Saturday, April 15, 2017

UFUFUO WA YESU KRISTO


HOSANA: YESU AMEFUFUKA
UFUFUO WA YESU KRISTO
Ufufuo wa Yesu uliwatia moyo sana wanafunzi wake. Hakuwa mfu kama maadui zake walivyoamini. Yesu alikuwa hai akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu ambaye hakuna mwanadamu angeweza kumdhuru. Ufufuo wake ulithibitisha kwamba alikuwa Mwana wa Mungu na Mungu, na kujua jambo hilo kuliwatia moyo wanafunzi wake, wakawa na shangwe kubwa badala ya huzuni. Na pia wakawa na ujasiri badala ya hofu. Ufufuo wa Yesu ulikuwa muhimu sana katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu na ulikuwa msingi wa habari njema waliyohubiri kwa ujasiri kotekote.
Mitume walijua kwamba ufufuo wa Yesu ulikuwa tofauti na ufufuo wowote uliotangulia. Watu waliofufuliwa mapema walifufuliwa wakiwa na miili ya kibinadamu na hatimaye walikufa tena. Yesu alifufuliwa akiwa na mwili wa roho ambao haungeweza kuharibika. (Soma Matendo 13:34.) Petro aliandika kwamba Yesu “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” Zaidi ya hayo, “yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Petro 3:18-22) Ufufuo wowote uliotangulia ufufuo wa Yesu ulikuwa muujiza wenye kustaajabisha, lakini ufufuo wa Yesu ulikuwa muujiza mkubwa hata zaidi.
TUNAJUAJE KWAMBA YESU ALIFUFULIWA?
Ufufuo wa Yesu ulitokeaje “kulingana na Maandiko”?
Kwanza, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu ufufuo wake ulitokea “kulingana na Maandiko.” Neno la Mungu lilitabiri ufufuo huo. Kwa mfano, Daudi aliandika kwamba mtumishi “mshikamanifu” zaidi wa Mungu hataachwa katika Kaburi. (Soma Zaburi 16:10.) Katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., mtume Petro alionyesha kwamba maneno hayo ya kinabii yalimhusu Yesu. Alisema hivi: “[Daudi] aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi wala mwili wake haukuona uharibifu.”—Matendo 2:23-27, 31.
Pili, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu tuna ushuhuda wa mashahidi wengi. Kwa siku 40, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake katika bustani ambamo kaburi lake lilikuwa, na pia aliwatokea njiani wakielekea Emau, na wakiwa sehemu nyingine. (Luka 24:13-15) Katika pindi hizo, aliongea na mtu mmoja-mmoja kutia ndani Petro, na pia aliongea na vikundi vya watu. Hata pindi fulani, Yesu aliyefufuliwa alitokea umati wa watu zaidi ya 500! Ushuhuda wa mashahidi wengi hivyo waliomwona Yesu aliyefufuliwa hauwezi kukanushwa.
Tatu, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu wanafunzi wake walitangaza ufufuo wake kwa bidii. Walinyanyaswa, wakateswa, na kuuawa kwa sababu ya kutangaza kwa bidii ufufuo wa Kristo. Kama Yesu hangekuwa amefufuliwa, yaani, ikiwa huo ulikuwa uwongo, kwanini Petro alihatarisha uhai wake kwa kuwatangazia viongozi wa kidini kuhusu ufufuo wa Kristo ilhali viongozi hao walimchukia Yesu na kupanga njama auawe? Kwa sababu Petro na wanafunzi wengine walikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa hai na alikuwa akiongoza kazi ambayo Mungu alitaka ifanywe. Isitoshe, ufufuo wa Yesu uliwahakikishia wafuasi wake kwamba wao pia wangefufuliwa. Kwa mfano, Stefano alikufa akiwa na uhakika kwamba wafu watafufuliwa.—Matendo. 7:55-60.
Ufufuo wa Kristo unatupatia ujasiri wa kuhubiri. Kwa miaka 2,000, maadui wa Mungu wametumia kila aina ya silaha kukomesha kazi ya kuhubiri habari njema—wametumia uasi-imani, dhihaka, vikundi vyenye ghasia, marufuku, mateso, na kuwaua watumishi wa Mungu. Hata hivyo, hakuna chochote, yaani, hakuna ‘silaha yoyote iliyofanywa juu yetu’ imekomesha kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. (Isaya 54:17) Hatuwaogopi watumishi au watumwa wa Shetani. Yesu yuko pamoja nasi, na anatusaidia kama alivyoahidi. (Mathayo 28:20) Hatuna sababu yoyote ya kuogopa kwa kuwa hata adui zetu wafanye nini, hawataweza kamwe kutunyamazisha!
Yesu alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima. Yule anayeniamini, hata akifa, atarudi kwenye uzima.” (Yohana 11:25) Kwa hakika, maneno hayo yenye kusisimua yatatimia. Yesu ana Mamlaka yote Mbinguni na Duniani ya kuwafufua wale wanaopata uhai wa kiroho mbinguni, na pia kuwafufua mabilioni ya watu wanaotumaini kuishi milele. Dhabihu ya Yesu inayofunika dhambi na pia ufufuo wake unatuhakikishia kwamba kifo hakitakuwapo tena. Je, kujua mambo hayo hakukupi nguvu za kuvumilia jaribu lolote lile na hata kukabili kifo kwa ujasiri?
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW