha ukweli huo hebu tuchunguze.
Uwezo wa kuasisi uhai (kuumba).
kwa upande wa Biblia tulishaona kupitia kitabu cha Mtume Yohana akiweka wazi kuwa Yesu (Neno) ni muumbaji wa vitu vyote…rejea Yohana 1:3 Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika.
Katika vitabu vingine vya kidini dhana ya uumbaji wa Yesu au uwezo wa kuasisi uhai huwekwa wazi ingawa kwa upande mwingine huelezwa kuwa Yesu naye aliwezeshwa na mamlaka nyingine kuwa na uwezo huo wa kuumba, hebu tulione hilo kwa upana wake katika Qur an tukufu:-
Qur-an 3:49
na atamfanya mtume kwa wana wa Israel awaambie nimekujieni na hoja kutoka kwa mola wenu ya kuwa “ninakuumbieni”katika udongo kama sura ya ndege kisha “nampulizia” mara anakuwa ndege kwa “Idhini” ya Mwenyezi Mungu …
Andiko hilo la msahafu kwanza linaweka wazi ukweli huo kuwa Bwana Yesu katika maisha yake ya utumishi aliwahi kufanya tendo hilo la kuasisi uhai kwa kuumba ndege kwa udongo na hatimaye kumpulizia pumzi ya uhai na mara ndege huyo akawa hai ambapo Qur an humalizia kwa kuonyesha kuwa alifanya hayo kwa idhini ya Mwenyezi Mungu tamko ambalo bado haliondoi uzito wa kuhusika kwa Bwana Yesu katika jukumu hilo la kuasisi viumbe linalomhusu Mwenyezi Mungu peke yake.
Tukiacha kujadili hoja hiyo inayojitokeza hapo bado wazo la msingi la Bwana Yesu kuhusika na uumbaji ndilo linalobeba msingi mzima wa aya hiyo ya Qur an kwa kuweka wazi ushiriki wake katika kazi hiyo mahsusi ya uumbaji na kwa hivyo anaingia katika sifa ya kuhusika kuasisi viumbe.
Katika hili kile kinachofanya uzito zaidi ni umaalumu wa tendo lenyewe la uumbaji ambalo kamwe Mungu hawezi kulifanya kwa kuhusisha mamlaka nyingine katika hatua nyeti za uumbaji kama tunavyosoma katika maandiko kadhaa toka vitabu vyote vya dini;-
Isaya 44:24
BWANA, Mkombozi wako, yeye aliye kuumba tumboni asema hivi, mimi ni Bwana, nifanyaye vitu vyote: nizitandazaye mbingu peke yangu: niienezaye nchi ni nani aliye pamoja nami?
Hapo Mungu mwenyewe anaonyesha jinsi tendo hilo la uumbaji lilivyo rasmi sana na yakuwa si tendo tu analoweza kuhusishwa kiumbe tu wa kawaida kushiriki mamlaka hiyo ya uasisi wa viumbe kwa kuwa kimsingi muasisi wa viumbe huwa juu ya viumbe hivyo.
Na katika kuonyesha uzito wa hilo maandiko ya msahafu tena huonyesha kuwa uumbaji ni mojawapo ya sifa muhimu inayompa Mungu vigezo na haki ya kuombwa na wanadamu katika mahitaji yao ya kilasiku, hivyo uumbaji ni ishara ya uwezo na haki ya kimamlaka ya Mungu.
Qur-an surat Al-hajj 22:73
Enyi watu! Unapigwa mfano, basi usikilizeni, hakika wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu hawawezi kuumba (hata) nzi …
Hivyo kwa muktaza huu tutakubaliana kuwa tendo hilo la Yesu kutajwa kuhusika na mamlaka ya uumbaji linampa Bwana Yesu haki ya msingi ya kustahili kuhusika na jukumu la ukombozi wa mwanadamu kwakuwa uwezo huo wa Yesu wa uumbaji unatoa picha juu ya uwezo wake hata katika jukumu la kukomboa.
Mamlaka dhidi ya Kifo (mauti).
Jambo jingine la msingi juu ya sifa za yule anayeweza kuvaa jukumu hilo la kumkomboa mwanadamu ni hili la uwezo dhidi ya nguvu ya mauti na kifo, katika hili pia tunaona jinsi Bwana Yesu anavyohusika moja kwa moja kwa kile kinachoonekana katika maandiko ya vitabu vyote yakimtaja Bwana Yesu kuwa na uwezo wa kufufua watu waliokufa ikiwa ni pamoja na yeye mwenyewe kushinda mauti na kufufuka:-
Qur-an 3:49
…Na ninawaponyesha vipofu na wenyewe mabalanga, na ninawafufua (baadhi ya) waliokufa, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu…….
Katika andiko hilo la Qur an zinatajwa sifa nyingine za Bwana Yesu kuwa pamoja na mambo sifa nyingine aliki pia alikuwa na uwezo wa kuponya vipofu na wakoma lakini zaidi sana Qur an inaweka wapi pia kuwa Bwana Yesu (Isa) alikuwa na uwezo wa kufufua watu waliokufa.
Sifa hii ya kufufua hubeba dhana nzima ya ushiriki wa Bwana Yesu katika jukumu la kubatilisha matokeo ya dhambi yanayozaa kifo na hivyo kuwa na sauti dhidi ya nguvu ya mauti kwa kuamuru kurejea kwa uhai kwa mtu aliyepoteza uhai huo.
Mkazo zaidi juu ya hili katika maandiko ya Biblia:-
Yahana 11:25
Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;
Hilo ni mojawapo kati ya matamko aliyowahi kuyatoa Bwana Yesu akionyesha mamlaka aliyonayo juu ya mauti na kwajumla Bwana Yesu anaonyesha hapo kuwa yeye ndiye mwenye dhamana na jukumu zima la kuwafufua wanadamu katika siku ya mwisho.
Kumbuka pia maandiko ya Biblia yanaweka bayana kuwa ukombozi dhidi ya hukumu ya mauti hauwezi kutolewa na mamlaka yeyote ile isipokuwa Mungu mwenyewe ndiye mwenye njia za kumnusuru mwanadamu dhidi ya mauti, tunaweza kuyasoma maneno hayo katika maandiko ya Biblia toka katika kitabu cha nabii Daudi:-
Zaburi 68:20
Mungu kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa; Na njia za kutoka mautini zina YEHOVA Bwana.
Hivyo wajibu wa kukomboa wanadamu kwa mujibu wa Biblia unatajwa kuwa ni wa kimbingu na hivyo kuhusika na Mwenyezi Mungu mwenyewe tendo ambalo linakaza wazo la ujio wa Yesu kwaajili ya ukombozi
Yesu alishuka kama mwanadamu toka asili ya Uungu ili kutukomboa’
Ninaamini kwa msingi huo wa maandiko tumepata ushahidi wa kutosha jinsi Bwana Yesu anavyostahili kuhusika na jukumu hili la ukombozi wa mwanadamu kwa kuwa kimsingi jukumu hilo la ukombozi wa mwanadamu lazima lifanywe na mtu mwenye sifa hizo mbili muhimu yaani ile ya uwezo wa kuasisi uhai pamoja na kurejesha uhai uliotoka.
Na kama hatua ya utekelezaji wa jukumu hilo ndipo ilimladhimu Bwana Yesu kufunika utukufu wa mamlaka yake ya kiungu ili kushuka na kutukomboa tendo ambalo ndilo linaibua hoja hii ya kudai kuwa Mungu hawezi kuzaliwa na kuonekana katika umbile la kibinadamu.
Lakini Katika kujibu swali hili ni vyema kwanza tujenge msingi kwa kusoma maandiko kadhaa katika mafunuo ya Biblia na hatimaye tupate maoni ya vitabu vingine ili kukaza uelewa wa mada hii nyeti.
Hebu tupitie maandiko haya yafuatayo:-
Kutoka 33:20
Kisha akasema, Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.
Katika andiko hilo la kwanza tunapata msingi wa uchambuzi wa mada hii kwa tamko hilo la Mungu akimweleza nabii Musa kuwa kamwe mwanadamu hawezi kumwona Mungu bayana akaishi.
Hivyo andiko hilo linazalisha madai muhimu kwa Mwenyezi Mungu katika jukumu lake la kushuka ili kumkomboa mwanadamu, madai ambayo yanaitaka mbingu kubuni kanuni ya kumfikia mwanadamu huyu kwa namna ambayo haitomwangamiza na badala yake kumwokoa.
Na kwa hali hiyo swali la msingi linalojitokeza hapa ni kuwa sasa’ ni kwa namna gani basi Mungu anaweza kumfikia mwanadamu huyu pasina mwanadamu huyo kuangamia kama matokeo ya kukabili uwepo wa Mungu wa ana kwa ana? Ili kujibu swali hilo nikuombe tusome maandiko haya yafuatayo:-
Ebrania 2:16-17
Maana ni hakika, hatwai asili ya malaika, ila atwaa asili ya mzao wa Ibrahimu.17Hivyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake.
Biblia hapo inatoa majibu ya swali hilo la msingi kwa kutajwa dhahili kuwa asili au hali ambayo Mungu angeitwaa katika kutekeleza jukumu hilo ni asili ya ubinadamu na pia inaeleza kuwa katika utekelezaji wa jukumu hilo ilikuwa ni lazima Yesu kuchukua hali ya mfanano na wanadamu nadipo hatimaye aweze kufanikisha jukumu hilo la kuleta suluhu ya dhambi kwa watu wake.
Kisa cha mama msamaria’
Kulikuwa na mama mmoja msamaria, mama huyu alikuwa akiishi eneo la baridi kali..siku moja alipokuwa akiota moto ndani katika nyumba yake ya vioo ndipo akaona ndege kwa nje’,ndege huyu alikuwa katika hali ya kuelekea kufa kutokana na baridi ingawa hatimaye ndege huyo alitimiza hatua ya kwanza ya furaha ya mama huyo kwa kutua kwenye mti mkubwa ulioota nje ya dirisha dogo la nyumba yake, na ndipo mama huyu akachukua mti mwingine mrefu anaoutumia kuchochea moto ndani na kuupitisha kwenye dirisha hilo ili ukaungane na ule wa nje na kutengeneza daraja na hatimaye kumwezesha ndege huyo kupita na kuingia ndani ili kujinusuru’…lakini ndege huyo alipoona mti huo ukichomoza toka kwenye dirisha hilo alihofu kwa kufikiri kuwa huenda ni mtu anayetaka kumpiga ili hatimaye kumfanya kitoweo na kwasababu hiyo ndege huyo aliruka na kutokomea kwenye baridi zaidi na hatimaye akafa huko’
Tamko la mama msamaria, alibaki kusema:- Laiti kama ningelikuwa na uwezo wa kujimithilisha’ nikawa mfano wa yule ndege’ ningelimsogelea na kumwambia’ ndege wenzangu eeeeh twende mule ndani tujinusuru na baridi!!!!!!
Kisa hicho kinaweka mkazo na kutoa mwangaza juu umuhimu wa tendo hilo la Bwana Yesu kuvaa umbile la kibinadamu katika harakati za kumfikia na kumwokoa mwanadamu, ambapo tunaona jinsi ambavyo haikuwa rahisi kwa mama msamaria kufanikisha dhamili yake ya kumwokoa yule ndege kwa njia ya kutumia mti ambao kimsingi kwa ndege huyo ulikuwa ni kitisho.
Kumbuka kuwa endapo Bwana Yesu angelikuja katika halihalisi ya utumkufu wake wa Kimungu wanadamu wangelihofu na kuangamia kama ambavyo tunaweza kuliona hilo katika mifano kadhaa ya matukio katika Biblia, soma historia hii ya kipindi cha wana wa Israel kwa utulivu:-
Kutoka 19:11-12
wawe tayari kwa siku ya tatu; maana siku ya tatu Bwana atashuka katika mlima wa Sinai machoni pa watu hawa wote17 Musa akawatoa hao watu katika kituo, akawaleta ili waonane na Mungu; wakasimama pande za chini za kile kilima. 18 Mlima wa Sinai wote pia ukatoa moshi, kwa sababu Bwana alishuka katika moto; na ule moshi wake ukapanda juu kama moshi wa tanuu, mlima wote ukatetemeka sana.19 Na hapo sauti ya baragumu ilipozidi kulia sana, Musa akanena, naye Mungu akamwitikia kwa sauti.20 Bwana akaushukia mlima, juu ya kilele cha mlima; Bwana akamwita Musa aende hata kilele cha mlima; Musa akapanda juu. 21 Ndipo Bwana akamwambia Musa, Shuka chini, uwaonye watu wasije wakapasua njia waje kwa Bwana kutazama,kisha wengi miongoni mwao wakaangamia.
