Monday, April 24, 2017

NABII ALIYE KAMA MUSA NI NANI?


▲ Musa na Yesu waliokoka mauaji ya watoto wavulana yaliyoamriwa na watawala wa wakati wao.—Kutoka 1:22; 2:1-10; Mathayo 2:13-18.
▲ Musa aliitwa kutoka Misri pamoja na ‘mzaliwa wa kwanza’ wa Yehova, taifa la Israeli. Yesu aliitwa kutoka Misri akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu.—Kutoka 4:22, 23; Hosea 11:1; Mathayo 2:15, 19-21.
▲ Musa na Yesu walifunga kula kwa siku 40 nyikani.—Kutoka 34:28; Mathayo 4:1, 2.
▲ Musa na Yesu walikuwa watu wapole na wanyenyekevu zaidi.—Hesabu 12:3; Mathayo 11:28-30.
▲ Musa na Yesu walifanya miujiza. —Kutoka 14:21-31; Zaburi 78:12-54; Mathayo 11:5; Marko 5:38-43; Luka 7:11-15, 18-23.
▲ Musa na Yesu walikuwa wapatanishi wa maagano kati ya Mungu na watu Wake.—Kutoka 24:3-8; 1 Timotheo 2:5, 6; Waebrania 8:10-13; 12:24.
Tunaishi nyakati za taabu. Wanadamu wanahitaji kiongozi aliye kama Musa—mtu aliye na uwezo na mamlaka na anayeshikamana na kanuni za maadili, kiongozi jasiri, mwenye huruma, na anayependa sana haki. Musa alipokufa, huenda Waisraeli walijiuliza, ‘Je, ulimwengu utamwona mtu kama yeye tena?’ Musa mwenyewe alijibu swali hilo.
Maandishi ya Musa yanaeleza jinsi magonjwa na kifo yalivyotokea na kwa nini Mungu ameruhusu uovu. (Mwanzo 3:1-19; Ayubu, sura ya 1, 2) Unabii wa kwanza wa Mungu unaopatikana katika Mwanzo 3:15, unaahidi kwamba uovu utakomeshwa hatimaye! Jinsi gani? Unabii huo ulionyesha kwamba mtu fulani angezaliwa ambaye angeleta wokovu. Ahadi hiyo iliwafanya watu wawe na tumaini kwamba Masihi angetokea na kuwakomboa wanadamu. Lakini Masihi huyo angekuwa nani? Musa anatusaidia kumtambua waziwazi.
Alipokaribia kufa, Musa aliandika maneno haya ya kinabii: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kumbukumbu la Torati 18:15) Baadaye mtume Petro alionyesha waziwazi kwamba maneno hayo yanamhusu Yesu.—Matendo 3:20-26.
Wasomi wengi Wayahudi wanapinga vikali uhusiano kati ya Musa na Yesu. Wanadai kwamba maneno hayo yanamhusu nabii yeyote wa kweli aliyetokea baada ya Musa. Hata hivyo, kulingana na Tanakh—The Holy Scriptures cha Jewish Publication Society, andiko la Kumbukumbu la Torati 34:10 linasema: “Hapakuinuka tena kamwe katika Israeli nabii kama Musa—ambaye BWANA aliteua, uso kwa uso.”
Naam, manabii wengi waaminifu kama vile Isaya na Yeremia, walitokea baada ya Musa. Lakini hakuna yeyote kati yao aliyekuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Mungu kama vile Musa, yaani kuzungumza naye “uso kwa uso.” Kwa hiyo ahadi ya Musa kuhusu nabii aliye ‘kama yeye’ ilimhusu mtu mmoja, yaani, Masihi! Inapendeza kwamba kabla ya Ukristo kuanzishwa na kabla ya mnyanyaso wa kidini kutoka kwa Wakristo wa uwongo, wasomi Wayahudi walikuwa na maoni hayohayo. Uthibitisho wa hilo unapatikana katika maandishi ya Kiyahudi kama vile kitabu Midrash Rabbah, kinachomtaja Musa kuwa mtangulizi wa “Mkombozi wa baadaye,” au Masihi.
Uhakika wa kwamba Yesu alikuwa kama Musa hauwezi kukanushwa. (Ona sanduku “Yesu Alikuwa Nabii Kama Musa.”) Yesu ana nguvu na mamlaka. (Mathayo 28:19) Yesu ni “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.” (Mathayo 11:29) Yesu anachukia uasi-sheria na ukosefu wa haki. (Waebrania 1:9) Basi anaweza kutuongoza vizuri sana! Yeye ndiye atakayekomesha uovu hivi karibuni na kufanya dunia iwe Paradiso ambayo Biblia inazungumzia.*
USIKOSE MADA YA "NABII YULE NI NANI?"
Shalom
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW