Sunday, April 23, 2017

TUMIA VIZURI ULIMI WAKO


Kuzungumza ni sehemu ya kawaida ya maisha yetu ya kila siku, hata hivyo hatuhitaji kuongea kila wakati. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya.” (Mhubiri 3:7) Kukaa kimya wengine wanapozungumza kunaweza kuwa ishara ya heshima. (Ayubu 6:24) Kudhibiti ulimi wetu ili tusiseme mambo ya siri ya wengine kunaonyesha kwamba tuna busara na utambuzi. (Met. 20:19) Isitoshe, ni jambo la hekima kuzuia ulimi wetu tunapokasirishwa.—Zaburi 4:4.
“Maneno ya kinywa changu . . . na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova.”—Zaburi 19:14.
Maneno yana nguvu za kuumiza na kuponya. (Soma Methali 12:18.) Kutumia maneno yanayoumiza ni jambo la kawaida katika ulimwengu wa Shetani. Leo, burudani nyingi huwachochea watu ‘kunoa ulimi wao kama upanga’ na kufyatua ‘maneno machungu kama mishale.’ (Zaburi 64:3) Mkristo anapaswa kuepuka mazoea hayo hatari. Mfano mmoja wa “maneno machungu” ni kejeli, yaani maneno yaliyokusudiwa kuwadhalilisha au kuwashutumu wengine. Mara nyingi kejeli huanza kama ucheshi, lakini inaweza kugeuka haraka na kuwa maneno yasiyo ya heshima au matusi. Kejeli zenye kuumiza ni mojawapo ya matukano ambayo Wakristo wanapaswa ‘kuyaondolea mbali.’ Ucheshi unaweza kufanya mazungumzo yawe yenye kufurahisha. Hata hivyo, tunahitaji kuepuka mtego wa kuwachekesha watu kwa kutumia maneno yasiyofaa au kebehi ambazo zitawaumiza au kuwadhalilisha wengine. Biblia inatuhimiza hivi: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.”—Efeso 4:29, 31.
Yesu alifundisha kwamba “kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Hivyo, kuchagua maneno yanayofaa huanzia moyoni. Kwa kawaida, maneno yetu hufunua hisia zetu kuelekea watu wengine. Ikiwa kweli tunawapenda na kuwajali watu, yaelekea tutazungumza mambo yanayofaa na yanayowajenga wengine.
Shalom,
Max Shimba mtumwa wa Yesu Kristo.

No comments:

FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE

  **URGENT UPDATE**   **FORMER MUSLIM EVANGELIST MUSA BELLO ARRESTED BY NIGERIAN POLICE** Shimba TV, New York has received distressing news ...

TRENDING NOW