Katika andiko hilo tunaona historia hiyo ya kile kilichowapata wana wa Israel ambao kimsingi walitoa madai ya kutaka kuonana na Mungu, na katika tukio hilo la kushuka kwa Mwenyezi Mungu ili kujifunua kwao wa Israel wengi walikufa kutokana na Mungu huyo kuja katika hali ambayo hawakuweza kuikabili.
Swali! Je’ Mungu aje katika hali gani ili mwadamu aweze kuikabili?
- Aje katika hali ya ng’ombe!
- Au aje katika hali ya simba! Au hali gani?
Biblia inataja namna Mungu alivyojidhihirisha kwa Kristo katika hali ambayo mwanadamu aliweza kuikabili.
1Timotheo 3:16
Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu. Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu.
Hivyo maandiko hayo ya Biblia yantaja njia hiyo ambayo Mungu aliitumia kujidhihirisha kwa wanadamu yaani kwa kutwaa mwili wa kibinadamu ingawa haki yake ilijulikana katika ulimwengu wa roho.
Maelezo ya vitabu vingine, je’ Mungu anaweza kuja katika maumbile tofauti?
Kabla ya kuhitimisha kipengele hiki ni vyema tukapata kwanza maoni toka katika vitabu vingine vya kidini ili kukaza uelewa wa uchambuzi huu na pengine kufungua zaidi ufahamu wa masomaji wangu ikiwa huenda si Mkristo.
Katika hatua ya awali maandiko ya msahafu wa Qur an yanataja sifa za Mwenyezi ambazo zitaanza kutujengea msingi wa uchambuzi katika kipengele hiki:-
Qur an 57:3
Yeye ndiye wa Mwanzo na ndiye wa Mwisho, Naye ndiye wa Dhahiri na wa Siri, naye ndiye Mjuzi wa kilakitu.
Andiko hilo linataja sifa hizo za msingi za Mungu ambapo moja ya sifa hizo ni ile Dhahiri na Siri, kupitia sifa hizi tunapata uthibitisho wa dhana nzima ya utendaji wa Mwenyezi Mungu katika hali mbalimbali yaani kwanza katika hali yake ya kutoonekana (Siri) na ile ya kujifunua Dhahiri na jambo la kufurahisha zaidi ni kuwa maandiko ya Qur an tukufu yameweka mifano muhimu juu ya aina zote hizi za mifumo ya utendaji wa Mwenyezi Mungu ambapo kwa mfano ile hali ya dhahiri inaonekana katika kisa cha nabii Musa kama tunavyosoma:-
Qur an 20:9-12
Na je imekujia hadithi ya Musa? 10’alipouona moto, akawaambia watu wake (aliokuwa nao) “Ngojeni, hakika nimeuona moto, huenda nikakuleteeni kijinga katika huo (moto)au nitapata mwongozaji katika moto huo (wakutuonyesha njia).11’ Basi alipofika akaitwa “Ewe Musa! 12’”Bilashaka Mimi ndiye Mola wako.Basi vua viatu vyako.hakika wewe uko katika bonde takatifu la Tuwa.
Hapo tunaona katika kisa hicho cha Nabii Musa kutokewa Mungu anajifunua kwa Musa kupitia kichaka cha moto ambapo Musa kwa kutojua anadhani hicho ni kichaka cha moto wa kawaidia tu na kumbe kichaka hicho kilikuja na uwepo wa Mungu, hivyo Musa kwa kukiona kichaka hicho alipaswa kukubali kuwa hapo alikutana na Mungu bayana. Rejea tamko la Mungu mwenyewe’ “Bilashaka mimi ndiye Mola wako”.
Shalom.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW